News
Vijana wahimizwa kuepuka mihadarati

Vijana wamehimizwa kujitenga na matumizi ya dawa za kulevya kutokana na athari zake ambazo zimechangia maisha ya vijana wengi kusambaratika.
Hii ni baada ya Mamlaka ya kukabiliana na mihadarati na vileo haramu nchini Nacada kubaini ongezeko la idadi ya vijana katika uraibu huo.
Akizungumza katika shule ya upili ya wavulana ya Malindi high katika kaunti ya Kilifi, mkurugenzi wa Wakfu wa Smachs-Charlene Ruto alisema vijana wana jukumu kubwa la kuchukua mwongozo wa maisha yao na wala sio kulaumu viongozi.
“Fukuza dawa za kulevya, karibisha mabadiliko, huu ndio ujumbe pekee tuliokuja kuwapa leo, vijana, asilimia 70 ya uongozi unaanza na wewe mwenyewe, tunapenda kuelekeza lawama kwa serikali ni mwalimu au mzazi, lakini kama vijana tuchukue jukumu na mabadiliko yanaanza na sisi wenyewe”,alisema Charlene Ruto.
Kwa upande wake Rais wa Muungano wa wanafunzi kaunti Kilifi Kahindi James Kalama alisema kaunti ya Kilifi ina vijana wengi ambao ni waraibu wa dawa za kulevya jambo ambalo linafaa kuangaziwa kwa kina, kauli ambayo iliungwa mkono na rais wa Jumuiya ya wanafunzi wa Pwani David Msongori.
“Kilifi inaidadi kubwa ya vijana ambao wameathirika na matumizi ya dawa za kulevya, tukifuata takwimu za Nacada na ndio maana tumekuja na kongamano kama hili ambao tuko nalo siku ya leo kuhamasisha athari ya mihadarati ili waweze kuachana nayo na kufuata elimu”, alisema Kalama.
Kwa upande wake naibu gavana wa kaunti ya Kilifi Flora Mbetsa Chibule aliwahimiza wanafunzi kuzingatia masomo yao ili kubadili msimamo wa maisha yao badala ya kujiingiza katika mambo yasiofaa.
“Mbali na kwamba tunafukuza dawa za kulevya eneo letu, nyinyi wanakilifi leo na vijana wote nchini tunasema tunawatambua na serikali inaimani na nyinyi.”, alisema Chibule.
Baadhi ya viongozi wa mashirika walioandamana na mwanawe rais William Ruto walisema matumizi ya dawa za kulevya yamesambaratisha maisha ya vijana wengi ambao wamekosa mwelekeo maishani, wakiwarai viongozi wa kaunti kuweka mikakati ya kunusuru maisha ya vijana hao.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Mahakama ya Kilifi imetoa hukumu kwa wanaume 6 wanaokabiliwa na mashtaka ya unajisi

Mahakama ya Kilifi imetoa hukumu kwa wanaume 6 wanaokabiliwa na mashtaka ya unajisi.
Hakimu wa Mahakama hiyo Ivy Wasike alimhukumu Lucky Munga na Hassan Daniel kifungo cha miaka 30 gerezani baada ya Mahakama kubaini kwamba walihusika kwa kuwatendea unyama watoto wa umri wa miaka 13 na 15.
Safari Karisa Lewa alihukumiwa kifungo cha miaka 15 gerezani kwa kumnajisi mtoto wake mwenyewe wa umri wa miaka 14 huku Eric Ruwa na Lucky Katana Kenga wakihukumiwa kifungo cha miaka 6 gerezani kwa kosa sawa na hilo.
Hata hivyo Mahakama hiyo ilimhukumu kifungo cha miaka 3 Kithi Kombe kutokana na kesi hiyo kwa mtoto wa miaka 15, japo baadaye Mahakama ikabaini kwamba mshukiwa sio baba halali wa mtoto aliyezaliwa baada ya Kithi kumnajisi mtoto huyo.
Akizungumza wakati wa vikao vya Mahakama baada ya kutoa hukumu hizo, Hakimu Wasike alisema Mahakama umezingatia ushahidi uliyotolewa Mahakamani huku akiwarai wananchi kujitenga na visawishi vibaya ili kuepuka mkono wa sheria.
Hakimu Wasike alihoji kwamba washtakiwa wa haki ya kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa Mahakama lakini kwa kuzingatia taratibu zote za Mahakama na sheria.
Taarifa ya Teclar Yeri
News
Thoya: Serikali kuu iongeze mgao wa fedha kwa sekta ya Afya

Naibu gavana wa kaunti ya Mombasa Francis Thoya ametoa changamoto kwa serikali kuu kuongeza mgao wa fedha ili kufanikisha utaoji wa huduma za afya.
Akizungumza katika kaunti hiyo, Thoya alisema kuwa huduma nyingi za afya katika kaunti hiyo ya Mombasa zinakabiliwa na changamoto ya raslimali ndogo hali ambayo inakwamisha juhudi za kuwahudumia wananchi ipasavyo.
Thoya pia alitaka serikali kuhakikisha inaharakisha kuajiri wahudumu zaidi wa afya ili wenyeji wa Mombasa waweze kupata huduma bora za matibabu bila changamoto zozote.
Aidha, Thoya alisema kwamba hali ya uhaba wa wahudumu wa afya ni changamoto kuu ambayo inazuia utoaji wa huduma bora za matibabu hali inayowafanya wale wachache waliopo kufanya kazi katika mazingira magumu.
Taarifa ya Janet Mumbi
-
News23 hours ago
Mahakama ya Kilifi imetoa hukumu kwa wanaume 6 wanaokabiliwa na mashtaka ya unajisi
-
Sports5 hours ago
Ndoto ya Harambee Stars ya kufuzu Kombe la Dunia 2026 Yagonga mwamba baada ya kupigwa 3-1 na Gambia Kasarani
-
Sports22 hours ago
Kocha wa Uingereza Thomas Tuchel akataa madai ya “laana” huku akilenga kuvunja ukame wa miaka 60 wa mataji makubwa