News
Mwili wa marehemu Samuel Kirao wafukuliwa

Hatimaye familia ya Marehemu Samuel Kirao Charo imepata haki ya kuuzika mwili wa mpendwa wao baada ya mzozo uliokuwepo hapo awali na kupelekea marehemu kuzikwa kwa mujibu wa dini ya Kiislamu.
Hii ni baada ya familia hiyo kushinda kesi kwenye Mahakama ya Malindi wakati ambapo Mahakama ya Kadhi ilikuwa imeidhinisha jamii ya Waislamu kuuzika mwili huo kwa msingi kwamba Marehemu alikuwa muislam hata wakati wa kufa kwake.
Jaji Mugure Thande wa Mahakama ya Malindi alitoa uamuzi wa kufukuliwa kwa mwili huo na kisha ukabidhiwe familia yake ili uzikwe upya baada ya familia kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa Mahakama ya Kadhi.
Eunice Kirao ambaye ni mama mzazi wa marehemu alisema marehemu alisilimishwa akiwa na akili punguani, akieleza kusikitishwa na jamii hiyo ya waislamu kutowapatia nafasi na badala yake ikashurutisha ibada ya mazishi kwa nguvu.
Kwa upande wake babake marehemu Stephen Kirao alisema wamepitia gharama nyingi za kuandaa mazishi kabla ya jamii ya waislamu kuuzika mwili wa marehemu, akisisitiza kuwa ni sharti gharama hizo zilipwe.

Familia ya Marehemu Samuel Kirao Charo katika makaburi ya Takaungu
Naye Kalume Charo ambaye ni kakake mkubwa marehemu alieleza kwamba hali haijakuwa nzuri muda wote huo kwani wamekuwa wakipitia kejeli na unyanyapaa katika eneo wanaloishi mbali na wazazi wao kuathirika kiafya.
Ikumbukwe kwamba marehemu Samuel aliuawa na umma baada ya kumuua kwa kumdunga kisu Ustadh mmoja eneo la Takaungu na kisha kuula utumbo wake.
Taarifa ya Hamis Kombe
News
Mahakama ya Malindi yawaachilia washukiwa 3 wa kesi ya Kwa Binzaro

Mahakama Kuu ya Malindi imewaachilia washukiwa watatu wanaohusishwa na kesi ya mauaji ya halaki ya watu katika kijiji cha Kwa Binzaro eneo bunge la Magarini kaunti ya Kilifi.
Hakimu wa Mahakama hiyo Joy Wesonga aliagiza kuachiliwa huru kwa Safari Kenga Nzai, Gona Charo Kalama na Kahindi Kazungu Garama wote wakiwa wakaazi wa kijiji hicho cha Kwa Binzaro.
Watatu hao walikuwa wamekamatwa baada ya kudaiwa kuuza shamba la ekari tano kwa mshukuwa mkuu wa mauaji ya watu katika kijiji cha Kwa Binzaro Sherleen Temba Anido.
Hakimu Wesonga aliwaagiza washukiwa hao kuhakikisha wanasalimisha nakala za vitambulisha vyao vya kitaifa kwa idara husika, kuripoti kwa Naibu Chifu wa eneo hilo mara mbili kwa wiki pamoja na kujisalimisha kwa maafisa wa upelelezi wa kesi hiyo mara moja kila baada ya wiki mbili.

Miili iliyofukuliwa katika kijiji cha Kwa Binzaro
Wakati huo huo upande wa mashtaka ukiongozwa na Naibu mkurugenzi wa mashtaka ya umma Jamie Yamina, uliomba kuwasilisha watu wengine wanne Mahakamani ikiwemo Jairus Otieno na mkewe Lilian Akinyi, Kahonzi Katana Karisa na Loise Zawadi waliojionda kama washukiwa na kugeuka kuwa mashahidi wa serikali.
Upande wa mashtaka pia uliaka kupewa siku 60 zaidi kuendelea kuzuiliwa kwa washukiwa wakuu Sherleen Temba Anido, James Kahindi Kazungu, Thomas Mukunwe na Kahidi Kazungu Garama katika kituo cha polisi cha Ngerenya, Kilifi, Watamu na Kijipwa ili kukamilisha uchunguzi wao kwani wanne hao wanakabiliwa na mashtaka ya itikadi kali, ugaidi, kujihusisha na uhalifu na kupanga mauaji.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Chrispus aomba msahama bunge la kaunti ya Taita Taveta

Mwakilishi wadi ya Bomani mjini Taveta kaunti ya Taita Taveta Chrispus Tondoo ameliomba bunge la kaunti hiyo msamaha kutokana na matamshi aliyoyatoa hapo awali akikashifu bunge hilo kwa madai ya kushamiri kwa visa vya ufisadi na utepetevu.
Tondoo akiomba msamaha katika bunge hilo alisema alitambua athari zilizosababishwa na matamshi hayo kwa wenyeji wa kaunti hiyo na bunge hilo, hali ambayo imemfanya kuchukua hatua hiyo ya kuomba msamaha.
Aidha Tondoo aliahidi kuliheshimu bunge hilo kwa mujibu wa kanuni na Sheria za bunge la kaunti ya Taita Taveta.
‘’Naomba msamaha kutokana na matamshi ambayo niliyatoa tarehe 2 na tarehe 3 mwezi wa Juni mwaka huu wa 2025 kwani hayakuwa yenye heshima kwa wenyeji wa Taita Taveta na bunge la kaunti’’, alisema Tondoo.
Tondoo alikuwa Mwakikishi wa wadi wa pili kuomba msamaha baada ya Mwakilishi wa wadi ya Kaloleni mjini Voi Ahmed Azari kuchukua hatua hiyo mwezi mmoja uliyopita.
Haya yalijiri baada ya kaimu spika wa bunge hilo Anselim Mwadime kuapa kuwachulia hatua za kisheria wanachama wanne wa bunge hilo, wawili wakiwa ni Tondoo na Azari ambayo tayari wameomba msamaha huku wawili wakiwa wamesalia bila kuomba msamaha.
Taarifa ya Janet Mumbi