Mshikilizi wa rekodi ya taifa ya mbio za mita 400, Mercy Oketch, amesema atatumia vyema faida ya kushindania nyumbani anapojiandaa kushiriki tena katika mashindano makubwa ya Kip Keino Classic yatakayofanyika Nairobi Ijumaa hii.
Mshikiliaji huyo wa rekodi ya kitaifa anasema kushindana mbele ya mashabiki wa nyumbani humtia hamasa na kumpa faraja zaidi ikilinganishwa na kushindana nje ya nchi, ambako wanariadha mara nyingi hukumbana na upweke.
“Kushindana hapa, kila mtu anakusapoti na kukushangilia. Nafikiri ni bora kuliko kushindana nje,” alisema Oketch. “Nje ya nchi, uko peke yako, hakuna mtu wa kukusaidia. Lakini hapa Kenya, watu watakuwa wakitushangilia.”
Oketch anaingia katika makala ya mwaka huu kama bingwa mtetezi wa mbio za mita 400 kwa wanawake katika Kip Keino Classic, ushindi uliothibitisha kuongezeka kwa umaarufu wake katika mashindano ya bara na kuonyesha kupanda kwake kwa kasi katika mbio fupi.
Anashikilia rekodi ya taifa katika mita 400 za ndani na nje na amekuwa akijijengea uzoefu hatua kwa hatua katika ulingo wa kimataifa kupitia mashindano makubwa na mikutano ya wanariadha wa kiwango cha juu.
Anapojiandaa kutetea taji lake, Oketch anasema amekuwa akizingatia maeneo muhimu ya kiufundi ya mbio zake ili kuboresha kiwango chake.
“Nimefanyia kazi kuanza kwangu na kumalizia mbio,” alieleza. “Natumaini mashindano haya yatakuwa mazuri, na nitafanya kila niwezalo.”
Mtaalamu wa mita 400 ametilia mkazo mkubwa katika utekelezaji wa mbio, hasa kuboresha sehemu ya mwanzo na kudumisha nguvu katika sehemu ya mwisho vipengele muhimu katika mbio ambazo mara nyingi huamuliwa katika mita 100 za mwisho.
Mashindano ya Kip Keino Classic, ambayo ni sehemu ya mfululizo wa World Athletics Continental Tour Gold, yanaendelea kuwapa wanariadha wa Kenya fursa adimu ya kushindana dhidi ya wapinzani wa kiwango cha dunia wakiwa nyumbani huku wakipima maendeleo yao katika jukwaa la kimataifa.
