News
Watu wawili wafariki kutokana na Mpox Mombasa

Serikali ya kaunti ya Mombasa imethibitisha vifo vya watu wawili kutokana na ugonjwa wa Mpox, huku maambukizi mapya yakiendelea kuripotiwa katika maeneo mbalimbali ya kaunti hiyo.
Msimamizi mkuu wa Idara ya afya kaunti ya Mombasa, Dkt Mohammed Hanif, alisema tangu ugonjwa wa Mpox uripotiwe humu nchini Julai 31, 2024, jumla ya visa 226 vimeripotiwa ikiwemo vifo 4, huku kaunti ya Mombasa ikiwa miongoni mwa kaunti 21 zilizoathirika.
Dkt Hanif alisema kisa cha kwanza cha Mpox kaunti ya Mombasa kiliripotiwa Septemba 3, 2024, na kufikia sasa watu 159 wamefanyiwa vipimo, ambapo 98 kati yao wamethibitishwa kuwa na maambukizi ya ugonjwa huo.
Akizungumza na Wanahabari, Dkti Hanif alisema kati ya wagonjwa hao, 24 wamelazwa katika kituo cha kutenga na kutibu wagonjwa katika kituo cha afya cha Coast General eneo la Utange huku akisema kumekuwa na ongezeko la maambukizi mapya mwezi ya Juni na Julai.
“Hii ugonjwa iko na tayari watu 159 wamefanyiwa vipimo ambapo 98 kati yao wamethibitishwa kuwa na maambukizi ya ugonjwa huo na kati ya wagonjwa hao, 24 wamelazwa katika kituo cha kutenga na kutibu wagonjwa katika kituo cha afya cha Coast General eneo la Utange”, alisema Dkt Hanif.
Kwa upande wake, Afisa wa Shirika la Stawisha Pwani, Vinceny Omoth, aliwataka wakenya hususan wale wanaoishi na virusi vya UKIMWI kuwa waangalifu na kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa wa Mpox.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Ujenzi wa barabara ya Kibaoni-Ganze-Bamba umeng’oa nanga

Baada ya wakaazi wa eneo bunge la Kilifi Kaskazini na Ganze kulalamikia ubovu wa barabara ya Kibaoni-Ganze hadi Bamba na kuangziwa na wanahabari, hali sasa ni tofauti.
Ujenzi wa barabara hiyo iliyoshudia utata na maandamano, sasa unaendelea huku mkandarasi akiwa katika hatua kupiga msasa barabara na kujenga mabomba na sehemu za kupitisha maji hasa kunaponyesha.
Justine Kandie ni muangalizi wa ujenzi wa barabara hiyo, alisema shughuli hiyo imegawanywa mara mbili, na kwa sasa wameanza ujenzi wa barabara hiyo kutoka eneo la Kibaoni mjini Kilifi kuelekea Ganze.
Kandie alisema mpango huo ulianza mwaka 2021 kutoka eneo bunge la Ganze kuelekea kibaoni japo ulisitishwa wakati huo na sasa wameanza tena kujenga umbali wa kilomita tano.
“Katika awamu ya kwanza kwa mwaka wa 2021 tulianza barabara kutoka Ganze tulikuwa tunafanya kilomita tano, kwa mda wa miaka miwili barabara ikasimama kidogo, baadaye kurudi kwa huu mwaka wa 2025 ndio tumepewa kile kiwango tuanze kutoka kibaoni kuelekea Ganze, katika hii awamu ya pili tunafanya kilomita tano ila kwa sababu barabara ni mbovu tumeamua kuanzia huku kwa Kimanje tukielekea Kibaoni ili barabara yetu iwe sawa wakati tunaposafirisha vifaa vya ujenzi”,alisema Kandie.
Baadhi ya mafundi wakiendelea na ujenzi wa barabara ya kuelekea Ganze
Picha:(Joseph Jira)
Kandie pia alisema mda wa miaka miwili aliopewa mkandarasi kukamilisha ujenzi huo wa barabara utategemea na mgao wa pesa zitatakaotolewa kufanikisha mradi huo.
“Ule mda wa kukamilisha barabara huwa inategemea uwezo wa mwanakandarasi kama ako na fedha za kutosha, itamsaidia kukamilisha kwa mda unaofaa, kwa sababu hii barabara yetu walikuwa wametupa kama miaka miwili ila saa hii mda umesonga”, aliongeza Kandie.
Wakaazi pamoja na wahudumu wa uchukuzi wa umma wanaotumia barabara hiyo wameeleza matumaini ya kuimarika kwa sekta ya uchukuzi sawa na uchumi mara tu ujenzi utakapokamilika.
Itakumbukwa kwamba barabara hiyo ilileta utata na kusababisha wakaazi kuandamana na kuifunga sawa na kutatiza shughuli za usafiri kwa mda.
“Hapo kwa usafiri na biashara huenda kukabadilika kwa sababu wengi pia wanakataa huku kwa sababu yah ii barabara vile ni mbovu hasa kazi zinakuwa ziko chini kwa sababu ya vumbi”,alisema Jeremiah Mwaringa
Tinga tinga za ujenzi wa barabara ya kuelekea Ganze.
Picha:(Joseph Jira)
Mvutano huo pia ulishuhudiwa baina ya mbunge wa Ganze Kenneth Kazungu Tungule na mbunge wa Kilifi Kaskazini Owen Baya kuhusu ujenzi wa barabara unakofaa kuanza kutekelezwa.
Hata hivyo muangalizi wa mradi huu aelieleza matumaini yake kuwa mvutano huo wa wanasiasa hautaathiri utendakazi wao huku akishinikiza wahudumu wa barabara hiyo kuwa na uvumilivu wakati wanapoendelea na ujenzi huo.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Kongamano la mabadiliko ya hali ya anga lafanyika Mombasa

Mratibu wa Kongamano la kimataifa linaloangazia masuala ya mabadiliko ya hali ya anga, INTER- GOVERNMEMTAL PANEL ON CLIMATE CHANGE, Patricia Nying’uro amesema jamii inasalia kuwa kiungo muhimu katika harakati za kuangazia mfumo wa mabadiliko ya hali ya hewa.
Kufuatia hilo, Nying’uro alitoa wito kwa wadau wa mazingira kuwekeza zaidi na kuhakikisha kila mmoja anashiriki ipasavyo katika kudhibiti mabadiliko hayo.
Nying’uro alisema Kongamano ambalo linaendelea katika kaunti ya Mombasa, linaangazia masuala ya mabadiliko ya hali ya anga na limewekeza kutambuliwa na jamii katika mikakati hiyo.
Akizungumza katika eneo la Shanzu wakati wa majadiliano hayo, Nying’uro alisema jumla ya mataifa 56 kati ya mataifa 195 yanayoshiriki kwenye mchakato wa kuweka mipango, sera na mikakati ya kudhibiti mabadiliko ya hali ya hewa yanakongamana eneo la Shanzu ili kuanisha ripoti ambayo itatoa muongozo rasmi wa kuangazia makali ya mabadiliko ya hali ya hewa.
Wakati huohuo, Nying’uro alisema pia kongamano hilo la kimataifa lina umuhimu mkubwa kwa taifa hili kwani Kenya itahusishwa moja kwa moja katika kupangilia sera za kimataifa za kudhibiti athari ya mabadiliko ya hali ya anga.
Taarifa ya Janet Shume