News
Mbunge wa Kilifi kaszkazini Owen Baya alaumiwa na wanaharakati.

Wanaharakati wa kupambana na utumizi wa dawa za kulevya kanda ya pwani wamemkosoa mbunge wa Kilifi Kaskazini Owen Baya kutokana na hatua ya kuondoa hoja bungeni ya kupinga biashara ya zao la Mugoka.
Wakiongozwa na Famau Mohammed Famau, wanaharakati hao walisema uraibu wa mugoka umeendelea kuathiri maisha ya vijana wengi pwani na walikuwa na matumaini na mbunge huyo kukomboa maisha ya vijana kupitia hoja hiyo.
Famau alimshauri Baya kutowasilisha barua rasmi ya kuhakiki kuondoa hoja hiyo bungeni, ila kuendelea na harakati za kupambana na uraibu wa mugoka na kukomboa maisha ya vijana wa pwani.
“Mheshimiwa Baya alipochukuwa mswada huu kuupeleka bungeni sisi tulifurahi sana na kumpongeza, na hivi sasa kuuondosha bungeni tumekasirika na amefanya jambo la aibu ambalo halingefaa kufanywa na kiongozi kama yeye”, alisema Famau.
Kwa upande wake afisa mratibu mipango katika shirika la Kenya Muslim Youth alliance Asili Randani, aliitaka serikali kuu kuhusisha vijana katika miradi inayoendelea ili kuwaepusha na uhaba wa ajira unaoshuhudiwa miongoni mwao.
“Hapa eneo bunge la Kilifi kaskazini kunajanga kubwa la matumizi ya dawa za kulevya, miradi hii ingehusisha jamii moja kwa moja vijana wetu wasinge kuwa katika swala lile, vijana wakula mugoka wengi wao wamepoteza mwelekeo na wamekuwa wazembe”, alisema Randani.
Afisa mratibu mipango katika shirika la Kenya Muslim Youth alliance Asili Randani akizungumza na wanahabari Kilifi
Itakumbukwa mapema mwaka jana wa 2024 baadhi ya magavana eneo la pwani walipiga marufuku biashara ya zao la mugoka japo vita hivyo havikufaulu.
Taarifa ya Joseph Jira.
News
Godhana, awataka wakaazi kutoingiza siasa miradi ya maendeleo

Gavana wa kaunti ya Tana River Dhadho Godhana amewataka wenyeji wa kaunti hiyo kujiepusha na wanasiasa ambao wanaingiza siasa kwenye masuala ya maendeleo.
Godhana alisema hilo limechangia kaunti ya Tana River kusalia nyuma kimaendeleo hali ambayo itasababisha miradi mingi kuzidi kukwama.
Godhana alisema ni lazima viongozi na wenyeji wa kaunti ya Tana River washirikiane na uongozi wa kaunti ili kuafikia utekelezaji wa miradi ya maendeleo.
Wakati huo huo Godhana aliesema mradi wa Village Cluster ambao umekuwa ukipingwa ndio utakaosaidia kudhibiti changamoto ambazo zinaikumba kaunti ya Tana River.
Naye Mahat Ali Loka ambaye ni Naibu Gavana wa kaunti ya Tana River, aliwaonya wanasiasa kutoka kaunti zingine dhidi ya kuingilia siasa za kaunti hiyo huku Spika wa bunge la kaunti hiyo Osman Noor Galole, akitoa onyo kwa wafanyikazi wa umma dhidi ya kujumu la serikali ya kaunti ya Tana River.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Mwili wapatikana baharini Shelly Beach Likoni

Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza kisa ambapo mwili wa mwanamme ambaye hajafahamika umepatikana ukielea katika maji ya bahari hindi kwenye ufuo wa Shelly Beach eneo bunge la Likoni.
Ripoti ya polisi ilibaini kuwa mwili huo uligunduliwa na wavuvi eneo hilo, ambao walipiga ripoti katika kituo cha polisi cha Shelly Beach kuhusiana na tukio hilo.
Polisi walisema hawakubaini mara moja anakotoka mtu huyo.
Vile vile haikubainika iwapo marehemu alizama au aliuawa kabla ya mwili wake kutupwa baharini.
Polisi walisema hawajakutana na stakabadhi zozote za kumtambulisha mtu huyo huku wakiwasihi wananchi kutoa taarifa iwapo wanafahamu familia ya marehemu.
Mwili unahifadhiwa katika hifadhi ya maiti katika hospitali ya Rufaa ya Coast General Mombasa wakati uchunguzi zaidi ukiendelea.
Taarifa ya Joseph Jira