News
Wakulima Kilifi wanufaika na Ng’ombe wa maziwa.

Serikali ya kaunti ya Kilifi kupitia idara ya kilimo imeanzisha mpango wa kusambaza wa Ng’ombe wa maziwa kwa makundi ya wakulima wa mifugo kaunti hiyo.
Akizungumza na wanahabari wakati wa zoezi la ugavi wa ng’ombe hao eneo la Kakuyuni, waziri wa kilimo kaunti ya Kilifi Chula Mwagona alibainisha kuwa tayari jumla ya Ng’ombe 150 wamesambazwa katika maeneo mbalimbali ya kaunti hiyo kwa wafugaji.
Mwagona alikariri kuwa mradi huo unalenga kusambaza takriban ng’ombe 500 kwa makundi ya wafugaji ifikapo mwishoni mwa mpango huo.
“Kaunti ya kilifi idadi ya ng’ombe ambao tumesambaza inafika zaidi ya 150, kila kundi linapata ng’ombe 30 na saa hii tuko na makundi 17”, alisema Mwagona.
Wakati huo huo waziri huyo alidokeza kuwa mradi huo utapunguza pakubwa tatizo la uhaba wa maziwa ambao umekuwa ukikumba kaunti ya Kilifi mara kwa mara.
“Wakati kama huu uhaba wa maziwa umepunguwa kwa sababu maziwa yako kwa wingi, na kwa sababu sisi tumeanza kuwapatia wakulima ng’ombe tunatarajia kwamba ng’ombe wakianza kuzaa na kukamuliwa lile tatizo la maziwa ambalo tulikuwa tunapata litakuwa haliko”, aliongeza waziri huyo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Wakaazi wa Voi waonywa dhidi ya ugonjwa wa MPOX

Daktari wa magonjwa ya kuambukiza katika hospitali ya rufaa ya Moi mjini Voi katika kaunti ya Taita Taveta Urbanius Kioko amewataka wenyeji wa kaunti hiyo kuzingatia maagizo ya Wizara ya Afya ili kujikinga dhidi ya maambukizi ya ugonjwa wa Mpox.
Akiongea kwenye warsha ya Wanahabari iliyofadhiliwa na Shirika la Stawisha Pwani, Daktari Kioko alisema wananchi wanapaswa kujikinga ili kudhibiti ugonjwa huo kuenea.
Kioko pia aliwataka wale ambao wana dalili za ugonjwa huo kufika kwenye vituo vya afya ili kutibiwa.
“Huu ugonjwa huwa unaenezwa kupitia kutangamana, kuvaa nguo za mwenzako na kupitia hewa wakati wa kuongea’’, alisema Kioko.

Wadau wa sekta ya Afya katika kikao na Wanahabari mjini Voi
Vilevile, Kioko alitaja kisa cha mgonjwa mmoja wa Mpox kilichothibitishwa siku ya Jumanne wiki hii mjini Voi huku visa vingi vikishamiri katika kaunti Mombasa.
Haya yanajiri huku Wizara ya Afya nchini ikishinikiza wananchi kujiepusha kula nyama za Wanyamapori miongoni mwa tahadhari zingine kama njia mojawapo ya kukabiliana na maambukizi ya ugonjwa wa Mpox.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Mzozo kati ya Kenye na Tanzania waendelea kutokota

Serikali ya Kenya imeiandikia barua jumuiya ya afrika mashariki kupinga vikwazo vilivyowekwa na Tanzania kuhusu kufanya biashara katika taifa hilo.
Katibu mkuu katika idara ya EAC Daktari Caroline Karugu, alisema kenya imebaini kuwa agizo hilo haliambatani kamwe na masharti muhimu ya itifaki ya soko la pamoja la EAC, ambayo inahakikisha uruhu wa watu kusafiri, kuhudumu na haki ya kuanzishwa kwa biashara na raia wa mataifa ya afrika mashariki.
Aidha Kenya iliasema imeandika rasmi barua kwa EAC kuiarifu rasmi jamhuri ya muungano wa Tanzania kuangazia upya agizo hilo ili kuhakikisha inafuata kikamilifu mkataba wa EAC na sheria za Jumuia.
Maafisa wa EAC kwa sasa wanafanya uchambuzi wa hatua hiyo na itawasilisha hatua zozote zilizokiukwa pamoja na kaununi zilizopo katika mkutano ujao wa baraza la kisekta la biashara, viwanda na uekezaji.
Taarifa ya Joseph Jira