News
Mbunge wa Kilifi kaszkazini Owen Baya alaumiwa na wanaharakati.

Wanaharakati wa kupambana na utumizi wa dawa za kulevya kanda ya pwani wamemkosoa mbunge wa Kilifi Kaskazini Owen Baya kutokana na hatua ya kuondoa hoja bungeni ya kupinga biashara ya zao la Mugoka.
Wakiongozwa na Famau Mohammed Famau, wanaharakati hao walisema uraibu wa mugoka umeendelea kuathiri maisha ya vijana wengi pwani na walikuwa na matumaini na mbunge huyo kukomboa maisha ya vijana kupitia hoja hiyo.
Famau alimshauri Baya kutowasilisha barua rasmi ya kuhakiki kuondoa hoja hiyo bungeni, ila kuendelea na harakati za kupambana na uraibu wa mugoka na kukomboa maisha ya vijana wa pwani.
“Mheshimiwa Baya alipochukuwa mswada huu kuupeleka bungeni sisi tulifurahi sana na kumpongeza, na hivi sasa kuuondosha bungeni tumekasirika na amefanya jambo la aibu ambalo halingefaa kufanywa na kiongozi kama yeye”, alisema Famau.
Kwa upande wake afisa mratibu mipango katika shirika la Kenya Muslim Youth alliance Asili Randani, aliitaka serikali kuu kuhusisha vijana katika miradi inayoendelea ili kuwaepusha na uhaba wa ajira unaoshuhudiwa miongoni mwao.
“Hapa eneo bunge la Kilifi kaskazini kunajanga kubwa la matumizi ya dawa za kulevya, miradi hii ingehusisha jamii moja kwa moja vijana wetu wasinge kuwa katika swala lile, vijana wakula mugoka wengi wao wamepoteza mwelekeo na wamekuwa wazembe”, alisema Randani.
Afisa mratibu mipango katika shirika la Kenya Muslim Youth alliance Asili Randani akizungumza na wanahabari Kilifi
Itakumbukwa mapema mwaka jana wa 2024 baadhi ya magavana eneo la pwani walipiga marufuku biashara ya zao la mugoka japo vita hivyo havikufaulu.
Taarifa ya Joseph Jira.
News
IEBC inaendelea kutambua vituo vya kusajili wapiga kura

Maafisa wa tume ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC wamesema wanaendelea na zoezi la kutambua sehemu za kuweka vituo vya kusajili wapiga kura hasa maeneo ya mashinani.
Afisa msimamizi wa tume ya IEBC eneo bunge la Ganze kaunti ya Kilifi, Mohammed Bahero Aboud alisema juhudi hizo ni kuhakikisha zoezi la usajili wapiga kura litakaloanza rasmi Septemba 29, mwaka huu linafaulu.
Akizungumza mjini Kilifi, Bahero alisema tume hiyo inatumia mbinu mpya ya kutambua vituo vya jadi vya usajili wapiga kura na kuweka vituo vipya kulingana na mapendekezo ya sheria.
Wakati huo huo alidokeza kwamba tume ya IEBC imekuwa ikihamashisha wakenya kutokubali kushawishiwa na wanasiasa na kujisajili katika maeneo yasiokuwa yao hasa msimu huu ambao zoezi hilo linakaribia kuanza.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Kaunti ya Mombasa kukumbatia matumizi ya mfumo wa miale ya jua

Serikali ya kaunti ya Mombasa imesema imeanza kutekeleza mpango wa kutumia nishati mbadala katika vituo vyote vya huduma za kaunti, kwa kuanza na mabadiliko ya mfumo wa taa hadi kutumia umeme wa miale ya jua.
Kwa mujibu wa waziri wa kawi, rasilimali asili na ustahimilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi kaunti ya Mombasa, Emily Achieng, hatua hii inalenga kupunguza gharama za matumizi ya umeme na kuhimiza matumizi ya nishati safi na rafiki kwa mazingira.
Mbali na hilo, waziri huyo alisema kaunti inaendelea kuweka vifaa maalum vya kupima ubora wa hewa katika maeneo mbalimbali ya mji na ndani ya taasisi za umma.
Lengo ni kupata ushahidi wa kisayansi kuhusu kiwango cha uchafuzi wa hewa, na kuchukuliwa kwa hatua za kisheria kwa wanaokiuka sheria.
Vifaa hivyo tayari vimewekwa katika hospitali ya rufaa ya Coast General na baadhi ya shule ikiwa ni sehemu ya mpango wa muda mrefu wa kaunti, kujenga ustahimilivu dhidi ya madhara ya mabadiliko ya tabianchi.
Mikakati hiyo pia itasaidia kaunti katika kufanya maamuzi kuhusu maeneo yanayofaa kuwekwa biashara fulani, ili kulinda wananchi dhidi ya maradhi yanayosababishwa na uchafuzi wa hewa.
Taarifa ya Mwanahabari wetu.