News
Pigo kwa Spika Mwambire, apokonywa walinzi

Karani wa bunge la kaunti ya Kilifi Emmanuel Ngala ameagiza kuondolewa kwa walinzi wanaolinda makaazi ya Spika wa bunge la kaunti hiyo Teddy Mwambire.
Kulingana na barua iliyoandikwa na Ngala kupitia bunge hilo na kuwasilishwa kwa Spika Mwambire, walinzi wote ambao wanalinda makaazi ya Spika huyo kupitia kampuni ya Ulinzi ya Ismax, hawatatekeleza tena majukumu yao.
Barua hiyo pia imefafanua kwamba hatua hiyo ni kutokana na bunge la kaunti ya Kilifi kumtimua Mamlakani Spika Mwambire Juni 30 mwaka huu baada ya Wawakilishi wadi 40 kati ya 51 kupiga kura ya kutokuwa na imani naye na kumbadua ofisini.
Barua hiyo hata hivyo imeweka wazi kwamba itamlazima Mwambire kutumia walinzi wa kibinafsi katika kufanikisha usalama wake na wala sio walinzi wanaotambulika na bodi ya bunge la kaunti ya Kilifi.
Haya yamejiri huku Spika Mwambire akipata idhini ya Mahakama kuu ya Malindi kuendelea na majukumu yake ya kikazi kufuatia kesi ambayo iliwasilishwa Mahakamani na wakenya wawili wanaopinga uamuzi wa bunge hilo wa kumtimua ofisini Spika Mwambire.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Mvuvi aliyezama baharini Watamu apatikana Tanariver

Mwili wa mvuvi Hudhefa Laly aliyepotea baharini huko Watamu eneo bunge la Kilifi Kaskazini Kaunti ya Kilifi akiwa na ndugu yake Athman Laly umepatikana eneo la Shakiko -Mathole, kaunti ya Tana River.
Ndugu hao wawili walitoweka habarini siku ya Alhamisi 24, Julai 2025 katika bahari hindi wakati wakiendelea na shughuli zao za uvuvi.
Vitengo mbali mbali vya uokozi vimekuwa vikiendesha zoezi la kutafuta miili ya wawili hao kwa ushirikiano na wavuvi eneo la Watamu.
Kufikia sasa mwili wa Athman Laly kakake Hudhefa ungali haujapatikana huku juhudi za kuutafuta zikiendelea.
Jamii ya wavuvi katika eneo la Watamu ikiongozwa na kiongozi wa vijana Bakari Shaban iliiomba serikali ya kaunti ya Kilifi na ile ya kitaifa kununua boti za uokozi ili kusaidia kuokoa maisha wakati kunapotokea dharura baharini.
“Tunaomba tupate boti za kuokoa maisha baharini, popote alipo waziri Ali Joho angalau tupate boti za uokozi kama mbili hapa Watamu ni kitovu cha utalii kunamahoteli mengi, watalii wote wanaokuja Watamu mpaka leo hakuna boti za uokozi”, alisema Shaban.
Awali wao wazazi wa wavuvi waliopotea baharini Lali Athman Lali na Dhurai Mohamed Ali waliiomba serikali kuweka juhudi zaidi za kuwasaidia kuwapata wanawao kwani ndio tegemeo kubwa kwa familia yao.
“Uko usaidizi unatumika, kuna vijana wanaojitolea kwa maboti wanaenda ile sehemu ambayo wavuvi wanavua, wanajaribu kuzunguka lakini toka siku hiyo hawajapata chochote: Katika Maisha yangu mimi nawategemea hawa watoto kunisomeshea hawa watoto wangu ambao ni wadogo zao mashule, kwa chakula kwa hivyo naomba serikali inisaidie kwa sababu ndio tegemeo langu hao watoto”.walisema wazazi.
Kisa hiki kilijiri miezi kadhaa baada ya mvuvi mmoja kutoka eneo la Mnarani mjini Kilifi kufariki baharini baada ya kugongwa kichwani kwa pondo na wavuvi wenzake kulipotokea mzozo kuhusu pato la samaki.
Kufikia sasa mwili wa mvuvi huyo haujapatikana.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Mombasa inaongoza kwa maambukizi ya MPOX nchini

Wizara ya afya nchini imesema kaunti ya Mombasa inaongoza kwa visa vya maambukizi ya ugonjwa wa Mpox.
Kwa mujibu wa mkurugenzi mkuu wa idara ya afya nchini Daktari Patrick Amoth, kaunti ya Mombasa imerekodi visa 139 kati ya visa 300 vilivyoripotiwa na wizara hiyo.
Amoth alidokeza kuwa serikali itatangaza siku maalum ya kutoa chanjo ya kudhibiti msambao wa ugonjwa huo wakishirikiana na shirika la afya ulimwenguni WHO.
Mkurugenzi huyo vile vile alimesema zoezi hilo litaambatana na hamasa kwa wananchi kuhusu namna ya kujikinga na maambukizi zaidi.
“Kwa wakati huu Mombasa ndio inaongoza kwa idadi ya visa 139 kwa hivyo tuchuke tahadhari kuhakikisha kwamba tunazuia maambukizi, na tunafanya mpango pamoja na shirika la afya duniani WHO, hapa tutakuja na mpango wa chanjo na ikifika huo wakati tunaomba watu wajitokeze wapate chanjo ili wapate kinga”,alisema Daktari Amoth.
Wakati huo huo Amoth aliokeza kuwa uchunguzi wa vifo vya watu wanne walioaga dunia wiki chache zilizopita huko Migadini, eneo bunge la Changamwe kaunti ya Mombasa umebaini walifariki kutokana na magonjwa mengine na wala sio maambukizi ya ugonjwa wa MPOX kama ilivyodhaniwa na wakaazi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu.