Business
Biashara ya Viazi Vitamu Yaendelea Kunga’ara Mjini Kilifi Licha ya Changamoto za Usafiri

Kilifi, Kenya – Wachuuzi wa viazi vitamu katika barabara ya mjini Kilifi wameripoti kuimarika kwa biashara hiyo ikilinganishwa na vipindi vya nyuma, wakisema hali hiyo imesababishwa na upatikanaji wa bidhaa hiyo kwa wingi kutoka mashambani.
Akizungumza na wanahabari, Joyce Kemboi, ambaye ni mmoja wa wachuuzi wa viazi vitamu katika eneo hilo, amesema kuwa kwa sasa wakulima wanavuna kwa wingi kutokana na hali nzuri ya mvua ambayo imeimarisha uzalishaji mashambani.
“Kwa sasa viazi vitamu vinapatikana kwa wingi sana, na hii imetuwezesha kufanya biashara nzuri. Wateja pia wameongezeka kwa sababu bidhaa ni safi na za bei nafuu,” amesema Kemboi.
Hata hivyo, licha ya mafanikio hayo, wachuuzi hao wanakabiliwa na changamoto ya gharama ya juu ya usafiri, hali inayochangiwa na kuharibika kwa barabara nyingi kufuatia mvua kubwa inayoendelea kunyesha katika maeneo mengi ya nchi.
Kemboi anasema kuwa usafirishaji wa viazi kutoka mashambani hadi sokoni umekuwa ghali mno, jambo ambalo linaathiri faida ya wachuuzi wa kiwango cha chini.
“Gharama ya kusafirisha gunia moja imepanda. Barabara nyingi zimeharibika, magari hayafiki kwa urahisi, na tunalazimika kutumia njia mbadala ambazo ni ghali,” ameongeza.
Kwa sasa, gunia la kilo 90 la viazi vitamu linauzwa kwa shilingi elfu 10, bei ambayo ni ya juu ikilinganishwa na msimu wa kiangazi ambapo gunia hilo hilo lingeuzwa kwa kati ya shilingi elfu 6 hadi 7.
Licha ya bei hiyo kupanda, wachuuzi wana matumaini kuwa soko litaendelea kuboreka hasa kwa kuwa bidhaa hiyo ina uhitaji mkubwa kwa wateja wa kila tabaka.
Business
Wakaazi wahofia mkurupuko wa magonjwa baada ya kuuziwa nyama Malindi

Wakaazi wa mji wa Malindi kaunti ya Kilifi wanaishi kwa hofu ya mkurupuko wa magonjwa baada ya kulalamikia kuuziwa nyama ya mifugo ambayo haijakaguliwa na maafisa wa mifugo eneo hilo.
Wakielezea manung’uniko yao, wakaazi hao walioongozwa na Kensa Ondiek walisema nyama ya mifugo inayouzwa eneo hilo haijakaguliwa, akiongeza kwamba kichinjio cha kipekee mjini humo pia kina wafanyikazi ambao ni wa umri wa chini ya miaka kumi na nane.
Wakaazi hao pia walisema mazingira ya kufanya kazi katika kichinjio hicho nai ya kutatanisha huku wachuuzi wa nyama wakifanya biashara zao mahali peupe na pachafu.
Vyombo vya Habari vilidhibitisha matukio hayo kupitia picha za watoto wakifanya kazi katika kichinjio hicho na kuchinjwa kwa mifugo siku ya Jumapili.
Afisa wa mifugo eneo la Malindi Godreck Mwaringa alitetea madai hayo akisema kwamba mifugo inayochinjwa katika kichinjio hicho hukaguliwa pindi inapofika, kabla na baada ya kuchinjwa.
Aliongezea kwamba maafisa husika hufanya kazi kuanzia siku ya Jumatatu hadi Jumamosi, japo akaweka wazi kwamba huenda wanaochinjwa siku ya Jumapili huwa ni uchinjaji wa dharura ambao pia nyama yake inafaa kukaguliwa kabla ya kuuzwa.
Hata hivyo alitoa tahadhari kwa wakazi wa Malindi kuhakikisha wananunua nyama iliyokaguliwa huku akionya kuwa watakaopatikana na mifugo wala nyama ambayo hazijakaguliwa watashtakiwa.
Taarifa ya Eric Ponda
Business
Biashara ya sare za shule imedidimia Kilifi

Wafanyibiashara wa kuuza sare za shule mjini Kilifi wamesema kuwa biashara hiyo iko chini msimu huu ikilinganishwa na wakati ambapo wanafunzi wakifungua shule mwezi wa kwanza.
Wakizungumza na cocofm wafanyibiashara hao walisema kuwa kwa sasa wazazi wengi hawanunui sare za shule kwa wingi ikilinganishwa na wakati ambapo shule zilikuwa zinafunguliwa kwa muhula wa kwanza.
Hata hivyo gharama ya juu ya maisha pia imetajwa kuchangia kudorora kwa biashara hiyo kwani wengi walilalamikia ukosefu wa fedha.
Walisema wanatarajia biashara hiyo kuimarika tena msimu ujao huku wakitoa wito kwa serikali kuu kuzingatia upya swala la kupanda kwa gharama ya maisha.
Taarifa ya Pauline Mwango