News
Mbinu mpya ya kuwaua wakongwe Kilifi na Kwale yaibua hofu

Mashirika ya kutetea haki za binadamu eneo la pwani yameeleza wasi wasi wao kuhusu madai ya kuibuka kwa mbinu mpya ya mauaji ya wazee katika kaunti ya Kilifi na Kwale kutokana na mizozo ya umiliki wa ardhi.
Kwa mujibu wa afisa wa shirika la Haki Yetu John Obonyo, kwa sasa wahusika wanatumia mbinu ya kuteketeza moto nyumba za wazee sawa na kuwanyonga ili kuonekana wamejitoa uhai ili kupoteza ushahidi.
Obonyo hata hivyo alibaini kwamba watu hulipwa kati ya shilingi elfu tatu hadi shilingi elfu nne, ili kutekeleza mauaji hayo.
“Mauaji ya wazee yamezidi sana, yamezidi kwa misingi kwamba mbinu ambayo wazee wanapoteza uhai imebadilika, njia moja ni kuwa wanachomwa kwa nyumba kusudi wapoteze ushahidi, njia ya pili ni kuwa wananyongwa, na mtu ambaye amejinyonga nitofauti na yule ambaye amenyongwa, kwa hivyo ni njia tu yakupoteza ushahidi, lakini cha kusikitisha zaidi ni kuwa imekuwa na bei, sehemu za kilifi ukiwa na elfu 30 unatoa uhai”,alibaini Obonyo.
Hata hivyo Obonyo alipendekeza wazazi kuandika wosia kwa familia zao wakati wa uhai wao ili kuepuka mizozo kama hiyo kushuhudiwa.
Kaunti za Kilifi na Kwale zimekuwa zikiongoza kwa visa hivyo ambapo wakongwe wamekuwa wakiuawa kwa tuhuma za ushirikina, japo ilibainika kuwa mauaji hayo yanachangiwa na wanafamilia kutaka kurithi mali.
Taarifa ya Mwanahabari wetu.
News
Mahakama ya Kilifi imetoa hukumu kwa wanaume 6 wanaokabiliwa na mashtaka ya unajisi

Mahakama ya Kilifi imetoa hukumu kwa wanaume 6 wanaokabiliwa na mashtaka ya unajisi.
Hakimu wa Mahakama hiyo Ivy Wasike alimhukumu Lucky Munga na Hassan Daniel kifungo cha miaka 30 gerezani baada ya Mahakama kubaini kwamba walihusika kwa kuwatendea unyama watoto wa umri wa miaka 13 na 15.
Safari Karisa Lewa alihukumiwa kifungo cha miaka 15 gerezani kwa kumnajisi mtoto wake mwenyewe wa umri wa miaka 14 huku Eric Ruwa na Lucky Katana Kenga wakihukumiwa kifungo cha miaka 6 gerezani kwa kosa sawa na hilo.
Hata hivyo Mahakama hiyo ilimhukumu kifungo cha miaka 3 Kithi Kombe kutokana na kesi hiyo kwa mtoto wa miaka 15, japo baadaye Mahakama ikabaini kwamba mshukiwa sio baba halali wa mtoto aliyezaliwa baada ya Kithi kumnajisi mtoto huyo.
Akizungumza wakati wa vikao vya Mahakama baada ya kutoa hukumu hizo, Hakimu Wasike alisema Mahakama umezingatia ushahidi uliyotolewa Mahakamani huku akiwarai wananchi kujitenga na visawishi vibaya ili kuepuka mkono wa sheria.
Hakimu Wasike alihoji kwamba washtakiwa wa haki ya kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa Mahakama lakini kwa kuzingatia taratibu zote za Mahakama na sheria.
Taarifa ya Teclar Yeri
News
Thoya: Serikali kuu iongeze mgao wa fedha kwa sekta ya Afya

Naibu gavana wa kaunti ya Mombasa Francis Thoya ametoa changamoto kwa serikali kuu kuongeza mgao wa fedha ili kufanikisha utaoji wa huduma za afya.
Akizungumza katika kaunti hiyo, Thoya alisema kuwa huduma nyingi za afya katika kaunti hiyo ya Mombasa zinakabiliwa na changamoto ya raslimali ndogo hali ambayo inakwamisha juhudi za kuwahudumia wananchi ipasavyo.
Thoya pia alitaka serikali kuhakikisha inaharakisha kuajiri wahudumu zaidi wa afya ili wenyeji wa Mombasa waweze kupata huduma bora za matibabu bila changamoto zozote.
Aidha, Thoya alisema kwamba hali ya uhaba wa wahudumu wa afya ni changamoto kuu ambayo inazuia utoaji wa huduma bora za matibabu hali inayowafanya wale wachache waliopo kufanya kazi katika mazingira magumu.
Taarifa ya Janet Mumbi