News
ODM Na PAA, Wafanya mikutano tofauti kuhusu bunge la Kilifi

Mikutano miwili muhimu ya faragha imefanyika Jumatatu Juni 2 2025, kujadilia usimamizi wa vyama vya ODM na PAA ndani na nje ya Bunge la Kaunti ya Kilifi.
Taarifa za kuamika zasema, mikutano hiyo miwili ilikusudia kujadili matukio ya hivi majuzi katika Bunge la Kaunti ya Kilifi na usimamizi wake.
Mazungumzo ya Chama cha ODM yaliofanyika mjini Kilifi na kuhudhuriwa na viongozi wote waliochaguliwa, yalijikita katika tetesi za kumtimua Spika wa Bunge Teddy Mwambire, huku kukiwa na mpasuko baina ya wafuasi wa Spika Teddy Mwambire na kwa upande mwengine, wandani wa Gavana Gideon Mung’aro.
Tofauti kubwa za uongozi wa chama hicho cha ODM zilizuka tangu mchakato wa uchaguzi wa mashinani uliotibuka mwaka uliopita na uhasama huo sasa kuelekezwa ndani ya bunge la Kaunti kutaka kumuondoa Spika mamlakani kupitia kura ya kutokuwa na Imani naye ikidaiwa anahujumu serikali ya Gavana Mung’aro.
Pia mkutano huo ulijadili uwezo Mwakilishi Wadi wa Watamu Ibrahim Matumbo wa kuendelea kuwa kiongozi wa wengi Bungeni.
Kuna habari ambazo hazijathibitishwa kwamba huenda chama cha ODM kinataka kumuondoa Ibrahim Matumbo na wadhfa wake kuchukuliwa na Mwakilishi Wadi ya Ganda Oscar Wanje.
Kwa upande mwengine katika mkutano wa Chama cha PAA uliofanyika katika makao makuu ya chama eneo la Nyali kaunti ya Mombasa, yalijikita katika masuala ya usimamizi ndani ya bunge hilo na kumlenga zaidi kiongozi wa walio wachache katika bunge hilo la kaunti Tom Chengo.
Chengo ambaye pia ni Mwakilishi Wadi wa Tezo- kaunti ya Kilifi, anashtumiwa kwa kuhujumu upinzani ndani ya bunge hilo kutokana na usuhuba wake na Gavana Gideon Mung’aro.
Akizungumza na Cocofm kwa njia ya simu, Katibu mkuu wa Chama cha PAA, amnaye pia ni mbunge wa Ganze Kenneth Kazungu, alikiri kufanyika kwa mkutano huo, siku ya Jumatatu Juni 2, na kwamba mkutano huo ulikuwa kuweka sawa usimamizi na shughuli za chama ndani na nje ya bunge la kaunti.
Katika siku za hivi majuzi bunge hilo limeshuhudiwa mpasuko mkubwa wa kiutawala na kupelekea kutatizwa kwa vikao vya bunge vya kujadili masuala nyeti yanayogusia bejeti na usimamizi wa fedha na utekelezwaji wa miradi katika Wizara ya Afya.
News
Ujenzi wa barabara ya Kibaoni-Ganze-Bamba umeng’oa nanga

