News
Ofisi za Shule ya Wavulana ya Kinango zimeteketea

Baadhi ya ofisi za Shule ya Wavulana ya Kinango kaunti ya Kwale zimeteketea baada ya moto kuzuka katika shuleni hiyo usiku wa kuamkia siku ya Jumatano.
Mwalimu mkuu wa shule hiyo Siasa Mwafungo alieleza kwamba licha ya chanzo cha moto huo bado hakijabainika huenda baadhi ya wanafunzi waliotaka kwenda kwa likizo ya sikukuu ya Eid-Ul-Adha walihusika katika mkasa huo.
Mwafun go alisema kwamba moto huo uliweza kudhibitiwa japo kiasi cha mali ya thamani ya pesa imeteketea ikiwemo vitabu na vifaa vingine wanavyotumia walimu kufanya kazi zao.
“Bado tunachunguza chanzo cha moto huo lakini kiasi cha mali ya thamani ya shule imepotea kufuatia mkasa huu wa moto, maafisa wa polisi watatueleza zaidi baada ya uchunguzi kukamilika”, alisema Mwalimu mkuu.
Mwalimu huyo mkuu aliwaonya wanafunzi kwamba yeyote atakayepatikana kuhusika na mkasa huo basi hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake ili iwe funzo kwa wanafunzi wengine wenye utovu wa nidhamu.
“Wanafunzi tumewaonya kwamba iwapo tutabaini kwamba wamehusika katika mkasa huu basi sheria lazima itachukua mkondo wake”, alisema Mwafungo.
Wakati huo huo aliwataka wazazi wa shule hiyo kutoa shaka kwani usalama wa wanafunzi umeimarishwa huku maafisa wa upelelezi wa jinai nchini DCI katika eneo bunge la Kinango wakifanya jitihada za kubaini chanzo cha moto huo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Mawakili Kilifi waungana kushtumu mauaji ya Wakili Mbobu

Siku chache baada ya Wakili Kyalo Mbobu kuuawa kinyama kwa kupigwa risasi mara kadhaa akiwa kwenye gari lake barabara ya Lang’ata jijini Nairobi, mawakili mjini Kilifi kaunti ya Kilifi wameungana na mawakili wengine nchini siku ya Ijumaa Semtemba 12 mwaka huu kufanya matembezi ya amani, wakishutumu vikali mauaji hayo.
Wakiongozwa na Mwakilishi wao Sesil Mila, mawakili hao walilaani vikali mauaji ya wakili Mbobu wakiishutumu serikali kwa kutowajibikia swala la usalama wa wananchi wake.
Aidha waliitaka idara ya usalama kuhakikisha kuwa inafanikisha wajibu wake wa kuwalinda mawakili wakisisitiza haja ya haki kupatikana kwa familia ya mwendazake wakili Kyalo.

Mawakili wa Kilifi wakiongozwa na Sesil Mila, washtumu mauaji ya Wakili Kyalo Mbobu
Mawakili hao sasa waliitaka idara ya upelezi na asasi zote husika kuhakikisha kuwa uchunguzi wa kina unafanywa kubaini watuhumiwa wa mauaji hayo ili wachukuliwe hatua kali za kisheria haraka iwezekanavyo.
Taarifa ya Hamis Kombe
News
IEBC inaendelea kutambua vituo vya kusajili wapiga kura

Maafisa wa tume ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC wamesema wanaendelea na zoezi la kutambua sehemu za kuweka vituo vya kusajili wapiga kura hasa maeneo ya mashinani.
Afisa msimamizi wa tume ya IEBC eneo bunge la Ganze kaunti ya Kilifi, Mohammed Bahero Aboud alisema juhudi hizo ni kuhakikisha zoezi la usajili wapiga kura litakaloanza rasmi Septemba 29, mwaka huu linafaulu.
Akizungumza mjini Kilifi, Bahero alisema tume hiyo inatumia mbinu mpya ya kutambua vituo vya jadi vya usajili wapiga kura na kuweka vituo vipya kulingana na mapendekezo ya sheria.
Wakati huo huo alidokeza kwamba tume ya IEBC imekuwa ikihamashisha wakenya kutokubali kushawishiwa na wanasiasa na kujisajili katika maeneo yasiokuwa yao hasa msimu huu ambao zoezi hilo linakaribia kuanza.
Taarifa ya Joseph Jira