News
Rais Ruto kuelekea nchini Uhispania na Uingereza

Rais William Ruto anatarajiwa kuondoka humu nchini na kuelekea nchini Uhispania na Uingereza kwa ziara ya kiserikali.
Kulingana na taarifa iliyotolewa na Ikulu ya Rais na kutiwa saini na Msemaji wa Ikulu Hussein Mohammed, Rais Ruto anatarajiwa kuondoka nchini leo Jumapili Juni, 29 na kuwasili katika jiji la Seville nchini Uhispania.
Katika taifa hilo, Kiongozi wa nchi amepangiwa kuhudhuria Kongamano la Nne la kimataifa la ufadhili wa Maendeleo ambapo viongozi mbalimbali wa kimataifa wataangazia kanuni mpya za ufadhili wa maendeleo.
Rais Ruto anatarajiwa kutetea kufufuliwa kwa mfumo wa kimataifa wa kushughulilia masuala ya muda mrefu kama vile umaskini uliokithiri, kuongezeka kwa ukosefu wa usawa na msukosuko wa kiuchumi pamoja na mabadiliko ya hali ya hewa na upotevu wa viumbe hai.
Rais Ruto pia ataongoza kikao cha ngazi ya juu wakati wa Kongamano hilo na kufanya mazungumzo na marais wa mataifa mbalimbali pamoja na Waziri mkuu wa Uhispania Pedro Sanchez na Mfalme Felipe wa Sita.
Hata hivyo baadaye ataelekea nchini Uingereza ambapo atatia saini ubai mpya wa kimkakati baina ya Kenya na Uingereza uliowekwa ili kufungua uwekezaji, kubuni nafasi za ajira na kukuza ushindani wa kimataifa wa Kenya katika biashara, hali ya hewa, teknolojia na usalama.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Wazee wa Kaya wanataka bunge kupitisha sheria kudhibiti mauaji ya wazee

Muungano wa Wazee wa Kaya kaunti ya Kilifi umeitaka serikali kuu kupitia bunge la kitaifa kubadilisha sheria ya mwaka wa 1926 kuhusu uchawi ili kuwezesha utamaduni kudhibiti mauaji ya wazee yanayoendelea kushuhudiwa kaunti ya Kilifi.
Wakiongozwa na Stanley Kahindi Kiraga wamesema kuwa sheria hiyo imechangia pakubwa mauaji ya wakongwe Kilifi kutokana na swala kuwa haitambui uwepo wa uchawi na jinsi ya kuudhibiti.
Kiraga sasa anasema ni sharti sheria hiyo iondolewe au ifanyiwe ukarabati bungeni hali itayopelekea uchawi kudhibitiwa kupitia mila na utamaduni.
“Vijana wanaowaua wazee wakiwasingizia kuwa wachawi wanazidi kuongezeka na kwa sababu hakuna sheria ya moja kwa moja ya kuwashtaki na kuwafunga” amesema Kiraga akieleza kusikitishwa kwake na ongezeko la magenge ya vijana wanaolipwa kutekelezwa mauaji ya wazee kwa shutuma za uchawi.
Taarifa ya Hamis Kombe
News
Mahakama ya Kilifi yaanzisha upya kesi ya ulaghai wa pesa

Mahakama ya Kilifi imeanzisha upya kesi ya mwanaume mmoja anayekabiliwa na shtaka la ulaghai wa pesa.
Hii ni baada ya Mwanaume huyo kwa jina Samuel Ngonyo, kuachiliwa kwa dhamana hapo awali lakini alikosa kudhuhuria vikao Mahakamani hali iliyopelekea kesi hiyo kuanzishwa upya.
Hakimu mkuu wa Mahakama hiyo Charles Obulutsa aliagiza jamaa huyo kuzuliwa rumande baada ya agizo la kukamatwa kwake kuidhinishwa na Mahakama baada ya jamaa huyo kupuuza vikao vya Mahakama vya awali.
Kabla ya agizo hilo, Mahakama ilielezwa kwamba mnamo tarehe tofauti kati ya mwezi Septemba hadi Oktoba mwaka 2021 katika maeneo la Ganze kaunti ya Kilifi kwa kutumia njia ya ulaghai, mshukiwa alichukua pesa taslimu shilingi elfu 50 ya mlalamishi Grace Sidi Katana.
Mahakama ilielezwa zaidi kwamba mshukiwa alitekeleza kitendo hicho baada kumdanganya Mlalamishi kwamba yeye ni Mwandishi na afisa wa kazi za umma hivyo angemsaidia Moses Katana mtoto wa mlalamishi kupata kazi ya serikali.
Kesi hiyo itaendelea mnamo tarehe 13 mwezi Agosti mwaka huu.
Taarifa ya Mwanahabari wetu