News
Ofisi za Shule ya Wavulana ya Kinango zimeteketea

Baadhi ya ofisi za Shule ya Wavulana ya Kinango kaunti ya Kwale zimeteketea baada ya moto kuzuka katika shuleni hiyo usiku wa kuamkia siku ya Jumatano.
Mwalimu mkuu wa shule hiyo Siasa Mwafungo alieleza kwamba licha ya chanzo cha moto huo bado hakijabainika huenda baadhi ya wanafunzi waliotaka kwenda kwa likizo ya sikukuu ya Eid-Ul-Adha walihusika katika mkasa huo.
Mwafun go alisema kwamba moto huo uliweza kudhibitiwa japo kiasi cha mali ya thamani ya pesa imeteketea ikiwemo vitabu na vifaa vingine wanavyotumia walimu kufanya kazi zao.
“Bado tunachunguza chanzo cha moto huo lakini kiasi cha mali ya thamani ya shule imepotea kufuatia mkasa huu wa moto, maafisa wa polisi watatueleza zaidi baada ya uchunguzi kukamilika”, alisema Mwalimu mkuu.
Mwalimu huyo mkuu aliwaonya wanafunzi kwamba yeyote atakayepatikana kuhusika na mkasa huo basi hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake ili iwe funzo kwa wanafunzi wengine wenye utovu wa nidhamu.
“Wanafunzi tumewaonya kwamba iwapo tutabaini kwamba wamehusika katika mkasa huu basi sheria lazima itachukua mkondo wake”, alisema Mwafungo.
Wakati huo huo aliwataka wazazi wa shule hiyo kutoa shaka kwani usalama wa wanafunzi umeimarishwa huku maafisa wa upelelezi wa jinai nchini DCI katika eneo bunge la Kinango wakifanya jitihada za kubaini chanzo cha moto huo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Waislam Waadhimisha Sikukuu ya Eid-Ul-Adha

Waislam kote duniani wanaadhimisha Sikukuu ya Eid-Ul-Adha, inayojulikana pia kama sikukuu ya sadaka, ambayo huadhimishwa katika mwezi wa Dhul Hijjah katika kalenda ya Kiislam.
Sikukuu hii ni moja ya nyakati tukufu zaidi katika Uislamu, ikiashiria kilele cha Hijja na kuadhimisha utiifu wa Nabii Ibrahimu aliyekuwa tayari kumtoa mwanawe Ismail kama sadaka kwa amri ya Mwenyezi Mungu.
Siku kumi za mwanzo za Dhul Hijjah zinahesabiwa kuwa siku takatifu zaidi, zikiwa zimejawa na ibada, kufunga, na dua.
Mwaka huu, zaidi ya mahujaji milioni 2 wanahudhuria Hijja katika mji mtakatifu wa Makkah nchini Saudi Arabia, Kenya ikipeleka wahujaji 4,500, kuhijji, ikiwa ni mojawapo ya idadi kubwa zaidi katika historia ya hivi karibuni.
Viongozi mbalimbali wa dini ya kiislam waliwahimiza waumini wa dini ya kiislam kuhakikisha wanasheherekea sikukuu ya Eid-ul-Adha pamoja na wale wasiojiweza kwa kuchinja mifugo na kugawa na watu wengine wasiobahati katika jamii.
Taarifa ya Lolani Kalu
News
Familia zilizoathirika na ujenzi wa barabara kuu ya Kilifi-Mtwapa zafidiwa.

Idara ya usalama kaunti ya Kilifi imesema serikali inaendelea na zoezi la kufidia familia zilizoathirika na ujenzi wa barabara kuu ya Kilifi kuelekea Mtwapa.
Kamisha wa kaunti ya Kilifi Josephat Biwot alidokeza kuwa kwa sasa maafisa wa shirika la Kenya power wanaendelea kuondoa nyaya za stima ili kutoa nafasi kwa mkandarasi kuendelea na shughuli za ujenzi.
Vile vile Biwot alisema ujenzi daraja mbili kubwa kaunti ya Kilifi unaendelea pamoja na ujenzi wa barabara ya Sabaki Sosoni kueleke Baricho hadi Baolala.
“Ujenzi wa barabara kuu ya Kilifi kuelekea Mtwapa unaendelea vyema, tunachokifanya sasa ni kufidia walioathirika, pia kenya power inaondoa nyaya kupisha mwanakandarasi kuendelea na ujenzi, vile vile ujenzi wa daraja mbili kuu kilifi unaendelea hasa ya Galana Kulalu na Baricho”, alisema Biwot.
Vile vile Kamishna huyo alidokeza kuwa serikali inaendelea na ujenzi wa miradi mbali mbali inayoambatanishwa na sekta ya uchumi wa bahari.
“Upande wa uchumi wa bahari miradi mingi inaendelea mfano ujenzi wa eneo la kuegesha boti kilifi, pia tunajenga makao makuu ya eneo la samaki ya kaunti, tuko na soko la samaki Malindi, tuko na eneo la kuhifadhi samaki la kichwa cha kati ambalo limekamilika na liligharimu shilingi milioni 250”, aliongeza Biwot.
Wakati huo huo wadau wa sekta ya Uvuvi eneo la Ngomeni wakiongozwa na Mwenyekiti wa Ngomeni BMU Said Athman aliitaka serikali kufuatilia kwa kina fedha zinazotolewa na serikali kudaidi miradi ya wavuvi.
“Tunapewa pesa ya makundi kwa mfano shilingi milioni tatu, ile pesa mpaka ikifikia jamii imeliwa, kwa mfano unapewa boti lakini halina vifaa sababu ile pesa imeliwa juu na maofisa mpaka ikifika nyanjani imeisha”, alisema Athman.
Mwenyekiti wa Ngomeni BMU Said Athman akizungumza na wanahabari Kilifi.
Taarifa ya Joseph Jira.