News
Vijana eneo la Junju, Kilifi wavuna wasipopanda

Maafisa wa Idara ya utawala wa mkoa katika wadi ya Junju kaunti ya Kilifi imeonya wakaazi wa kijiji cha Mwembetsungu dhidi ya kuendekeza visa vya wizi.
Hii ni baada ya mwanamke mmoja kunusurika kifo mikononi mwa wakaazi waliokuwa na gadhabu baada ya kumfumania akiiba mahindi kwenye shamba moja kijijini humo.
Mzee wa Mtaa kwenye kijiji hicho Elijah Mbigo alisema visa vya wizi wa mahindi kijijini humo vimekithiri mno msimu huu, huku akitaja kufikia sasa zaidi ya mashamba matano yamevamiwa na mahindi kuibiwa.
Akiongea na coco fm, Mbigo aliweka wazi kwamba tayari mikakati ya kukabiliana na wizi huo imewekwa huku akiwataka wakaazi wa kijiji hicho kushirikiana ili kuhakikisha wanaotekeleza wizi huo wanapatikana na kuchukuliwa hatua kali za kisheria.
“Onyo ninatoa kila siku lakini bado halijazingati kwa sababu vijana hapa niwavivu hawataki vibarua, hata wakiitwa kazi mahali hawaendi, sasa hiyo inafanya mtaa umeharibika kwa sababu ya uvivu wa vijana”, alisema Mbigo.
Kauli yake iliungwa mkono na mzee wa nyumba kumi kwenye kijiji hicho Benson Mganga ambaye alisisitiza haja ya ushirikiano miongoni mwa wakaazi huku akitaka sheria kali kuchukuliwa endapo wanaotekeleza wizi huo watapatikana.
Taarifa ya Mwanahabari wetu.
News
Mahakama ya Malindi yawaachilia washukiwa 3 wa kesi ya Kwa Binzaro

Mahakama Kuu ya Malindi imewaachilia washukiwa watatu wanaohusishwa na kesi ya mauaji ya halaki ya watu katika kijiji cha Kwa Binzaro eneo bunge la Magarini kaunti ya Kilifi.
Hakimu wa Mahakama hiyo Joy Wesonga aliagiza kuachiliwa huru kwa Safari Kenga Nzai, Gona Charo Kalama na Kahindi Kazungu Garama wote wakiwa wakaazi wa kijiji hicho cha Kwa Binzaro.
Watatu hao walikuwa wamekamatwa baada ya kudaiwa kuuza shamba la ekari tano kwa mshukuwa mkuu wa mauaji ya watu katika kijiji cha Kwa Binzaro Sherleen Temba Anido.
Hakimu Wesonga aliwaagiza washukiwa hao kuhakikisha wanasalimisha nakala za vitambulisha vyao vya kitaifa kwa idara husika, kuripoti kwa Naibu Chifu wa eneo hilo mara mbili kwa wiki pamoja na kujisalimisha kwa maafisa wa upelelezi wa kesi hiyo mara moja kila baada ya wiki mbili.

Miili iliyofukuliwa katika kijiji cha Kwa Binzaro
Wakati huo huo upande wa mashtaka ukiongozwa na Naibu mkurugenzi wa mashtaka ya umma Jamie Yamina, uliomba kuwasilisha watu wengine wanne Mahakamani ikiwemo Jairus Otieno na mkewe Lilian Akinyi, Kahonzi Katana Karisa na Loise Zawadi waliojionda kama washukiwa na kugeuka kuwa mashahidi wa serikali.
Upande wa mashtaka pia uliaka kupewa siku 60 zaidi kuendelea kuzuiliwa kwa washukiwa wakuu Sherleen Temba Anido, James Kahindi Kazungu, Thomas Mukunwe na Kahidi Kazungu Garama katika kituo cha polisi cha Ngerenya, Kilifi, Watamu na Kijipwa ili kukamilisha uchunguzi wao kwani wanne hao wanakabiliwa na mashtaka ya itikadi kali, ugaidi, kujihusisha na uhalifu na kupanga mauaji.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Chrispus aomba msahama bunge la kaunti ya Taita Taveta

Mwakilishi wadi ya Bomani mjini Taveta kaunti ya Taita Taveta Chrispus Tondoo ameliomba bunge la kaunti hiyo msamaha kutokana na matamshi aliyoyatoa hapo awali akikashifu bunge hilo kwa madai ya kushamiri kwa visa vya ufisadi na utepetevu.
Tondoo akiomba msamaha katika bunge hilo alisema alitambua athari zilizosababishwa na matamshi hayo kwa wenyeji wa kaunti hiyo na bunge hilo, hali ambayo imemfanya kuchukua hatua hiyo ya kuomba msamaha.
Aidha Tondoo aliahidi kuliheshimu bunge hilo kwa mujibu wa kanuni na Sheria za bunge la kaunti ya Taita Taveta.
‘’Naomba msamaha kutokana na matamshi ambayo niliyatoa tarehe 2 na tarehe 3 mwezi wa Juni mwaka huu wa 2025 kwani hayakuwa yenye heshima kwa wenyeji wa Taita Taveta na bunge la kaunti’’, alisema Tondoo.
Tondoo alikuwa Mwakikishi wa wadi wa pili kuomba msamaha baada ya Mwakilishi wa wadi ya Kaloleni mjini Voi Ahmed Azari kuchukua hatua hiyo mwezi mmoja uliyopita.
Haya yalijiri baada ya kaimu spika wa bunge hilo Anselim Mwadime kuapa kuwachulia hatua za kisheria wanachama wanne wa bunge hilo, wawili wakiwa ni Tondoo na Azari ambayo tayari wameomba msamaha huku wawili wakiwa wamesalia bila kuomba msamaha.
Taarifa ya Janet Mumbi