News
UN yakosoa mauaji ya Saba saba

Ofisi ya kamishna mkuu wa haki za kibinadamu wa umoja wa mataifa (OHCHR) imeibua wasiwasi kuhusu maandamano ya siku ya Saba Saba nchini Kenya, ambapo makumi ya raia waliuawa na wengine kujeruhiwa.
Katika taarifa yake siku ya Jumanne, kamishna mkuu wa umoja wa mataifa wa haki za kibinadamu Volker Türk alilaani ukiukwaji wa haki za binadamu nchini Kenya, na kuahidi kushirikiana na Kenya katika kutatua changamoto vile vile katika uchunguzi.
“Tumesikitishwa sana na mauaji ya jana ya takriban watu 10, pamoja na uporaji na uharibifu wa mali nchini Kenya wakati polisi na vikosi vingine vya usalama vilijibu maandamano ya ghasia katika mji mkuu wa Nairobi na kaunti zingine 16. Risasi za sumu, risasi za mpira, gesi ya kutoa machozi na maji ya kuwasha zilitumika,” ilisema OHCHR kupitia msemaji wake Ravina Shamdasani.
Türk alitoa wito wa utulivu pamona na heshima kamili kwa uhuru wa kujieleza, kujumuika na kukusanyika kwa amani.
“Ni muhimu kwamba malalamiko halali katika mzizi wa maandamano haya yashughulikiwe,” alisema.
Kamishna Mkuu pia alihimiza kwamba mauaji na ukiukwaji wa haki za binadamu “kuchunguzwa kwa haraka, kikamilifu, kwa uhuru na kwa uwazi.”
Wakati wa maandamano ya Julai 7, 2025, polisi waliripoti kwamba raia 11 waliuawa na 567 walikamatwa.
Pia, huduma ya kitaifa ya polisi (NPS) ilisema maafisa 52 na raia 11 walijeruhiwa, magari 12 ya polisi, magari 3 ya serikali na magari 4 ya raia yaliharibiwa.
“Chini ya sheria ya kimataifa ya haki za binadamu, nguvu ya kimakusudi ya maafisa wa kutekeleza sheria, ikiwa ni pamoja na silaha, inapaswa kutumika tu inapobidi ili kulinda maisha kutokana na tishio linalokaribia,” aliongeza Türk.
Maandamano yaliyoshuhudiwa siku ya Saba Saba yalikuja baada ya wiki mbili tu baada ya raia 15 kuuawa mnamo Juni 25, 2025.
Kisha, wakenya waliandamana katika ukumbusho wa mauaji ya zaidi ya watu 60 wakati wa maandamano ya kupinga ushuru mnamo Juni 2024.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Mahakama ya Malindi yawaachilia washukiwa 3 wa kesi ya Kwa Binzaro

Mahakama Kuu ya Malindi imewaachilia washukiwa watatu wanaohusishwa na kesi ya mauaji ya halaki ya watu katika kijiji cha Kwa Binzaro eneo bunge la Magarini kaunti ya Kilifi.
Hakimu wa Mahakama hiyo Joy Wesonga aliagiza kuachiliwa huru kwa Safari Kenga Nzai, Gona Charo Kalama na Kahindi Kazungu Garama wote wakiwa wakaazi wa kijiji hicho cha Kwa Binzaro.
Watatu hao walikuwa wamekamatwa baada ya kudaiwa kuuza shamba la ekari tano kwa mshukuwa mkuu wa mauaji ya watu katika kijiji cha Kwa Binzaro Sherleen Temba Anido.
Hakimu Wesonga aliwaagiza washukiwa hao kuhakikisha wanasalimisha nakala za vitambulisha vyao vya kitaifa kwa idara husika, kuripoti kwa Naibu Chifu wa eneo hilo mara mbili kwa wiki pamoja na kujisalimisha kwa maafisa wa upelelezi wa kesi hiyo mara moja kila baada ya wiki mbili.

Miili iliyofukuliwa katika kijiji cha Kwa Binzaro
Wakati huo huo upande wa mashtaka ukiongozwa na Naibu mkurugenzi wa mashtaka ya umma Jamie Yamina, uliomba kuwasilisha watu wengine wanne Mahakamani ikiwemo Jairus Otieno na mkewe Lilian Akinyi, Kahonzi Katana Karisa na Loise Zawadi waliojionda kama washukiwa na kugeuka kuwa mashahidi wa serikali.
Upande wa mashtaka pia uliaka kupewa siku 60 zaidi kuendelea kuzuiliwa kwa washukiwa wakuu Sherleen Temba Anido, James Kahindi Kazungu, Thomas Mukunwe na Kahidi Kazungu Garama katika kituo cha polisi cha Ngerenya, Kilifi, Watamu na Kijipwa ili kukamilisha uchunguzi wao kwani wanne hao wanakabiliwa na mashtaka ya itikadi kali, ugaidi, kujihusisha na uhalifu na kupanga mauaji.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Chrispus aomba msahama bunge la kaunti ya Taita Taveta

Mwakilishi wadi ya Bomani mjini Taveta kaunti ya Taita Taveta Chrispus Tondoo ameliomba bunge la kaunti hiyo msamaha kutokana na matamshi aliyoyatoa hapo awali akikashifu bunge hilo kwa madai ya kushamiri kwa visa vya ufisadi na utepetevu.
Tondoo akiomba msamaha katika bunge hilo alisema alitambua athari zilizosababishwa na matamshi hayo kwa wenyeji wa kaunti hiyo na bunge hilo, hali ambayo imemfanya kuchukua hatua hiyo ya kuomba msamaha.
Aidha Tondoo aliahidi kuliheshimu bunge hilo kwa mujibu wa kanuni na Sheria za bunge la kaunti ya Taita Taveta.
‘’Naomba msamaha kutokana na matamshi ambayo niliyatoa tarehe 2 na tarehe 3 mwezi wa Juni mwaka huu wa 2025 kwani hayakuwa yenye heshima kwa wenyeji wa Taita Taveta na bunge la kaunti’’, alisema Tondoo.
Tondoo alikuwa Mwakikishi wa wadi wa pili kuomba msamaha baada ya Mwakilishi wa wadi ya Kaloleni mjini Voi Ahmed Azari kuchukua hatua hiyo mwezi mmoja uliyopita.
Haya yalijiri baada ya kaimu spika wa bunge hilo Anselim Mwadime kuapa kuwachulia hatua za kisheria wanachama wanne wa bunge hilo, wawili wakiwa ni Tondoo na Azari ambayo tayari wameomba msamaha huku wawili wakiwa wamesalia bila kuomba msamaha.
Taarifa ya Janet Mumbi