News
Bi Rachel azindua mpango wa “lishe bora” shuleni

Ofisi ya mke wa Rais Bi Rachel Ruto, imezindua mpango wa lishe bora kupitia utoaji wa maziwa kwa watoto wa shule kama sehemu ya mpango wa kuboresha afya na kuongeza nguvu kwa watoto ili waweze kuendelea na masomo yao shuleni bila changamoto zozote.
Akingumza katika Shule ya msingi ya Kachororoni eneo bunge la Ganze kaunti ya Kilifi, Bi Rachel alisema mpango huo wa Feed One End Hunger ambao umefanikishwa kwa ushirikiano na Bodi ya Maziwa nchini KDB na Muungano wa ushirika wa maziwa, Meru utadhibiti utapiamlo kwa watoto.
Bi Rachel Ruto alisema wanafunzi wengi nchini ambao wanatoka kwenye familia zisizojiweza hasa kifedha wamekuwa wakisitisha masomo yao kutokana na njaa na utapiamlo kutokana na ukosefu wa lishe bora.
“Afya ya mtoto ni muhimu sana na ikiwa mpango huu wa lishe bora utakumbatiwa, wanafunzi wengi shuleni watafanya vyema katika masomo yao”, alisema Bi Rachel Ruto.
Kwa upande wake Katibu mkuu katika Wizara ya Kilimo nchini Jonathan Mueke ambaye alikuwa ameandamana na Bi Rachel Ruto aliupongeza mpango huo akiutaja kama hatua muhimu ya kufanikisha elimu shuleni.
Naye Naibu Gavana wa kaunti ya Kilifi Flora Mbetsa Chibule alisema tangu kuzinduliwa kwa mpango wa lishe shuleni kaunti ya Kilifi, wanafunzi wengi wamekuwa wakijiunga na shule mbalimbali ikilinganishwa na miaka ya nyuma na kuahidi kushirikiana na ofisi ya mke wa rais Bi Rachel Ruto katika kuhakikisha unafikishwa vilivyo.
Hata hivyo Mbunge wa Ganze Kenneth Kazungu Tungule alitoa wito kwa Rais William Samoei Ruto kujenga barabara ya Kilifi – Ganze – Bamba ili kuimarisha shughuli za uchukuzi eneo hilo.
Kauli ambayo iliungwa mkono na Mwakilishi wa Kike kaunti ya Kilifi Getrude Mbeyu, ambaye alisema eneo bunge la Ganze lina raslimali nyingi na huenda Ganze ikawa eneo tajiri zaidi nchini iwapo raslimali hizo zitatumika ipasavyo na kuipongeza Serikali kuu kupitia Wizara ya Utalii na wanyamapori nchini kutoa kima cha shilingi milioni 60 za fidia kwa wakaazi wa kaunti ya Kilifi walioathiriwa na wanyamapori.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Mvuvi aliyezama baharini Watamu apatikana Tanariver

Mwili wa mvuvi Hudhefa Laly aliyepotea baharini huko Watamu eneo bunge la Kilifi Kaskazini Kaunti ya Kilifi akiwa na ndugu yake Athman Laly umepatikana eneo la Shakiko -Mathole, kaunti ya Tana River.
Ndugu hao wawili walitoweka habarini siku ya Alhamisi 24, Julai 2025 katika bahari hindi wakati wakiendelea na shughuli zao za uvuvi.
Vitengo mbali mbali vya uokozi vimekuwa vikiendesha zoezi la kutafuta miili ya wawili hao kwa ushirikiano na wavuvi eneo la Watamu.
Kufikia sasa mwili wa Athman Laly kakake Hudhefa ungali haujapatikana huku juhudi za kuutafuta zikiendelea.
Jamii ya wavuvi katika eneo la Watamu ikiongozwa na kiongozi wa vijana Bakari Shaban iliiomba serikali ya kaunti ya Kilifi na ile ya kitaifa kununua boti za uokozi ili kusaidia kuokoa maisha wakati kunapotokea dharura baharini.
“Tunaomba tupate boti za kuokoa maisha baharini, popote alipo waziri Ali Joho angalau tupate boti za uokozi kama mbili hapa Watamu ni kitovu cha utalii kunamahoteli mengi, watalii wote wanaokuja Watamu mpaka leo hakuna boti za uokozi”, alisema Shaban.
Awali wao wazazi wa wavuvi waliopotea baharini Lali Athman Lali na Dhurai Mohamed Ali waliiomba serikali kuweka juhudi zaidi za kuwasaidia kuwapata wanawao kwani ndio tegemeo kubwa kwa familia yao.
“Uko usaidizi unatumika, kuna vijana wanaojitolea kwa maboti wanaenda ile sehemu ambayo wavuvi wanavua, wanajaribu kuzunguka lakini toka siku hiyo hawajapata chochote: Katika Maisha yangu mimi nawategemea hawa watoto kunisomeshea hawa watoto wangu ambao ni wadogo zao mashule, kwa chakula kwa hivyo naomba serikali inisaidie kwa sababu ndio tegemeo langu hao watoto”.walisema wazazi.
Kisa hiki kilijiri miezi kadhaa baada ya mvuvi mmoja kutoka eneo la Mnarani mjini Kilifi kufariki baharini baada ya kugongwa kichwani kwa pondo na wavuvi wenzake kulipotokea mzozo kuhusu pato la samaki.
Kufikia sasa mwili wa mvuvi huyo haujapatikana.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Mombasa inaongoza kwa maambukizi ya MPOX nchini

Wizara ya afya nchini imesema kaunti ya Mombasa inaongoza kwa visa vya maambukizi ya ugonjwa wa Mpox.
Kwa mujibu wa mkurugenzi mkuu wa idara ya afya nchini Daktari Patrick Amoth, kaunti ya Mombasa imerekodi visa 139 kati ya visa 300 vilivyoripotiwa na wizara hiyo.
Amoth alidokeza kuwa serikali itatangaza siku maalum ya kutoa chanjo ya kudhibiti msambao wa ugonjwa huo wakishirikiana na shirika la afya ulimwenguni WHO.
Mkurugenzi huyo vile vile alimesema zoezi hilo litaambatana na hamasa kwa wananchi kuhusu namna ya kujikinga na maambukizi zaidi.
“Kwa wakati huu Mombasa ndio inaongoza kwa idadi ya visa 139 kwa hivyo tuchuke tahadhari kuhakikisha kwamba tunazuia maambukizi, na tunafanya mpango pamoja na shirika la afya duniani WHO, hapa tutakuja na mpango wa chanjo na ikifika huo wakati tunaomba watu wajitokeze wapate chanjo ili wapate kinga”,alisema Daktari Amoth.
Wakati huo huo Amoth aliokeza kuwa uchunguzi wa vifo vya watu wanne walioaga dunia wiki chache zilizopita huko Migadini, eneo bunge la Changamwe kaunti ya Mombasa umebaini walifariki kutokana na magonjwa mengine na wala sio maambukizi ya ugonjwa wa MPOX kama ilivyodhaniwa na wakaazi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu.