News
Wanafunzi wa chuo kikuu cha Pwani wanataka uwazi kuhusu kifo cha Ojwang’

Baadhi ya wanafunzi wa chuo kikuu cha pwani mjini Kilifi kaunti ya Kilifi walijitokeza na kuilaumu serikali wakidai kwamba imezembea kulinda usalama wa raia wake kutokana na visa vya mauaji ya mara kwa mara dhidi ya raia.
Wakizungumza nje ya lango la chuo hicho wakiongozwa na Vincent Obondo wanafunzi hao waliitaka serikali kuwachukulia hatua maafisa wote wanaohusishwa na kifo cha Albert Ojwang’ mwanablogu ambaye alikuwa mwanafunzi wa chuo hicho.
Obondo pia alilaumu viongozi wa kisiasa nchini ambao wameonekana kunyamazia kisa hicho cha mauaji ya Ojwang wakisisitiza kujiuzulu kwa Naibu Inspekta Jenerali wa polisi Eliud Laga’t ili kupisha uchunguzi.
“Albert hakujigongesha kwa ukuta jinsi ambavyo polisi wenyewe wanasema, sasa tunauliza serikali ni nini ambayo vijana walifanya ambacho kinakufanya uwachukie hivi, kwa viongozi wetu kwa nini mmenyamaza sana hamjajitokeza waziwazi kuuliza serikali kwa nini wanafanya, tuko hapa kuuliza na kuagiza serikali kuchukua hatua kwa Eliud Laga’t aweze kujiuzulu pamoja na msemaji wa huduma ya kitaifa ya polisi”, walisema wanafunzi hao.

Wanafunzi wa chuo kikuu cha Pwani wakilalamikia mauaji ya Albert Ojwang’
Walidai lalama zote zinaelekezwa kwa Naibu Inspekta jenerali wa polisi Eliud Laga’t hivyo anapaswa kuwajibishwa wakidai hakuna uhuru wa kujieleza nchini na serikali imekuwa ikiendekeza udikteta na kunyamazisha wakosoaji wake.
“Hata hiyo nafasi heri ibaki wazi kuliko yule jamaa awe pale, kwa sababu nchi yetu haiwezi kuwa namna hii, sisi vijana tutajitokeza namna gani kuonyesha tuko salama au hatuko salama, Nasimama hapa nikiwa na wasiwasi sana kwa sababu sijui nitakujiwa lini lakini hatuogopi na ikifika mwaka 2027 tunaambia kila mtu kuwa unakuja kwa kituo cha kupigia kura na vitu viwili, kwanza kitambulisho cha kitaifa na pili akili yako timamu”, waliongeza wanafunzi hao.
Kwa upande wao Wanaharakati wa kutetea haki za binadamu kaunti ya Kilifi wakiongozwa na Mwanase Ahmed, wameitaka serikali kuhakikisha maafisa wote wa polisi wanaohusishwa na visa vya mauaji ya raia kuwajibishwa.
“Sio mara ya kwanza kwa polisi kua wananchi hii kitu inaendelea na hakuna mtu ambaye amekamatwa na kufunguliwa mashtaka tangu mwaka jana, mimi nataka wachukuliwe hatua, tuko na jela, huu ni uhalifu dhidi ya binadamu”, aliongeza Mwanase.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Wakaazi wa Voi waonywa dhidi ya ugonjwa wa MPOX

Daktari wa magonjwa ya kuambukiza katika hospitali ya rufaa ya Moi mjini Voi katika kaunti ya Taita Taveta Urbanius Kioko amewataka wenyeji wa kaunti hiyo kuzingatia maagizo ya Wizara ya Afya ili kujikinga dhidi ya maambukizi ya ugonjwa wa Mpox.
Akiongea kwenye warsha ya Wanahabari iliyofadhiliwa na Shirika la Stawisha Pwani, Daktari Kioko alisema wananchi wanapaswa kujikinga ili kudhibiti ugonjwa huo kuenea.
Kioko pia aliwataka wale ambao wana dalili za ugonjwa huo kufika kwenye vituo vya afya ili kutibiwa.
“Huu ugonjwa huwa unaenezwa kupitia kutangamana, kuvaa nguo za mwenzako na kupitia hewa wakati wa kuongea’’, alisema Kioko.

Wadau wa sekta ya Afya katika kikao na Wanahabari mjini Voi
Vilevile, Kioko alitaja kisa cha mgonjwa mmoja wa Mpox kilichothibitishwa siku ya Jumanne wiki hii mjini Voi huku visa vingi vikishamiri katika kaunti Mombasa.
Haya yanajiri huku Wizara ya Afya nchini ikishinikiza wananchi kujiepusha kula nyama za Wanyamapori miongoni mwa tahadhari zingine kama njia mojawapo ya kukabiliana na maambukizi ya ugonjwa wa Mpox.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Mzozo kati ya Kenye na Tanzania waendelea kutokota

Serikali ya Kenya imeiandikia barua jumuiya ya afrika mashariki kupinga vikwazo vilivyowekwa na Tanzania kuhusu kufanya biashara katika taifa hilo.
Katibu mkuu katika idara ya EAC Daktari Caroline Karugu, alisema kenya imebaini kuwa agizo hilo haliambatani kamwe na masharti muhimu ya itifaki ya soko la pamoja la EAC, ambayo inahakikisha uruhu wa watu kusafiri, kuhudumu na haki ya kuanzishwa kwa biashara na raia wa mataifa ya afrika mashariki.
Aidha Kenya iliasema imeandika rasmi barua kwa EAC kuiarifu rasmi jamhuri ya muungano wa Tanzania kuangazia upya agizo hilo ili kuhakikisha inafuata kikamilifu mkataba wa EAC na sheria za Jumuia.
Maafisa wa EAC kwa sasa wanafanya uchambuzi wa hatua hiyo na itawasilisha hatua zozote zilizokiukwa pamoja na kaununi zilizopo katika mkutano ujao wa baraza la kisekta la biashara, viwanda na uekezaji.
Taarifa ya Joseph Jira