News
Wadau wa amani wabuni mbinu za kudhibiti utovu wa usalama

Wadau wa amani katika kaunti ya Kilifi wameishinikiza jamii kuzingatia amani na uwiano.
Wakiongozwa na Harold Mwatua ambaye ni Mwenyekiti wa kamati ya amani katika kaunti ya Kilifi, wadau hao walisisitiza haja ya uhusiano mwema baina ya maafisa wa usalama na jamii.
Mwatua alisema hali hiyo itasaidia sana katika kuimarisha usalama katika kaunti ya Kilifi kwa jumla.
“Nyinyi kama jamii mnawafahamu wale wote wanaotekeleza uhalifu, ushirikiano wenu na maafisa wa polisi utawezesha wahalifu kukamatwa na kushtakiwa” alisema Mwatua katika hafla ya kujenga uhusiano mwema baina ya maafisa wa usalama na raia kwenye uwanja wa Karisa Maitha mjini Kilifi.
“Polisi ni binadamu kama wewe, ni mtu kama wewe, ni jirani na ndugu yako tuishi nao kwa amani na uwiano” aliongeza Mwatua.
Akiunga mkono kauli hiyo Mwenyekiti wa baraza la Wahubiri na Maimam ukanda wa Pwani CICC, Askofu Amos Lewa aliataka wakaazi kutojenga uadui na maafisa wa polisi iwapo wanapania kuona utovu wa usalama ukidhibitiwa.
Askofu Lewa pia aliwashinikiza wananchi kuzingatia amani hata katika kupigania haki huku akikashifu vikali maandamano ya vurugu na ghasia yaliyoshuhudiwa siku ya sabasaba jijini Nairobi.
Hafla hiyo iliwaleta pamoja maafisa wa usalama, maafisa tawala, mashirika ya kijamii na wananchi ili kutangaza Amani sawa na kujenga uhusiano mwema kati ya polisi na wananchi.
Taarifa ya Hamis Kombe
News
Godhana, awataka wakaazi kutoingiza siasa miradi ya maendeleo

Gavana wa kaunti ya Tana River Dhadho Godhana amewataka wenyeji wa kaunti hiyo kujiepusha na wanasiasa ambao wanaingiza siasa kwenye masuala ya maendeleo.
Godhana alisema hilo limechangia kaunti ya Tana River kusalia nyuma kimaendeleo hali ambayo itasababisha miradi mingi kuzidi kukwama.
Godhana alisema ni lazima viongozi na wenyeji wa kaunti ya Tana River washirikiane na uongozi wa kaunti ili kuafikia utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Wakati huo huo Godhana aliesema mradi wa Village Cluster ambao umekuwa ukipingwa ndio utakaosaidia kudhibiti changamoto ambazo zinaikumba kaunti ya Tana River.
Naye Mahat Ali Loka ambaye ni Naibu Gavana wa kaunti ya Tana River, aliwaonya wanasiasa kutoka kaunti zingine dhidi ya kuingilia siasa za kaunti hiyo huku Spika wa bunge la kaunti hiyo Osman Noor Galole, akitoa onyo kwa wafanyikazi wa umma dhidi ya kujumu la serikali ya kaunti ya Tana River.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Mwili wapatikana baharini Shelly Beach Likoni

Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza kisa ambapo mwili wa mwanamme ambaye hajafahamika umepatikana ukielea katika maji ya bahari hindi kwenye ufuo wa Shelly Beach eneo bunge la Likoni.
Ripoti ya polisi ilibaini kuwa mwili huo uligunduliwa na wavuvi eneo hilo, ambao walipiga ripoti katika kituo cha polisi cha Shelly Beach kuhusiana na tukio hilo.
Polisi walisema hawakubaini mara moja anakotoka mtu huyo.
Vile vile haikubainika iwapo marehemu alizama au aliuawa kabla ya mwili wake kutupwa baharini.
Polisi walisema hawajakutana na stakabadhi zozote za kumtambulisha mtu huyo huku wakiwasihi wananchi kutoa taarifa iwapo wanafahamu familia ya marehemu.
Mwili unahifadhiwa katika hifadhi ya maiti katika hospitali ya Rufaa ya Coast General Mombasa wakati uchunguzi zaidi ukiendelea.
Taarifa ya Joseph Jira