News
Viongozi wa kisiasa wampigia debe Joho kuwa Kiongozi wa Pwani

Baadhi ya viongozi wa kisiasa kaunti ya Mombasa wanaendelea kumpigia debe Waziri wa madini na uchumi wa bahari na maziwa nchini, Ali Hassan Joho kuwa Kiongozi wa Pwani, ambaye atapeperusha bendera ya urais katika uchaguzi mkuu wa mwaka wa 2032.
Viongozi hao wakiongozwa na Mwakilishi wa kike kaunti ya Mombasa Zamzam Mohamed wamesema Waziri Joho ana uwezo mkubwa wa kuliunganisha eneo la Pwani ili liweze kunufaika kimaendeleo kama maeneo mengine nchini.
“Leo rais ametutunuku, ametupatia Hassan Ali Joho kama Waziri wa Blue Economy ambayo inahusu kaunti zetu, na Waziri Hassan Joho anachapa kazi, kwa hivyo safari yetu sisi tumeianza’’, alisema Zamzam.
Zamzam alisema Joho amekuwa kwenye siasa kwa miaka mingi na ana uzoefu katika uongozi, hivyo basi anapaswa kupeperusha bendera hiyo.
Ni kauli ambayo imeunga mkono na Mbunge wa Jomvu Badi Twalib ambaye amesisitiza ushirikiano baina ya viongozi ili kuhakikisha malengo hayo yanaafikiwa ipasavyo.
Naye Mbunge wa Kisauni Rashid Bedzimba alisema maeneo mengine ya nchi yanajiandaa kuwa na kiongozi ambaye ataliongoza taifa hili na kusisitiza umuhimu wa Wapwani kushirikiana ili Joho aweze kuwa rais wa taifa hili mwaka wa 2032.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Wahudumu wa afya Lamu watishia kuishtaki serikali ya kaunti hiyo

Wahudumu wa Afya kaunti ya Lamu wametishia kuelekea Mahakamani kuishtaki serikali ya kaunti hiyo kwa kukaidi kutekeleza matakwa yao.
Wahudumu hao waliishtumu serikali ya kaunti ya Lamu kwa kupuuza matakwa yao na badala yake kutumia vitisho ili kuwashurutisha kurejea kazini.
Kulingana na viongozi wa wahudumu hao, licha ya mgomo wao kuendelea kwa zaidi ya wiki mbili serikali ya kaunti hiyo imekataa kata kuandaa vikao vya kusuluhisha malalamishi yao.
Baadhi ya changamoto wanazolalamikia ni pamoja na kufanya kazi kwa zaidi ya miaka 10 bila ya kupandishwa vyeo, kupuuzwa kwa mkataba wa makubaliano ya nyongeza ya mishahara, kunyimwa kwa mishahara kwa baadhi ya wahudumu hao miongoni mwa matakwa mengine.
“Mkiendelea kutufinyilia itabidi tufuate njia ya sheria kwa sababu tunajua tunalilia haki yetu, haiwezekani serikali ya kaunti inashindwa kutupandisha vyeo ilhali tumefanya kazi kwa miaka 15 sasa, hatuwezi kuendelea kufanya kazi katika mazingira duni na pia mkataba wa makubaliano kuhusu nyongeza ya mishahara sharti itekelezwe” walisisitiza viongozi hao.
Wakati uo huo serikali ya kaunti ya Lamu imejibu malimishi yao kupitia barua na kutangaza kuwa mgomu huo ni kinyume cha seria na kuwataka wahudumu hao kurejea kazini mara moja.
Taarifa ya Elizabeth Mwende
News
Rais Ruto atuma KDF kusimamia ujenzi wa hospitali nchini

Rais William Ruto ametuma jeshi la KDF kusimamia ujenzi wa vituo vya afya zaidi ya 75 kote nchini katika juhudi za kuhakikisha ujenzi unakamilika kwa haraka.
Akizungumza katika kaunti ya Narok wakati wa uzinduzi wa hospitali ya Sogoo Level 4, waziri wa ulinzi Patrick Mariru alifichua kuwa ujenzi wa hospitali hiyo yenye mamlaka kamili itakamilika baada ya mda wa miezi 11.
Ujenzi wa hospitali ya Sogoo Level 4 ulivutia rais Ruto alipozuru eneo hilo mwezi mei mwaka 2025, jambo lililomfanya kuagiza KDF kuipandisha hadhi.
Mariru hata hivyo alishikilia kuwa wafanyikazi wote wasio na ujuzi watatolewa kutoka kwa jamii.
“Jeshi litamsimamia mkandarasi. Hilo liwe wazi, kazi yote itafanywa na vijana wa Sogoo. Tutaweka maafisa wawili na kila jioni watanipa ripoti ya maendeleo,” alisema Mariru.
“Tuna zaidi ya miradi 75 tunayosimamia na sio kwamba tunabadilisha wakala wa serikali tunataka tu kushirikiana na ofisi tofauti miongoni mwao wizara za afya na michezo.”
Taarifa ya Joseph Jira