Gavana wa kaunti ya Kirinyaga Ann Waiguru ameomba msamaha kwa niaba ya serikali kwa wakaazi wa Mlima Kenya kufuatia kubanduliwa mamlakani kwa aliyekuwa naibu rais Rigathi Gachagua mwaka 2024.
Waiguru amejitenga na mchakato wa kumbandua mamlakani kwa Righadhi Gachagua akidai hakuhusika katika hatua hiyo kwani haikuhusisha uongozi wa serikali za kaunti.
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mradi wa maji wa shilingi milioni 200 katika eneo la Mwea, Waiguru ameomba wakaazi kupokea msamaha wake pamoja na ule wa serikali na kuungana katika kumuunga mkono rais William Ruto katika uchaguzi mkuu ujao.
‘Najua mliskia uchungu, kwa sababu nimewaskiza siwezi sema sijaskia vile mnasema, mimi naishi huku lakini huo uchungu usiwe ndio unatutengenisha miaka ishirini ambayo inakuja, mimi ndio nimesema nijitolee hata kama sikuweko, mimi ni serikali ya kaunti, sisi tulikuwa huku mashinani.’’ alisema Waiguru.
Gavana huyo alisema licha ya hasira na msukosuko wa kisiasa unaoshuhudiwa katika eneo hilo, wakaazi hawapaswa kufanya maamuzi ya kumkataa rais William Ruto kwa misingi ya hasira bali wanapaswa kufanya maamuzi ya kisiasa kwa busara.
‘Maneno yalikuwa kule bunge, lakini mimi nasema kama mlikosewa sana kwa sababu mimi niko kwa hii serikali basi kwa jumla wacha niseme pole sana, pokeeni pole zangu’’ aliongeza Waiguru.
Taarifa ya Joseph Jira
