News
Walimu 294 wa shule za chekechea wamepandishwa vyeo Taita Taveta

Jumla ya walimu 294 wa shule za chekechea kaunti ya Taita Taveta wamepandishwa vyeo kulingana na kiwango chao cha masomo yao.
Akiwahutubia walimu hao gavana wa kaunti ya Taita Taveta Andrew Mwadime alisema hatua hiyo inalenga kuboresha utendakazi sawa na kuwatia motisha baada ya juhudi zao kukosa kutambuliwa kwa mda mrefu.
Hata hivyo Mwadime aliwataka walimu hao kuwajibika zaidi katika maeneo yao ya kazi, akitaja sekta ya elimu kuwa nguzo muhimu katika ujenzi wa jamii bora na iliyo na maadili.
“Mlikuwa mnafanya kazi kwa muda mrefu, mlikuwa mnafundisha, mwalipwa elfu tatu, saa ingine mwaenda bila mshahara.Hamna aliyemtambua hapo awali’’, alisema Mwadime.
Ni Kauli iliungwa mkono na naibu gavana wa kaunti hiyo Christine Kilalo ambaye aliwahimiza walimu hao kuwafunza watoto ipasavyo ili viwango vya elimu kwenye kaunti hiyo viweze kuimarika hata zaidi.
Walimu waliopandishwa cheo ni kati ya walimu 697 wanaofundisha katika shule mbalimbali za chekechea kaunti ya Taita Taveta.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Washukiwa 42 wa magenge ya uhalifu wakamatwa, Malindi

Maafisa wa polisi Malindi kaunti ya Kilifi wanasema wamewanasa washukiwa 42 wa magenge ya uhalifu katika msako kwenye mitaa ya Karima, Soweto, Milano na Mgandini.
Polisi ilisema msako huo umewawezesha kuwakamata washukiwa 11 wa genge la “Wakali Mwisho” na wanawake watano kwa visa vya utovu wa nidhamu.
Msako huo unafuatia zaira ya kamanda wa polisi ukanda wa pwani Ali Nuno katika eneo hilo na kuwataka polisi kuongeza juhudi za kukabiliana na wanachama wa magenge hayo wanaoendelea kuwahangaisha wananchi.
Simu 14 zilizoshukiwa kuwa za wizi zilinaswa kutoka kwa mshukiwa Ahmed Ali.
Magenge ya uhalifu wakiwemo wale wanaojiita mawoza ni miongoni mwa makundi ya vijana ambao wamekuwa wakitatiza amani na usalama miongoni mwa wakaazi eneo hilo.
Idara ya usalama ilikuwa mbioni kuwasaka wahalifu katika mji huo wa kitalii katika juhudi za kurejesha amani na utulivu.
Vijana hao wamekuwa wakiwavamia wakaazi na kutekeleza vitendo vya wizi.
Taarifa ya Joseph Jira.
News
Mabadiliko ya tabianchi yatajwa kuchangia mapato duni ya samaki, Lamu

Wadau katika sekta ya mazingira kaunti ya Lamu wanasema mabadiliko ya hali ya anga yanayoshuhudiwa sawa na ujenzi wa bandari ya Lamu kumechangia mapato ya samaki kupungua katika bahari hindi.
Mahmoud Yusuf ambaye ni mwanazingira alisema zana za kizamani wanazotumia wavuvi kuvua samaki pia zinachangia mapato duni ya samaki.
Yusuf alisema tangu ujenzi huo wa bandari uanze, maji ya bahari chini yamekuwa na matope kutokana na kuchimbwa na kufukuliwa kwa bahari, hali iliyochangia samaki kutorokea bahari kuu.
Mwanamazingira huyo aliitaka serikali kuwapa wavuvi vifaa vya kisasa vya uvuvi sawa na meli za uvuvi zitakazowawezesha kufika maji makuu, baada ya bandari ya ndani kuharibika.
Taarifa ya Joseph Jira.