Business

Biashara ya Viazi Vitamu Yaendelea Kunga’ara Mjini Kilifi Licha ya Changamoto za Usafiri

Published

on

Kilifi, Kenya – Wachuuzi wa viazi vitamu katika barabara ya mjini Kilifi wameripoti kuimarika kwa biashara hiyo ikilinganishwa na vipindi vya nyuma, wakisema hali hiyo imesababishwa na upatikanaji wa bidhaa hiyo kwa wingi kutoka mashambani.

Akizungumza na wanahabari, Joyce Kemboi, ambaye ni mmoja wa wachuuzi wa viazi vitamu katika eneo hilo, amesema kuwa kwa sasa wakulima wanavuna kwa wingi kutokana na hali nzuri ya mvua ambayo imeimarisha uzalishaji mashambani.

“Kwa sasa viazi vitamu vinapatikana kwa wingi sana, na hii imetuwezesha kufanya biashara nzuri. Wateja pia wameongezeka kwa sababu bidhaa ni safi na za bei nafuu,” amesema Kemboi.

Hata hivyo, licha ya mafanikio hayo, wachuuzi hao wanakabiliwa na changamoto ya gharama ya juu ya usafiri, hali inayochangiwa na kuharibika kwa barabara nyingi kufuatia mvua kubwa inayoendelea kunyesha katika maeneo mengi ya nchi.

Kemboi anasema kuwa usafirishaji wa viazi kutoka mashambani hadi sokoni umekuwa ghali mno, jambo ambalo linaathiri faida ya wachuuzi wa kiwango cha chini.

“Gharama ya kusafirisha gunia moja imepanda. Barabara nyingi zimeharibika, magari hayafiki kwa urahisi, na tunalazimika kutumia njia mbadala ambazo ni ghali,” ameongeza.

Kwa sasa, gunia la kilo 90 la viazi vitamu linauzwa kwa shilingi elfu 10, bei ambayo ni ya juu ikilinganishwa na msimu wa kiangazi ambapo gunia hilo hilo lingeuzwa kwa kati ya shilingi elfu 6 hadi 7.

Licha ya bei hiyo kupanda, wachuuzi wana matumaini kuwa soko litaendelea kuboreka hasa kwa kuwa bidhaa hiyo ina uhitaji mkubwa kwa wateja wa kila tabaka.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Trending

Exit mobile version