News
ODM Na PAA, Wafanya mikutano tofauti kuhusu bunge la Kilifi

Mikutano miwili muhimu ya faragha imefanyika Jumatatu Juni 2 2025, kujadilia usimamizi wa vyama vya ODM na PAA ndani na nje ya Bunge la Kaunti ya Kilifi.
Taarifa za kuamika zasema, mikutano hiyo miwili ilikusudia kujadili matukio ya hivi majuzi katika Bunge la Kaunti ya Kilifi na usimamizi wake.
Mazungumzo ya Chama cha ODM yaliofanyika mjini Kilifi na kuhudhuriwa na viongozi wote waliochaguliwa, yalijikita katika tetesi za kumtimua Spika wa Bunge Teddy Mwambire, huku kukiwa na mpasuko baina ya wafuasi wa Spika Teddy Mwambire na kwa upande mwengine, wandani wa Gavana Gideon Mung’aro.
Tofauti kubwa za uongozi wa chama hicho cha ODM zilizuka tangu mchakato wa uchaguzi wa mashinani uliotibuka mwaka uliopita na uhasama huo sasa kuelekezwa ndani ya bunge la Kaunti kutaka kumuondoa Spika mamlakani kupitia kura ya kutokuwa na Imani naye ikidaiwa anahujumu serikali ya Gavana Mung’aro.
Pia mkutano huo ulijadili uwezo Mwakilishi Wadi wa Watamu Ibrahim Matumbo wa kuendelea kuwa kiongozi wa wengi Bungeni.
Kuna habari ambazo hazijathibitishwa kwamba huenda chama cha ODM kinataka kumuondoa Ibrahim Matumbo na wadhfa wake kuchukuliwa na Mwakilishi Wadi ya Ganda Oscar Wanje.
Kwa upande mwengine katika mkutano wa Chama cha PAA uliofanyika katika makao makuu ya chama eneo la Nyali kaunti ya Mombasa, yalijikita katika masuala ya usimamizi ndani ya bunge hilo na kumlenga zaidi kiongozi wa walio wachache katika bunge hilo la kaunti Tom Chengo.
Chengo ambaye pia ni Mwakilishi Wadi wa Tezo- kaunti ya Kilifi, anashtumiwa kwa kuhujumu upinzani ndani ya bunge hilo kutokana na usuhuba wake na Gavana Gideon Mung’aro.
Akizungumza na Cocofm kwa njia ya simu, Katibu mkuu wa Chama cha PAA, amnaye pia ni mbunge wa Ganze Kenneth Kazungu, alikiri kufanyika kwa mkutano huo, siku ya Jumatatu Juni 2, na kwamba mkutano huo ulikuwa kuweka sawa usimamizi na shughuli za chama ndani na nje ya bunge la kaunti.
Katika siku za hivi majuzi bunge hilo limeshuhudiwa mpasuko mkubwa wa kiutawala na kupelekea kutatizwa kwa vikao vya bunge vya kujadili masuala nyeti yanayogusia bejeti na usimamizi wa fedha na utekelezwaji wa miradi katika Wizara ya Afya.
News
Wahudumu wa afya Lamu watishia kuishtaki serikali ya kaunti hiyo

Wahudumu wa Afya kaunti ya Lamu wametishia kuelekea Mahakamani kuishtaki serikali ya kaunti hiyo kwa kukaidi kutekeleza matakwa yao.
Wahudumu hao waliishtumu serikali ya kaunti ya Lamu kwa kupuuza matakwa yao na badala yake kutumia vitisho ili kuwashurutisha kurejea kazini.
Kulingana na viongozi wa wahudumu hao, licha ya mgomo wao kuendelea kwa zaidi ya wiki mbili serikali ya kaunti hiyo imekataa kata kuandaa vikao vya kusuluhisha malalamishi yao.
Baadhi ya changamoto wanazolalamikia ni pamoja na kufanya kazi kwa zaidi ya miaka 10 bila ya kupandishwa vyeo, kupuuzwa kwa mkataba wa makubaliano ya nyongeza ya mishahara, kunyimwa kwa mishahara kwa baadhi ya wahudumu hao miongoni mwa matakwa mengine.
“Mkiendelea kutufinyilia itabidi tufuate njia ya sheria kwa sababu tunajua tunalilia haki yetu, haiwezekani serikali ya kaunti inashindwa kutupandisha vyeo ilhali tumefanya kazi kwa miaka 15 sasa, hatuwezi kuendelea kufanya kazi katika mazingira duni na pia mkataba wa makubaliano kuhusu nyongeza ya mishahara sharti itekelezwe” walisisitiza viongozi hao.
Wakati uo huo serikali ya kaunti ya Lamu imejibu malimishi yao kupitia barua na kutangaza kuwa mgomu huo ni kinyume cha seria na kuwataka wahudumu hao kurejea kazini mara moja.
Taarifa ya Elizabeth Mwende
News
Rais Ruto atuma KDF kusimamia ujenzi wa hospitali nchini

Rais William Ruto ametuma jeshi la KDF kusimamia ujenzi wa vituo vya afya zaidi ya 75 kote nchini katika juhudi za kuhakikisha ujenzi unakamilika kwa haraka.
Akizungumza katika kaunti ya Narok wakati wa uzinduzi wa hospitali ya Sogoo Level 4, waziri wa ulinzi Patrick Mariru alifichua kuwa ujenzi wa hospitali hiyo yenye mamlaka kamili itakamilika baada ya mda wa miezi 11.
Ujenzi wa hospitali ya Sogoo Level 4 ulivutia rais Ruto alipozuru eneo hilo mwezi mei mwaka 2025, jambo lililomfanya kuagiza KDF kuipandisha hadhi.
Mariru hata hivyo alishikilia kuwa wafanyikazi wote wasio na ujuzi watatolewa kutoka kwa jamii.
“Jeshi litamsimamia mkandarasi. Hilo liwe wazi, kazi yote itafanywa na vijana wa Sogoo. Tutaweka maafisa wawili na kila jioni watanipa ripoti ya maendeleo,” alisema Mariru.
“Tuna zaidi ya miradi 75 tunayosimamia na sio kwamba tunabadilisha wakala wa serikali tunataka tu kushirikiana na ofisi tofauti miongoni mwao wizara za afya na michezo.”
Taarifa ya Joseph Jira