Baada ya wakaazi wa eneo bunge la Kilifi Kaskazini na Ganze kulalamikia ubovu wa barabara ya Kibaoni-Ganze hadi Bamba na kuangziwa na wanahabari, hali sasa ni tofauti.
Ujenzi wa barabara hiyo iliyoshudia utata na maandamano, sasa unaendelea huku mkandarasi akiwa katika hatua kupiga msasa barabara na kujenga mabomba na sehemu za kupitisha maji hasa kunaponyesha.
Justine Kandie ni muangalizi wa ujenzi wa barabara hiyo, alisema shughuli hiyo imegawanywa mara mbili, na kwa sasa wameanza ujenzi wa barabara hiyo kutoka eneo la Kibaoni mjini Kilifi kuelekea Ganze.
Kandie alisema mpango huo ulianza mwaka 2021 kutoka eneo bunge la Ganze kuelekea kibaoni japo ulisitishwa wakati huo na sasa wameanza tena kujenga umbali wa kilomita tano.
“Katika awamu ya kwanza kwa mwaka wa 2021 tulianza barabara kutoka Ganze tulikuwa tunafanya kilomita tano, kwa mda wa miaka miwili barabara ikasimama kidogo, baadaye kurudi kwa huu mwaka wa 2025 ndio tumepewa kile kiwango tuanze kutoka kibaoni kuelekea Ganze, katika hii awamu ya pili tunafanya kilomita tano ila kwa sababu barabara ni mbovu tumeamua kuanzia huku kwa Kimanje tukielekea Kibaoni ili barabara yetu iwe sawa wakati tunaposafirisha vifaa vya ujenzi”,alisema Kandie.
Baadhi ya mafundi wakiendelea na ujenzi wa barabara ya kuelekea Ganze
Picha:(Joseph Jira)
Kandie pia alisema mda wa miaka miwili aliopewa mkandarasi kukamilisha ujenzi huo wa barabara utategemea na mgao wa pesa zitatakaotolewa kufanikisha mradi huo.
“Ule mda wa kukamilisha barabara huwa inategemea uwezo wa mwanakandarasi kama ako na fedha za kutosha, itamsaidia kukamilisha kwa mda unaofaa, kwa sababu hii barabara yetu walikuwa wametupa kama miaka miwili ila saa hii mda umesonga”, aliongeza Kandie.
Wakaazi pamoja na wahudumu wa uchukuzi wa umma wanaotumia barabara hiyo wameeleza matumaini ya kuimarika kwa sekta ya uchukuzi sawa na uchumi mara tu ujenzi utakapokamilika.
Itakumbukwa kwamba barabara hiyo ilileta utata na kusababisha wakaazi kuandamana na kuifunga sawa na kutatiza shughuli za usafiri kwa mda.
“Hapo kwa usafiri na biashara huenda kukabadilika kwa sababu wengi pia wanakataa huku kwa sababu yah ii barabara vile ni mbovu hasa kazi zinakuwa ziko chini kwa sababu ya vumbi”,alisema Jeremiah Mwaringa
Tinga tinga za ujenzi wa barabara ya kuelekea Ganze.
Picha:(Joseph Jira)
Mvutano huo pia ulishuhudiwa baina ya mbunge wa Ganze Kenneth Kazungu Tungule na mbunge wa Kilifi Kaskazini Owen Baya kuhusu ujenzi wa barabara unakofaa kuanza kutekelezwa.
Hata hivyo muangalizi wa mradi huu aelieleza matumaini yake kuwa mvutano huo wa wanasiasa hautaathiri utendakazi wao huku akishinikiza wahudumu wa barabara hiyo kuwa na uvumilivu wakati wanapoendelea na ujenzi huo.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Kongamano la mabadiliko ya hali ya anga lafanyika Mombasa

Mratibu wa Kongamano la kimataifa linaloangazia masuala ya mabadiliko ya hali ya anga, INTER- GOVERNMEMTAL PANEL ON CLIMATE CHANGE, Patricia Nying’uro amesema jamii inasalia kuwa kiungo muhimu katika harakati za kuangazia mfumo wa mabadiliko ya hali ya hewa.
Kufuatia hilo, Nying’uro alitoa wito kwa wadau wa mazingira kuwekeza zaidi na kuhakikisha kila mmoja anashiriki ipasavyo katika kudhibiti mabadiliko hayo.
Nying’uro alisema Kongamano ambalo linaendelea katika kaunti ya Mombasa, linaangazia masuala ya mabadiliko ya hali ya anga na limewekeza kutambuliwa na jamii katika mikakati hiyo.
Akizungumza katika eneo la Shanzu wakati wa majadiliano hayo, Nying’uro alisema jumla ya mataifa 56 kati ya mataifa 195 yanayoshiriki kwenye mchakato wa kuweka mipango, sera na mikakati ya kudhibiti mabadiliko ya hali ya hewa yanakongamana eneo la Shanzu ili kuanisha ripoti ambayo itatoa muongozo rasmi wa kuangazia makali ya mabadiliko ya hali ya hewa.
Wakati huohuo, Nying’uro alisema pia kongamano hilo la kimataifa lina umuhimu mkubwa kwa taifa hili kwani Kenya itahusishwa moja kwa moja katika kupangilia sera za kimataifa za kudhibiti athari ya mabadiliko ya hali ya anga.
Taarifa ya Janet Shume