News
Viongozi wa kisiasa wampigia debe Joho kuwa Kiongozi wa Pwani
Baadhi ya viongozi wa kisiasa kaunti ya Mombasa wanaendelea kumpigia debe Waziri wa madini na uchumi wa bahari na maziwa nchini, Ali Hassan Joho kuwa Kiongozi wa Pwani, ambaye atapeperusha bendera ya urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka wa 2032.
Viongozi hao wakiongozwa na Mwakilishi wa kike kaunti ya Mombasa Zamzam Mohamed wamesema Waziri Joho ana uwezo mkubwa wa kuliunganisha eneo la Pwani ili liweze kunufaika kimaendeleo kama maeneo mengine nchini.
“Leo rais ametutunuku, ametupatia Hassan Ali Joho kama Waziri wa Blue Economy ambayo inahusu kaunti zetu, na Waziri Hassan Joho anachapa kazi, kwa hivyo safari yetu sisi tumeianza’’, alisema Zamzam.
Zamzam alisema Joho amekuwa kwenye siasa kwa miaka mingi na ana uzoefu katika uongozi, hivyo basi anapaswa kupeperusha bendera hiyo.
Ni kauli ambayo imeunga mkono na Mbunge wa Jomvu Badi Twalib ambaye amesisitiza ushirikiano baina ya viongozi ili kuhakikisha malengo hayo yanaafikiwa ipasavyo.
Naye Mbunge wa Kisauni Rashid Bedzimba alisema maeneo mengine ya nchi yanajiandaa kuwa na kiongozi ambaye ataliongoza taifa hili na kusisitiza umuhimu wa Wapwani kushirikiana ili Joho aweze kuwa rais wa taifa hili mwaka wa 2032.
Taarifa ya Janet Mumbi