News
Mbunge wa Kilifi kaszkazini Owen Baya alaumiwa na wanaharakati.

Wanaharakati wa kupambana na utumizi wa dawa za kulevya kanda ya pwani wamemkosoa mbunge wa Kilifi Kaskazini Owen Baya kutokana na hatua ya kuondoa hoja bungeni ya kupinga biashara ya zao la Mugoka.
Wakiongozwa na Famau Mohammed Famau, wanaharakati hao walisema uraibu wa mugoka umeendelea kuathiri maisha ya vijana wengi pwani na walikuwa na matumaini na mbunge huyo kukomboa maisha ya vijana kupitia hoja hiyo.
Famau alimshauri Baya kutowasilisha barua rasmi ya kuhakiki kuondoa hoja hiyo bungeni, ila kuendelea na harakati za kupambana na uraibu wa mugoka na kukomboa maisha ya vijana wa pwani.
“Mheshimiwa Baya alipochukuwa mswada huu kuupeleka bungeni sisi tulifurahi sana na kumpongeza, na hivi sasa kuuondosha bungeni tumekasirika na amefanya jambo la aibu ambalo halingefaa kufanywa na kiongozi kama yeye”, alisema Famau.
Kwa upande wake afisa mratibu mipango katika shirika la Kenya Muslim Youth alliance Asili Randani, aliitaka serikali kuu kuhusisha vijana katika miradi inayoendelea ili kuwaepusha na uhaba wa ajira unaoshuhudiwa miongoni mwao.
“Hapa eneo bunge la Kilifi kaskazini kunajanga kubwa la matumizi ya dawa za kulevya, miradi hii ingehusisha jamii moja kwa moja vijana wetu wasinge kuwa katika swala lile, vijana wakula mugoka wengi wao wamepoteza mwelekeo na wamekuwa wazembe”, alisema Randani.
Afisa mratibu mipango katika shirika la Kenya Muslim Youth alliance Asili Randani akizungumza na wanahabari Kilifi
Itakumbukwa mapema mwaka jana wa 2024 baadhi ya magavana eneo la pwani walipiga marufuku biashara ya zao la mugoka japo vita hivyo havikufaulu.
Taarifa ya Joseph Jira.
News
Wahudumu wa afya Lamu watishia kuishtaki serikali ya kaunti hiyo

Wahudumu wa Afya kaunti ya Lamu wametishia kuelekea Mahakamani kuishtaki serikali ya kaunti hiyo kwa kukaidi kutekeleza matakwa yao.
Wahudumu hao waliishtumu serikali ya kaunti ya Lamu kwa kupuuza matakwa yao na badala yake kutumia vitisho ili kuwashurutisha kurejea kazini.
Kulingana na viongozi wa wahudumu hao, licha ya mgomo wao kuendelea kwa zaidi ya wiki mbili serikali ya kaunti hiyo imekataa kata kuandaa vikao vya kusuluhisha malalamishi yao.
Baadhi ya changamoto wanazolalamikia ni pamoja na kufanya kazi kwa zaidi ya miaka 10 bila ya kupandishwa vyeo, kupuuzwa kwa mkataba wa makubaliano ya nyongeza ya mishahara, kunyimwa kwa mishahara kwa baadhi ya wahudumu hao miongoni mwa matakwa mengine.
“Mkiendelea kutufinyilia itabidi tufuate njia ya sheria kwa sababu tunajua tunalilia haki yetu, haiwezekani serikali ya kaunti inashindwa kutupandisha vyeo ilhali tumefanya kazi kwa miaka 15 sasa, hatuwezi kuendelea kufanya kazi katika mazingira duni na pia mkataba wa makubaliano kuhusu nyongeza ya mishahara sharti itekelezwe” walisisitiza viongozi hao.
Wakati uo huo serikali ya kaunti ya Lamu imejibu malimishi yao kupitia barua na kutangaza kuwa mgomu huo ni kinyume cha seria na kuwataka wahudumu hao kurejea kazini mara moja.
Taarifa ya Elizabeth Mwende
News
Rais Ruto atuma KDF kusimamia ujenzi wa hospitali nchini

Rais William Ruto ametuma jeshi la KDF kusimamia ujenzi wa vituo vya afya zaidi ya 75 kote nchini katika juhudi za kuhakikisha ujenzi unakamilika kwa haraka.
Akizungumza katika kaunti ya Narok wakati wa uzinduzi wa hospitali ya Sogoo Level 4, waziri wa ulinzi Patrick Mariru alifichua kuwa ujenzi wa hospitali hiyo yenye mamlaka kamili itakamilika baada ya mda wa miezi 11.
Ujenzi wa hospitali ya Sogoo Level 4 ulivutia rais Ruto alipozuru eneo hilo mwezi mei mwaka 2025, jambo lililomfanya kuagiza KDF kuipandisha hadhi.
Mariru hata hivyo alishikilia kuwa wafanyikazi wote wasio na ujuzi watatolewa kutoka kwa jamii.
“Jeshi litamsimamia mkandarasi. Hilo liwe wazi, kazi yote itafanywa na vijana wa Sogoo. Tutaweka maafisa wawili na kila jioni watanipa ripoti ya maendeleo,” alisema Mariru.
“Tuna zaidi ya miradi 75 tunayosimamia na sio kwamba tunabadilisha wakala wa serikali tunataka tu kushirikiana na ofisi tofauti miongoni mwao wizara za afya na michezo.”
Taarifa ya Joseph Jira