Mboga Imejileta; Arrow Bwoy Aitisha Pigano Dhidi ya Shakib

Mboga Imejileta; Arrow Bwoy Aitisha Pigano Dhidi ya Shakib

Msanii maarufu wa Kenya, Arrow Bwoy, amezua gumzo mtandaoni baada ya kumualika wazi wazi mfanyabiashara kutoka Uganda, Shakib Cham, kwenye pambano la ndondi.

Hii imekuja baada ya kipigo cha hadharani ambacho Shakib alipokea kutoka kwa msanii mwenzake wa Uganda, Rickman, hali iliyoacha mashabiki wengi wakisema: “Sasa ata Arrow Bwoy anaweza!”

Kupitia video inayosambaa kwenye mitandao ya kijamii, Arrow Bwoy, anayefahamika kwa vibao kama Digi Digi, hakuonyesha woga wowote. Kwa ucheshi, alisema amekuwa akisubiri nafasi kama hii kwa muda mrefu.

“Mboga imejileta,” alisema kwa kujiamini, akimaanisha kuwa Shakib amejileta mwenyewe kwenye kipigo.

“Chakula kiko tayari. Niko tayari kwa pambano hili.”

Arrow Bwoy pia hakusita kumtaja mke wa Shakib, Zari Hassan, akimtaka akae mbali na ulingo siku ya pambano hilo kwa usalama wake binafsi.

“Zari, usijisumbue kuja. Hii si sehemu ya wanawake. Usije ukazimia tukapata janga la pili,” alisema kwa kejeli.

Hata hivyo, wakosoaji wake walikumbusha jamii kuhusu video za awali zinazoonyesha Arrow Bwoy akichapwa na polisi wakati wa maandamano ya kupinga mswada wa fedha. Swali likabaki: Je, kweli ana uwezo wa kumpiga Shakib au ni porojo za mitandaoni?

Kwa jina la Zari kuingizwa kwenye sakata hili, mvutano umeongezeka na mashabiki kote Afrika Mashariki wanasubiri kuona kama Shakib atakubali changamoto hii ya kihistoria.

“Zari, kama unasikia, mtume tu kijana wako aje achukue kichapo — kichapo cha kimataifa,” Arrow Bwoy alimalizia kwa msisitizo.

Kwa sasa, macho yote yako kwa Shakib. Je, atakubali changamoto hii na kuweka historia mpya ya burudani Afrika Mashariki?