News
Rais Ruto atia saini Miswada miwili kupiga jeki Mgao wa Serikali za Kaunti

Rais William Ruto ametia saini na kuwa sheria miswaada miwili muhimu inayokusudiwa kupiga jeki ufadhili wa Serikali za Ugatuzi nchini.
Rais Ruto ambaye anahudhuria Kongamano la Ugatuzi mwaka huu katika kaunti ya Homa Bay, ametia saini mswada kuhusu Ugavi wa pato la serikali kwa hazina za Kaunti wa 2025, na pia Mswada mwengine unaotoa muongozo wa matumizi ya fedha za serikali za Kaunti wa 2023.
Mswaada unaohusu usimamizi na muongozo wa matumizi ya pesa za kaunti sasa umefutiliwa mbali na kubuni Hazina ya mabunge ya Kaunti zote 47.
Mswaada huo wa nyongeza ya pato kwa kaunti umeongoza kiwango cha hapo awali kutoka Shilingi billioni 387.4 mwaka uliopita hadi kiwango cha Shilingi bilioni 415 katika kipindi cha mwaka huu 2025/26 cha matumizi ya pesa serikalini.
Hafla hiyo ya kutia saini miswaada hiyo miwili,imefanyika katika Ikulu ndogo kaunti ya Homabay Jumatano Agostu 13 2025.
Mswaada huo uliowasilishwa bungeni na Senta wa Meru Kathuri Murungi, unayapa uhuru zaidi Mabunge ya Kaunti katika masuala ya usimamizi wa fedha zao.
Hatua hiyo imetokea wakati Kongamano la Ugatuzi limefunguliwa rasmi katika Kaunti ya Homabay, kutathmini mafanikio na changamoto kwa serikali za Kaunti.
Kongamano hilo linahudhuriwa miongoni mwa wengine Wafanyi biashara na washika Dau mbali mbali wa kimaendeleo katika ngazi za Kaunti.
Hazina kuu ya Serikali sasa inatarajiwa kuhakikisha kuwa mgao huo wa fedha unafikia hazina za serikali za Kuanti kabla ya tarehe 15 ya kila mwezi
Katika muda wa miaka miwili iliyopita serikali kuu ya kitaifa imeshtumiwa vikali na Baraza la Magavana, kwa madai ya njama za kuhujumu Ugatuzi nchini.
Taarifa ya Eric Ponda
News
Maandalizi ya Maadhimisho ya Chenda Chenda

Ni dhahiri sasa kutakuwa maaadhimisho ya Chenda Chenda siku ya Jumanne Septemba 9, 2025 kwa wakati mmoja katika kaunti ya Kwale na kaunti ya Kilifi.
Waasisi wa maadhimisho haya ambao ni wWazee wa kutoka Kaya zote za Wamijikenda walitangaza mwaka uliopita kwamba maadhimisho ya mwaka huu yafanyika katika kaunti ya Kwale baada ya kuandaliwa eneo la Kaya fungo kaunti ya Kilifi mwaka jana.
Na baada ya vikao vya mashauriano baina ya Wazee wa Kaya zote hivi majuzi katika eneo la Rabai, Wazee hao waliafikiana kwa kauli moja kwamba maadhimisho hayo ya mwaka huu yaandaliwe katika Kaya ya Mtswakara eneo bunge la Kinango katika Kaunti ya Kwale.
Lakini baada ya tangazo hilo kutolewa, serikali ya kaunti ya Kilifi ilitangaza kufanya maadhimisho hayo katika uwanja wa chuo kikuu cha Pwani.
Tangazo hilo liliwaghadhabisha mno Wazee wa Kaya ambao katika taarifa kwa Wanahabari walisema wanaendelea na mipango ya maadhimisho hayo katika kaunti ya Kwale.

Maandalizi ya Maadhimisho ya Chenda Chenda, kaunti ya Kilifi
Hali hii imezua tofauti kubwa baina ya Gavana wa kaunti ya Kilifi Gedion Maitha Mung’aro anayedaiwa kuenda kinyume na utaratibu wa tamaduni za Kaya, ambapo maadhimisho hayo yanapasa kufanyika katika viwanja vya Kaya kama njia moja ya kuwaheshimu wavyele wa Kaya za Kimijikenda.
Huku hayo yakijiri maandalizi ya maadhimisho hayo yanaendelea katika uwanja wa Chuo kikuu cha Pwani.
Wazee wa Kaya wanalaumu kitendo hiki na kuongeza kwamba maandalizi haya yanamsukumo wa kisiasa na wala sio ule wa kitamaduni na unaokusudiwa kuleta umoja wa Wamijikenda.
Taarifa ya Eric Ponda
News
Jopo la kushughulikia fidia kwa waathiriwa wa maandamano laanza kazi

Jopo lililoundwa na Rais William Ruto kushughulikia masuala ya fidia ya waathiriwa wa ukatili wa polisi wakati wa maadamano limeanza kikao cha wiki moja huku mjadala kuhusu uhalali na uwazi wa jopo hili ukitiliwa shaka na kupokea upinzani mkali kutoka kwa baadhi ya wanaharakati wa kutetea haki za kibinadamu na viongozi wa upinzani.
Jopo hilo linaongozwa na Prof. Makau Mutua na naibu wake Rais wa Chama cha Wanasheria nchini (LSK), Faith Odhiambo, ambaye uteuzi wake umeibua mjadala mkali.
Baadhi ya Wanasheria walimshutumu Odhiambo kwa “kusaliti haki,” lakini yeye alisisitiza kwamba jukumu lake ni kuhakikisha waathiriwa wa ukatili wa polisi wanapata haki waliyoikosa kwa muda mrefu.
Aliongeza kuwa jopo hilo lina nafasi ya kuleta mabadiliko ya kihistoria katika upatikanaji wa fidia kwa waathiriwa.
Kwa mujibu wa maelezo yake, jopo hilo si tume ya kikatiba wala chombo cha kisheria chini ya Katiba, bali ni jopo la ushauri lililoanzishwa na Rais chini ya Kifungu cha 132(4)(a).
Vile vile alibainisha kuwa wanachama wa jopo hilo si maafisa wa umma hivyo uteuzi wao hauhitaji mchakato wa Tume ya Utumishi wa Umma kwa mujibu wa Kifungu cha 260 cha Katiba.

Jopo lililoundwa na Rais William Ruto kushughulikia ya fidia ya waathiriwa wa maadamano
Hata hivyo, wakosoaji walisema linaweza kukiuka mamlaka ya ofisi huru kama Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP), Inspekta Jenerali wa Polisi na Tume ya Kitaifa ya Haki za Binadamu (KNCHR). Jopo hilo limekanusha madai hayo, likisema jukumu lake ni kusaidia na sio kuchukua nafasi ya taasisi zilizopo.
Wapo pia wanaouliza uhalali wa serikali kuwalipa fidia waathiriwa ilhali serikali hiyo hiyo imeshtumiwa kwa mauaji, kutoweka kwa baadhi ya wakosoaji wa serikali kwa njia tatanishi na kuacha familia na majeraha yasiyotibika.
Jopo hilo pia linasisitiza kikatiba, serikali ndiyo chombo kinachobeba wajibu wa kurekebisha madhila kwa niaba ya taifa. Hata kama madhara yalisababishwa na maafisa wa serikali, haitazuiwa kuwafidia waathiriwa.
Taarifa ya Elizabeth Mwende