News
Serikali yatenga shilingi milioni 250 kwa Walemavu.

Serikali kupitia Wizara ya Leba na maslahi ya kijamii imetenga shilingi milioni 250 mwaka wa 2025 ili kuimarisha uwezeshaji wa watu wanaoishi na ulemavu nchini.
Katibu mkuu wa wizara hiyo Joseph Motari alitangaza kuwa ufadhili huo utasaidia masuala ya elimu, kuwawesha kiuchumi pamoja na teknolojia kwa jamii hiyo.
Motari alibainisha hayo wakati wa kikao cha 18 cha mkutano wa nchi wanachama wa mkataba wa haki za watu wenye ulemavu (CRPD) jijini New York nchini Marekani.
“Kenya inaongeza juhudi zake za kujumuisha uchumi kwa kutenga zaidi ya shilingi milioni 250 mwaka huu kupitia msaada wa elimu, uwezeshaji wa kiuchumi na msaada wa kiteknolojia”, Motari alisema.
Katibu huyo pia aliangazia utekelezaji wa mpangilio wa mkakati wa mwaka 2023-27 ambao unayapa kipaumbela masuala ya ufahamu, uwezeshaji wa kijamii na kiuchumi, vile vile ujumuishaji wa kidijitali kwa watu wanaoishi na ulemavu.
Kulingana na Motari, takribani makaazi elfu 63 yatanufaika na program za serikali za kusambaza pesa na upokezaji wa marupurupu ya kila mwezi ya shilingi elfu mbili.
Kati ya hao zaidi ya walengwa elfu 20 wanafadhiliwa chini ya mpango ujulikanao kama Autism and Developmental Disabilities programme.
Mwaka 2024, serikali ilisambaza takriban vifaa 4,200 vya usaidizi kwa jamii hiyo pamoja na kutoa ufadhili wa masomo kwa wanafunzi 2,500 wanaoishi na ulemavu.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Papa Leo XIV amteua Askofu wa kwanza kutoka China

Makao makuu ya Kanisa Katoliki duniani mjini Vatican ilitangaza uteuzi wa kwanza wa Askofu mwenye asili ya China chini ya usimamizi wa Papa Leo XIV.
Hii inaashiria uungaji mkono wa Papa mpya kwa makubaliano yenye utata juu ya uteuzi uliyopingwa na mtangulizi wake na Beijing.
Ofisi ya Vatican imeeleza kuridhishwa na China kwa kutambua kuteuliwa kwa Joseph Lin Yuntuan kama Askofu msaidizi wa Fuzhou, mji mkuu wa jimbo la Fujian kusini mashariki.
Papa alifanya uteuzi huo tarehe 5 mwezi Juni mwaka huu wa 2025.
“Tukio hili linawakilisha matunda zaidi ya mazungumzo kati ya kiti kitakatifu na Mamlaka ya China na ni hatua muhimu katika safari ya Jumuiya ya dayosisi,” ilisema katika taarifa.
Uongozi wa Vatican na ule wa Kikomunisti wa China hauna uhusiano rasmi wa kidiplomasia, kwani Vatican inaitambua Taiwan huku Beijing ikidai kisiwa hicho kinachojitawala ni eneo lake.
Lakini katika makubaliano ya kihistoria, walikubaliana mwaka 2018 kuruhusu pande zote mbili kuwa na usemi katika kuwataja maaskofu nchini China, ambayo ina takriban Wakatoliki milioni 12.
Hata hivyo hayati Papa Francis alipokuwa akitafuta nafasi ya Kanisa kuingia nchini China, mkataba huo ulifanywa upya mara kadhaa, wa hivi karibuni ikiwa ni mnamo Oktoba 2024, baada ya mda wa miaka minne.
Papa Francis alifariki Aprili 21 mwaka 2025 baada ya miaka 12 ya kuhudumu kama Kiongozi wa waumini wa Kanisa katoliki duniani wapatao bilioni 1.4 na Papa Leo alichaguliwa katika kongamano la Makadinali Mei 8 mwaka 2025.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Inspekta Jenerali Kanja aomba Msamaha.

Inspekta Jenerali wa polisi Douglas Kanja ameomba msamaha kwa kutoa ripoti isiyo sahihi kuhusu uchunguzi wa mauaji dhidi ya mwalimu na mwanablogu Albert Ojwang.
Mapema wiki hii, Kanja alidai kuwa Ojwang alifariki kwa kujitoa uhai baada ya kujigonga kichwa kwenye kuta za seli za polisi.
Madai hayo yalizua taharuki miongoni mwa wananchi ambao walishutumu polisi kwa kujaribu kuficha ukweli kuhusu kifo cha mwanablogu huyo.
Wakati wa kikao cha bunge la seneti siku ya jumatano tarehe 11 mwaka 2025, inspekta jenerali Kanja alilaani mauaji hayo na kudai hangeweza kutoa tamko lolote hadi mamlaka huru ya kutathmini utendakazi wa polisi (IPOA) ikamilishe uchunguzi wake.
Pia aliapa kuwachukulia hatua maafisa wa polisi waliompatia ripoti hiyo akitaja taratibu za kinidhamu zitaambatana na taratibu za kawaida za uendeshaji.
“Ikiwa katika uchunguzi unaoendelea na IPOA tutajua ukweli, maafisa waliotoa ripoti ya awali watalazimika kukabiliwa na taratibu za kinidhamu, kutokana na kile tulichosikia hapa, tutaendelea na kuchukua hatua zinazohitajika dhidi ya afisa aliyetupa nyenzo siku hiyo,” Kanja alisema.
Hata hivyo maseneta hao walipinga matamshi ya Kanja na kudokeza kuwa IPOA imefutilia mbali madai ya Ojwang’ kujiua kufuatia kutolewa kwa matokeo ya uchunguzi wa maiti.
Ripoti ya upasuaji wa maiti ya mwanapatholojia wa serikali Bernard Midia , ilithibitisha kuwa Ojwang alitendewa ukatili, kunyongwa, kuteswa na kuuawa na maafisa wa polisi.

Albert Ojwang’ mwalimu na mwanablogu anayedaiwa kuuawa na maafisa wa polisi.
Kisa cha mauaji ya mwanablogu huyo Albert Ojwang’ kilizua mihemko miongoni mwa wakenya huku baadhi ya vijana pamoja na wanaharakati wa kutetea haki za kibinadam nchini wakiandamana wakishinikiza naibu inspekta mkuu wa polisi Eliud Lagat kujiuzulu na kuchukuliwa hatua za kisheria.
Taarifa ya Joseph Jira