Mkurugenzi wa KPA Kapteni William anusurika kwenye ajali ya barabarani

Mkurugenzi wa KPA Kapteni William anusurika kwenye ajali ya barabarani

Afisa mkuu mtendaji wa Mamlaka ya Bandari nchini (KPA) Kapteni William Ruto, amenusurika baada ya kuhusika kwa ajali mbaya ya barabarani iliyosababisha kifo cha binti yake, huku wanafamilia wengine wakinusurika na kupokea matibabu.

Katika taarifa iliyotolewa na Mamlaka ya KPA ilisema ajali hiyo ilitokea siku ya Ijumaa jioni alipokuwa akisafiri pamoja na familia yake, na kuthibitisha kuwa binti yake alifariki dunia huku wengine wakinusurika katika ajali hiyo.

Mamlaka hiyo ilieleza kuwa Kapteni Ruto na familia yake wako katika hali thabiti na chini ya uangalizi wa karibu wa madaktari, na ikaeleza matumaini ya kupona kwa haraka na kikamilifu kutokana na majeraha waliyopata.

“Tunasikitika sana kwa msiba huu mzito na tunatoa pole zetu za dhati kwa Kapteni Ruto na familia yake katika kipindi hiki kigumu,” ilisema Idara ya Mawasiliano ya KPA.

Mamlaka hiyo iliomba familia hiyo ipewe faragha wakati huu wa maombolezo, ikiwahimiza umma na vyombo vya habari kuheshimu nafasi yao wanapokabiliana na msiba huo.

Ilitambua msaada kutoka kwa Gavana wa Mombasa Abdulswamad Shariff Nassir na Gavana wa Taita Taveta Andrew Mwadime kwa msaada wao wa haraka kufuatia ajali hiyo.

Idara hiyo pia iliwashukuru wafanyakazi, washirika, wadau na umma kwa msaada wao, uvumilivu na ushirikiano wao wakati wa tukio hilo na mchakato wa kupona.

KPA ilisema inaendelea kushirikiana na mashirika husika kubaini chanzo na mazingira ya ajali hiyo na itatoa taarifa zaidi kadri maelezo zaidi yatakavyopatikana.

Taarifa ya Mwahoka Mtsumi