News
Ofisi za Shule ya Wavulana ya Kinango zimeteketea

Baadhi ya ofisi za Shule ya Wavulana ya Kinango kaunti ya Kwale zimeteketea baada ya moto kuzuka katika shuleni hiyo usiku wa kuamkia siku ya Jumatano.
Mwalimu mkuu wa shule hiyo Siasa Mwafungo alieleza kwamba licha ya chanzo cha moto huo bado hakijabainika huenda baadhi ya wanafunzi waliotaka kwenda kwa likizo ya sikukuu ya Eid-Ul-Adha walihusika katika mkasa huo.
Mwafun go alisema kwamba moto huo uliweza kudhibitiwa japo kiasi cha mali ya thamani ya pesa imeteketea ikiwemo vitabu na vifaa vingine wanavyotumia walimu kufanya kazi zao.
“Bado tunachunguza chanzo cha moto huo lakini kiasi cha mali ya thamani ya shule imepotea kufuatia mkasa huu wa moto, maafisa wa polisi watatueleza zaidi baada ya uchunguzi kukamilika”, alisema Mwalimu mkuu.
Mwalimu huyo mkuu aliwaonya wanafunzi kwamba yeyote atakayepatikana kuhusika na mkasa huo basi hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake ili iwe funzo kwa wanafunzi wengine wenye utovu wa nidhamu.
“Wanafunzi tumewaonya kwamba iwapo tutabaini kwamba wamehusika katika mkasa huu basi sheria lazima itachukua mkondo wake”, alisema Mwafungo.
Wakati huo huo aliwataka wazazi wa shule hiyo kutoa shaka kwani usalama wa wanafunzi umeimarishwa huku maafisa wa upelelezi wa jinai nchini DCI katika eneo bunge la Kinango wakifanya jitihada za kubaini chanzo cha moto huo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Joho, awahimiza wakenya kujisajili katika “Boma Yangu”

Waziri wa Madini na Uchumi wa raslimali za bahari Ali Hassan Joho, aliwahimiza wakenya kujisajili katika mpango wa “Boma Yangu” ili kunufaika na nyumba za bei nafuu zinazojengwa katika maeneo mbalimbali nchini.
Waziri Joho alipongeza mradi huo wa serikali, akisema unalenga kuwaondoa wakenya kutoka kwenye makaazi duni na kuwapatia makaazi bora yenye hadhi na mazingira salama ya kuishi.
Akizungumza katika kaunti ya Mombasa baada ya swala ya Eid-ul-Adha, Joho aliwahimiza wakaazi wa eneo la Pwani kuchukua hatua za haraka kujisajili ili wasikose fursa hiyo muhimu ya kuboresha maisha yao.
“Kuna huu mradi unaitwa Affordable Housing, huu mradi mmeona umefanywa mahali kwingi sana na sai usajili wa ule mradi ambao utafanyika pale VOK eneo bunge la Nyali, nyumba 1,976 zitajengwa na mambo mengine, nawasihi kwa heshima kubwa sana waingie kwa Boma Yangu wajisajili”, alisema Joho.
Kwa upande wake Kamishna wa kaunti ya Mombasa Mohamed Nur aliwahimiza vijana kujitokeza kwa wingi kutuma maombi ya nafasi za ajira katika mpango wa kazi mtaani kwa vijana.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
KHRC: Wasichana elfu moja ni wajawazito, Lamu

Takribani wasichana elfu moja kaunti ya Lamu wameripotiwa kupata mimba za utotoni kati ya mwaka wa 2024/25 huku visa vingi vikichangiwa na dhulma za kingono na ndoa za mapema.
Kulingana na Masharika ya kutetea haki za kibinadamu la MUHURI pamoja na lile la Kenya Human Rights Commission, KHRC serikali imeshindwa kuwakabili kisheria wahusika huku waathiriwa ambao ni wasichana wadogo wakiendelea kuhangaika.
Takwimu kutoka kwa kamati ya jinsia kaunti ya Lamu, iliwasilisha kwa kamati ya kitaifa inayoangazia masuala ya dhulma za jinsia kuwa kaunti hiyo ilinakili visa zaidi ya 700 vya mimba za utotoni mwaka wa 2024.
Takwimu hioz pia ziliweka wazi kwamba visa vingine zaidi ya 200 viliripotiwa kati ya mwezi Januari na Mei mwaka huu wa 2025.
Kulingana na ripoti kutoka kwa baraza la kitaifa la kudhibiti magonjwa NSDCC ilieonysha kwamba wasichana wanarika zaidi ya 600 nchini walipata mimba mwaka 2023.
Taarifa ya Janet Mumbi