News
Mwili wa marehemu Samuel Kirao wafukuliwa

Hatimaye familia ya Marehemu Samuel Kirao Charo imepata haki ya kuuzika mwili wa mpendwa wao baada ya mzozo uliokuwepo hapo awali na kupelekea marehemu kuzikwa kwa mujibu wa dini ya Kiislamu.
Hii ni baada ya familia hiyo kushinda kesi kwenye Mahakama ya Malindi wakati ambapo Mahakama ya Kadhi ilikuwa imeidhinisha jamii ya Waislamu kuuzika mwili huo kwa msingi kwamba Marehemu alikuwa muislam hata wakati wa kufa kwake.
Jaji Mugure Thande wa Mahakama ya Malindi alitoa uamuzi wa kufukuliwa kwa mwili huo na kisha ukabidhiwe familia yake ili uzikwe upya baada ya familia kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa Mahakama ya Kadhi.
Eunice Kirao ambaye ni mama mzazi wa marehemu alisema marehemu alisilimishwa akiwa na akili punguani, akieleza kusikitishwa na jamii hiyo ya waislamu kutowapatia nafasi na badala yake ikashurutisha ibada ya mazishi kwa nguvu.
Kwa upande wake babake marehemu Stephen Kirao alisema wamepitia gharama nyingi za kuandaa mazishi kabla ya jamii ya waislamu kuuzika mwili wa marehemu, akisisitiza kuwa ni sharti gharama hizo zilipwe.

Familia ya Marehemu Samuel Kirao Charo katika makaburi ya Takaungu
Naye Kalume Charo ambaye ni kakake mkubwa marehemu alieleza kwamba hali haijakuwa nzuri muda wote huo kwani wamekuwa wakipitia kejeli na unyanyapaa katika eneo wanaloishi mbali na wazazi wao kuathirika kiafya.
Ikumbukwe kwamba marehemu Samuel aliuawa na umma baada ya kumuua kwa kumdunga kisu Ustadh mmoja eneo la Takaungu na kisha kuula utumbo wake.
Taarifa ya Hamis Kombe
News
Mabadiliko ya tabianchi yatajwa kuchangia mapato duni ya samaki, Lamu

Wadau katika sekta ya mazingira kaunti ya Lamu wanasema mabadiliko ya hali ya anga yanayoshuhudiwa sawa na ujenzi wa bandari ya Lamu kumechangia mapato ya samaki kupungua katika bahari hindi.
Mahmoud Yusuf ambaye ni mwanazingira alisema zana za kizamani wanazotumia wavuvi kuvua samaki pia zinachangia mapato duni ya samaki.
Yusuf alisema tangu ujenzi huo wa bandari uanze, maji ya bahari chini yamekuwa na matope kutokana na kuchimbwa na kufukuliwa kwa bahari, hali iliyochangia samaki kutorokea bahari kuu.
Mwanamazingira huyo aliitaka serikali kuwapa wavuvi vifaa vya kisasa vya uvuvi sawa na meli za uvuvi zitakazowawezesha kufika maji makuu, baada ya bandari ya ndani kuharibika.
Taarifa ya Joseph Jira.
News
Gachagua atangaza azma ya kuwania urais 2027

Kinara wa chama cha DCP Rigathi Gachagua ametangaza nia ya kuwania wadhfa wa urais mwaka 2027 akilenga kumg’oa rais William Ruto mamlakani.
Gachagua amekuwa akifanya ziara katika eneo la mlima kenya pamoja na viongozi wa chama chake akitumia mikutano ya barabarani kutangaza azma yake ya kuwania urais.
Kulingana na Gachagua serikali ya sasa inatumia mikutano ya ikulu kuendeleza vitendo vya ufisadi, na ameahidi kuwa akichaguliwa atakomesha matumizi mabaya ya fedha za umma.
Katika ziara hiyo viongozi wa chama chake walieza kuwa Gachagua ndiye mgombea anayefaa kupeperusha bendera ya upinzani, wakidai eneo la mlima kenya limejiondoa katika uungwaji mkono wa serikali ya sasa.
Taarifa ya Joseph Jira.