News
Waziri Ruku, aunga mkono mswada tata wa kuzuia maandamano

Waziri wa utumishi wa umma nchini Geoffrey Ruku ameendelea kuunga mkono mswada tata wa kudhibiti mikutano na maandamano wa mwaka 2024.
Mswada huo, ambao kwa mara ya kwanza uliwasilishwa na Ruku wakati alipokuwa Mbunge wa Mbeere Kaskazini, umeibuka tena wakati huu ambapo maandamano yanayoongozwa na vijana wa kizazi cha Gen Z yanaendelea kushika kasi kote nchini.
Maandamano haya yameibua hisia kali huku vijana wakiibua masuala ya haki za binadamu, uwajibikaji wa serikali, na mustakabali wa taifa.
Waziri Ruku alitetea mswada huo, akisema kwamba mfumo wa sasa wa kisheria kuhusu mikutano na maandamano hauna nguvu za kutosha kudhibiti maandamano ya vurugu na ghasia kwani maandamano ambayo yamekuwa yakifanyika nchini yamekosa mwelekeo na uongozi thabaiti.
“Sheria ya umma ya mwaka 1952 ni ya zamani sana. Haikutungwa kwa ajili ya Kenya ya kidemokrasia na kwamba sheria mpya itanyamazisha wakenya kwa vurugu na kuwezesha maandamano ya amani, alisema Ruku.
Kulingana na Waziri huyo, mswada mpya unapendekeza kufutwa kwa sehemu ya 5 na 6 ya sheria ya agizo la umma na badala yake kuanzisha mfumo mpya wa kusimamia maandamano na mikutano ya hadhara.
Kwa mujibu wa mapendekezo ya sheria hiyo, waandamanaji watalazimika kutoa taarifa kwa polisi kati ya siku 3 hadi 14 kabla ya kufanyika kwa mkutano au maandamano yoyote.
Hata hivyo, wachanganuzi wa masuala ya kisiasa pamoja na Wanaharakati wa kutetea haki za kibinadamu wamekosoa vikali mswada huo, wakisema ni njama fiche ya kuzuia sauti za wananchi, hasa vijana wa kizazi cha Gen Z.
Wakosoaji hao walisema mswada huo mpya unaweza kuibua masharti magumu zaidi kwa umma kuandamana kwa amani na kwamba kuhatarisha haki ya msingi ya kujieleza na kukusanyika kwa amani.
Mswada huo unalenga kuchukua mkondo mpya baada ya Mwakilishi Kike kaunti ya Nairobi Esther Passaris kuwasilishwa mapendekezo mpya kuhusu mswada huo ambapo analenga kuzuia waandamanaji kuandamana katika maeneo yaliopigwa marufuku hasa bunge, Mahakama, ofisi kuu za umma na Ikulu pamoja na waandamanaji hao kuwa umbali wa mita 100 kutoka maeneo hayo.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Mahakama ya Malindi yawaachilia washukiwa 3 wa kesi ya Kwa Binzaro

Mahakama Kuu ya Malindi imewaachilia washukiwa watatu wanaohusishwa na kesi ya mauaji ya halaki ya watu katika kijiji cha Kwa Binzaro eneo bunge la Magarini kaunti ya Kilifi.
Hakimu wa Mahakama hiyo Joy Wesonga aliagiza kuachiliwa huru kwa Safari Kenga Nzai, Gona Charo Kalama na Kahindi Kazungu Garama wote wakiwa wakaazi wa kijiji hicho cha Kwa Binzaro.
Watatu hao walikuwa wamekamatwa baada ya kudaiwa kuuza shamba la ekari tano kwa mshukuwa mkuu wa mauaji ya watu katika kijiji cha Kwa Binzaro Sherleen Temba Anido.
Hakimu Wesonga aliwaagiza washukiwa hao kuhakikisha wanasalimisha nakala za vitambulisha vyao vya kitaifa kwa idara husika, kuripoti kwa Naibu Chifu wa eneo hilo mara mbili kwa wiki pamoja na kujisalimisha kwa maafisa wa upelelezi wa kesi hiyo mara moja kila baada ya wiki mbili.

Miili iliyofukuliwa katika kijiji cha Kwa Binzaro
Wakati huo huo upande wa mashtaka ukiongozwa na Naibu mkurugenzi wa mashtaka ya umma Jamie Yamina, uliomba kuwasilisha watu wengine wanne Mahakamani ikiwemo Jairus Otieno na mkewe Lilian Akinyi, Kahonzi Katana Karisa na Loise Zawadi waliojionda kama washukiwa na kugeuka kuwa mashahidi wa serikali.
Upande wa mashtaka pia uliaka kupewa siku 60 zaidi kuendelea kuzuiliwa kwa washukiwa wakuu Sherleen Temba Anido, James Kahindi Kazungu, Thomas Mukunwe na Kahidi Kazungu Garama katika kituo cha polisi cha Ngerenya, Kilifi, Watamu na Kijipwa ili kukamilisha uchunguzi wao kwani wanne hao wanakabiliwa na mashtaka ya itikadi kali, ugaidi, kujihusisha na uhalifu na kupanga mauaji.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Chrispus aomba msahama bunge la kaunti ya Taita Taveta

Mwakilishi wadi ya Bomani mjini Taveta kaunti ya Taita Taveta Chrispus Tondoo ameliomba bunge la kaunti hiyo msamaha kutokana na matamshi aliyoyatoa hapo awali akikashifu bunge hilo kwa madai ya kushamiri kwa visa vya ufisadi na utepetevu.
Tondoo akiomba msamaha katika bunge hilo alisema alitambua athari zilizosababishwa na matamshi hayo kwa wenyeji wa kaunti hiyo na bunge hilo, hali ambayo imemfanya kuchukua hatua hiyo ya kuomba msamaha.
Aidha Tondoo aliahidi kuliheshimu bunge hilo kwa mujibu wa kanuni na Sheria za bunge la kaunti ya Taita Taveta.
‘’Naomba msamaha kutokana na matamshi ambayo niliyatoa tarehe 2 na tarehe 3 mwezi wa Juni mwaka huu wa 2025 kwani hayakuwa yenye heshima kwa wenyeji wa Taita Taveta na bunge la kaunti’’, alisema Tondoo.
Tondoo alikuwa Mwakikishi wa wadi wa pili kuomba msamaha baada ya Mwakilishi wa wadi ya Kaloleni mjini Voi Ahmed Azari kuchukua hatua hiyo mwezi mmoja uliyopita.
Haya yalijiri baada ya kaimu spika wa bunge hilo Anselim Mwadime kuapa kuwachulia hatua za kisheria wanachama wanne wa bunge hilo, wawili wakiwa ni Tondoo na Azari ambayo tayari wameomba msamaha huku wawili wakiwa wamesalia bila kuomba msamaha.
Taarifa ya Janet Mumbi