News
Viongozi wa kisiasa wampigia debe Joho kuwa Kiongozi wa Pwani

Baadhi ya viongozi wa kisiasa kaunti ya Mombasa wanaendelea kumpigia debe Waziri wa madini na uchumi wa bahari na maziwa nchini, Ali Hassan Joho kuwa Kiongozi wa Pwani, ambaye atapeperusha bendera ya urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka wa 2032.
Viongozi hao wakiongozwa na Mwakilishi wa kike kaunti ya Mombasa Zamzam Mohamed wamesema Waziri Joho ana uwezo mkubwa wa kuliunganisha eneo la Pwani ili liweze kunufaika kimaendeleo kama maeneo mengine nchini.
“Leo rais ametutunuku, ametupatia Hassan Ali Joho kama Waziri wa Blue Economy ambayo inahusu kaunti zetu, na Waziri Hassan Joho anachapa kazi, kwa hivyo safari yetu sisi tumeianza’’, alisema Zamzam.
Zamzam alisema Joho amekuwa kwenye siasa kwa miaka mingi na ana uzoefu katika uongozi, hivyo basi anapaswa kupeperusha bendera hiyo.
Ni kauli ambayo imeunga mkono na Mbunge wa Jomvu Badi Twalib ambaye amesisitiza ushirikiano baina ya viongozi ili kuhakikisha malengo hayo yanaafikiwa ipasavyo.
Naye Mbunge wa Kisauni Rashid Bedzimba alisema maeneo mengine ya nchi yanajiandaa kuwa na kiongozi ambaye ataliongoza taifa hili na kusisitiza umuhimu wa Wapwani kushirikiana ili Joho aweze kuwa rais wa taifa hili mwaka wa 2032.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Chengo, awahimiza viongozi wa Pwani kutumia nafasi zao vizuri

Mwakilishi wa wadi ya Tezo kaunti ya Kilifi, Thomas Chengo alitoa wito kwa viongozi wa Pwani kutumia nafasi walizo nazo katika uongozi wa Kenya Kwanza ili kuboresha kaunti za Pwani kimaendeleo.
Chengo ambaye pia ni Kiongozi wa walio wachache katika bunge la kaunti ya Kilifi, alisema kuna viongozi wengi wa Pwani ambao wako serikalini na ikiwa watatumia fursa hiyo ipasavyo huenda wapwani wakanufaika zaidi kupitia miradi mbalimbali.
Kulingana na Chengo, hii ndio mara ya kwanza kwa wapwani kuwa na viongozi wengi serikalini na akasisitiza umuhimu wa ushirikiano ili kuliboresha eneo la Pwani kama maeneo mengine nchini.
“Nataka ijulikane kwamba hii sio ajali na ikiwa hatutashikana vizuri, tukatumia hii nafasi vizuri nafasi hii kujirudia tena sio rahisi’’, alisema Chengo.
Vilevile aliwashinikiza viongozi wa kaunti ya Kilifi kuwahudumia wenyeji na kutekeleza miradi ya maendeleo badala ya kunyoshea kidole cha lawama kwa masuala ambayo hayana manufaa.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Waislam Waadhimisha Sikukuu ya Eid-Ul-Adha

Waislam kote duniani wanaadhimisha Sikukuu ya Eid-Ul-Adha, inayojulikana pia kama sikukuu ya sadaka, ambayo huadhimishwa katika mwezi wa Dhul Hijjah katika kalenda ya Kiislam.
Sikukuu hii ni moja ya nyakati tukufu zaidi katika Uislamu, ikiashiria kilele cha Hijja na kuadhimisha utiifu wa Nabii Ibrahimu aliyekuwa tayari kumtoa mwanawe Ismail kama sadaka kwa amri ya Mwenyezi Mungu.
Siku kumi za mwanzo za Dhul Hijjah zinahesabiwa kuwa siku takatifu zaidi, zikiwa zimejawa na ibada, kufunga, na dua.
Mwaka huu, zaidi ya mahujaji milioni 2 wanahudhuria Hijja katika mji mtakatifu wa Makkah nchini Saudi Arabia, Kenya ikipeleka wahujaji 4,500, kuhijji, ikiwa ni mojawapo ya idadi kubwa zaidi katika historia ya hivi karibuni.
Viongozi mbalimbali wa dini ya kiislam waliwahimiza waumini wa dini ya kiislam kuhakikisha wanasheherekea sikukuu ya Eid-ul-Adha pamoja na wale wasiojiweza kwa kuchinja mifugo na kugawa na watu wengine wasiobahati katika jamii.
Taarifa ya Lolani Kalu