News
Viongozi wa kisiasa wampigia debe Joho kuwa Kiongozi wa Pwani

Baadhi ya viongozi wa kisiasa kaunti ya Mombasa wanaendelea kumpigia debe Waziri wa madini na uchumi wa bahari na maziwa nchini, Ali Hassan Joho kuwa Kiongozi wa Pwani, ambaye atapeperusha bendera ya urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka wa 2032.
Viongozi hao wakiongozwa na Mwakilishi wa kike kaunti ya Mombasa Zamzam Mohamed wamesema Waziri Joho ana uwezo mkubwa wa kuliunganisha eneo la Pwani ili liweze kunufaika kimaendeleo kama maeneo mengine nchini.
“Leo rais ametutunuku, ametupatia Hassan Ali Joho kama Waziri wa Blue Economy ambayo inahusu kaunti zetu, na Waziri Hassan Joho anachapa kazi, kwa hivyo safari yetu sisi tumeianza’’, alisema Zamzam.
Zamzam alisema Joho amekuwa kwenye siasa kwa miaka mingi na ana uzoefu katika uongozi, hivyo basi anapaswa kupeperusha bendera hiyo.
Ni kauli ambayo imeunga mkono na Mbunge wa Jomvu Badi Twalib ambaye amesisitiza ushirikiano baina ya viongozi ili kuhakikisha malengo hayo yanaafikiwa ipasavyo.
Naye Mbunge wa Kisauni Rashid Bedzimba alisema maeneo mengine ya nchi yanajiandaa kuwa na kiongozi ambaye ataliongoza taifa hili na kusisitiza umuhimu wa Wapwani kushirikiana ili Joho aweze kuwa rais wa taifa hili mwaka wa 2032.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Godhana, awataka wakaazi kutoingiza siasa miradi ya maendeleo

Gavana wa kaunti ya Tana River Dhadho Godhana amewataka wenyeji wa kaunti hiyo kujiepusha na wanasiasa ambao wanaingiza siasa kwenye masuala ya maendeleo.
Godhana alisema hilo limechangia kaunti ya Tana River kusalia nyuma kimaendeleo hali ambayo itasababisha miradi mingi kuzidi kukwama.
Godhana alisema ni lazima viongozi na wenyeji wa kaunti ya Tana River washirikiane na uongozi wa kaunti ili kuafikia utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Wakati huo huo Godhana aliesema mradi wa Village Cluster ambao umekuwa ukipingwa ndio utakaosaidia kudhibiti changamoto ambazo zinaikumba kaunti ya Tana River.
Naye Mahat Ali Loka ambaye ni Naibu Gavana wa kaunti ya Tana River, aliwaonya wanasiasa kutoka kaunti zingine dhidi ya kuingilia siasa za kaunti hiyo huku Spika wa bunge la kaunti hiyo Osman Noor Galole, akitoa onyo kwa wafanyikazi wa umma dhidi ya kujumu la serikali ya kaunti ya Tana River.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Mwili wapatikana baharini Shelly Beach Likoni

Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza kisa ambapo mwili wa mwanamme ambaye hajafahamika umepatikana ukielea katika maji ya bahari hindi kwenye ufuo wa Shelly Beach eneo bunge la Likoni.
Ripoti ya polisi ilibaini kuwa mwili huo uligunduliwa na wavuvi eneo hilo, ambao walipiga ripoti katika kituo cha polisi cha Shelly Beach kuhusiana na tukio hilo.
Polisi walisema hawakubaini mara moja anakotoka mtu huyo.
Vile vile haikubainika iwapo marehemu alizama au aliuawa kabla ya mwili wake kutupwa baharini.
Polisi walisema hawajakutana na stakabadhi zozote za kumtambulisha mtu huyo huku wakiwasihi wananchi kutoa taarifa iwapo wanafahamu familia ya marehemu.
Mwili unahifadhiwa katika hifadhi ya maiti katika hospitali ya Rufaa ya Coast General Mombasa wakati uchunguzi zaidi ukiendelea.
Taarifa ya Joseph Jira