News
Rais Ruto kuelekea nchini Uhispania na Uingereza

Rais William Ruto anatarajiwa kuondoka humu nchini na kuelekea nchini Uhispania na Uingereza kwa ziara ya kiserikali.
Kulingana na taarifa iliyotolewa na Ikulu ya Rais na kutiwa saini na Msemaji wa Ikulu Hussein Mohammed, Rais Ruto anatarajiwa kuondoka nchini leo Jumapili Juni, 29 na kuwasili katika jiji la Seville nchini Uhispania.
Katika taifa hilo, Kiongozi wa nchi amepangiwa kuhudhuria Kongamano la Nne la kimataifa la ufadhili wa Maendeleo ambapo viongozi mbalimbali wa kimataifa wataangazia kanuni mpya za ufadhili wa maendeleo.
Rais Ruto anatarajiwa kutetea kufufuliwa kwa mfumo wa kimataifa wa kushughulilia masuala ya muda mrefu kama vile umaskini uliokithiri, kuongezeka kwa ukosefu wa usawa na msukosuko wa kiuchumi pamoja na mabadiliko ya hali ya hewa na upotevu wa viumbe hai.
Rais Ruto pia ataongoza kikao cha ngazi ya juu wakati wa Kongamano hilo na kufanya mazungumzo na marais wa mataifa mbalimbali pamoja na Waziri mkuu wa Uhispania Pedro Sanchez na Mfalme Felipe wa Sita.
Hata hivyo baadaye ataelekea nchini Uingereza ambapo atatia saini ubai mpya wa kimkakati baina ya Kenya na Uingereza uliowekwa ili kufungua uwekezaji, kubuni nafasi za ajira na kukuza ushindani wa kimataifa wa Kenya katika biashara, hali ya hewa, teknolojia na usalama.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Anselim, ashutumu utovu wa usalama Taita Taveta

Kaimu Spika katika bunge la kaunti ya Taita Taveta Anselim Mwadime alieleza kusikitishwa na mauaji ya mhudumu mmoja wa bodaboda aliyeuliwa na kisha pikipiki yake kuchukuliwa katika eneo la chuo kikuu cha Taita Taveta.
Mwadime alisema kuna baadhi ya abiria ambao ni wahuni hubebwa na kisha kuwashambulia wahudumu wa pikipiki hadi kuwaua au hata kutoweka na pikipiki.
Aidha, Mwadime alisema kama viongozi wa kaunti ya Taita Taveta hawataruhusu visa hivyo kuendelezwa katika kaunti hiyo.
Vilevile, Mwadime aliishinikiza idara ya usalama kwenye kaunti ya Taita Taveta kuwajibika ipasavyo ili kudhibiti visa vya utovu wa usalama katika sekta ya bodaboda na wanaohusika wakabiliwe kisheria.
“Hili jambo linafaa kufuatiliwa kwa undani. Na tunalilaani vikali sisi kama viongozi wa Taita Taveta’’ alisema Mwadime.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Viongozi wahimizwa kushirikiana kubuni ajira kwa vijana

Mwakilishi wa wadi ya Sabaki eneo bunge la Magarini kaunti ya Kilifi Rose Baraka alitoa wito kwa viongozi wa kaunti ya Kilifi kushirikiana na mashirika ya kijamii pamoja na wawekezaji katika kaunti ya Kilifi ili kudhibiti changamoto za ukosefu wa ajira miongoni mwa vijana.
Rose alisema hatua hiyo itasaidia pakubwa kuwaepusha vijana kujiingiza kwenye utumizi wa mihadarati sawa na uhalifu.
Akizungumza wakati wa kikao kilichowaleta pamoja maafisa wa shirika la SHOFCO pamoja na wakaazi wa Sabaki, Rose aliahidi kushirikiana na mashirika mbalimbali ya kijamii katika juhudi za kuwasadia wananchi kujiendeleza kupitia mpango wa ajira.
“Vijana ni wengi, kazi ni kidogo. Sisi kama viongozi tunastahili kutia bidii kutafuta haya mashirika ili tuangalie vijana wetu wasaidika vipi’’ alisema Rose Baraka.
Kwa upande wake Afisa wa Shirika la SHOFCO eneo la Magarini Kelvin Mtawali Karisa aliupongeza ushirikiano wa mwakilishi wa wadi huyo na shirika hilo na kuwataka vijana kujiunga kwenye makundi mbalimbali ili waweze kupata mikopo ya kujiendeleza kimaisha.
Taarifa ya Janet Mumbi