News
Bi Rachel azindua mpango wa “lishe bora” shuleni

Ofisi ya mke wa Rais Bi Rachel Ruto, imezindua mpango wa lishe bora kupitia utoaji wa maziwa kwa watoto wa shule kama sehemu ya mpango wa kuboresha afya na kuongeza nguvu kwa watoto ili waweze kuendelea na masomo yao shuleni bila changamoto zozote.
Akingumza katika Shule ya msingi ya Kachororoni eneo bunge la Ganze kaunti ya Kilifi, Bi Rachel alisema mpango huo wa Feed One End Hunger ambao umefanikishwa kwa ushirikiano na Bodi ya Maziwa nchini KDB na Muungano wa ushirika wa maziwa, Meru utadhibiti utapiamlo kwa watoto.
Bi Rachel Ruto alisema wanafunzi wengi nchini ambao wanatoka kwenye familia zisizojiweza hasa kifedha wamekuwa wakisitisha masomo yao kutokana na njaa na utapiamlo kutokana na ukosefu wa lishe bora.
“Afya ya mtoto ni muhimu sana na ikiwa mpango huu wa lishe bora utakumbatiwa, wanafunzi wengi shuleni watafanya vyema katika masomo yao”, alisema Bi Rachel Ruto.
Kwa upande wake Katibu mkuu katika Wizara ya Kilimo nchini Jonathan Mueke ambaye alikuwa ameandamana na Bi Rachel Ruto aliupongeza mpango huo akiutaja kama hatua muhimu ya kufanikisha elimu shuleni.
Naye Naibu Gavana wa kaunti ya Kilifi Flora Mbetsa Chibule alisema tangu kuzinduliwa kwa mpango wa lishe shuleni kaunti ya Kilifi, wanafunzi wengi wamekuwa wakijiunga na shule mbalimbali ikilinganishwa na miaka ya nyuma na kuahidi kushirikiana na ofisi ya mke wa rais Bi Rachel Ruto katika kuhakikisha unafikishwa vilivyo.
Hata hivyo Mbunge wa Ganze Kenneth Kazungu Tungule alitoa wito kwa Rais William Samoei Ruto kujenga barabara ya Kilifi – Ganze – Bamba ili kuimarisha shughuli za uchukuzi eneo hilo.
Kauli ambayo iliungwa mkono na Mwakilishi wa Kike kaunti ya Kilifi Getrude Mbeyu, ambaye alisema eneo bunge la Ganze lina raslimali nyingi na huenda Ganze ikawa eneo tajiri zaidi nchini iwapo raslimali hizo zitatumika ipasavyo na kuipongeza Serikali kuu kupitia Wizara ya Utalii na wanyamapori nchini kutoa kima cha shilingi milioni 60 za fidia kwa wakaazi wa kaunti ya Kilifi walioathiriwa na wanyamapori.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Anselim, ashutumu utovu wa usalama Taita Taveta

Kaimu Spika katika bunge la kaunti ya Taita Taveta Anselim Mwadime alieleza kusikitishwa na mauaji ya mhudumu mmoja wa bodaboda aliyeuliwa na kisha pikipiki yake kuchukuliwa katika eneo la chuo kikuu cha Taita Taveta.
Mwadime alisema kuna baadhi ya abiria ambao ni wahuni hubebwa na kisha kuwashambulia wahudumu wa pikipiki hadi kuwaua au hata kutoweka na pikipiki.
Aidha, Mwadime alisema kama viongozi wa kaunti ya Taita Taveta hawataruhusu visa hivyo kuendelezwa katika kaunti hiyo.
Vilevile, Mwadime aliishinikiza idara ya usalama kwenye kaunti ya Taita Taveta kuwajibika ipasavyo ili kudhibiti visa vya utovu wa usalama katika sekta ya bodaboda na wanaohusika wakabiliwe kisheria.
“Hili jambo linafaa kufuatiliwa kwa undani. Na tunalilaani vikali sisi kama viongozi wa Taita Taveta’’ alisema Mwadime.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Viongozi wahimizwa kushirikiana kubuni ajira kwa vijana

Mwakilishi wa wadi ya Sabaki eneo bunge la Magarini kaunti ya Kilifi Rose Baraka alitoa wito kwa viongozi wa kaunti ya Kilifi kushirikiana na mashirika ya kijamii pamoja na wawekezaji katika kaunti ya Kilifi ili kudhibiti changamoto za ukosefu wa ajira miongoni mwa vijana.
Rose alisema hatua hiyo itasaidia pakubwa kuwaepusha vijana kujiingiza kwenye utumizi wa mihadarati sawa na uhalifu.
Akizungumza wakati wa kikao kilichowaleta pamoja maafisa wa shirika la SHOFCO pamoja na wakaazi wa Sabaki, Rose aliahidi kushirikiana na mashirika mbalimbali ya kijamii katika juhudi za kuwasadia wananchi kujiendeleza kupitia mpango wa ajira.
“Vijana ni wengi, kazi ni kidogo. Sisi kama viongozi tunastahili kutia bidii kutafuta haya mashirika ili tuangalie vijana wetu wasaidika vipi’’ alisema Rose Baraka.
Kwa upande wake Afisa wa Shirika la SHOFCO eneo la Magarini Kelvin Mtawali Karisa aliupongeza ushirikiano wa mwakilishi wa wadi huyo na shirika hilo na kuwataka vijana kujiunga kwenye makundi mbalimbali ili waweze kupata mikopo ya kujiendeleza kimaisha.
Taarifa ya Janet Mumbi