News
Mahakama kuu yabatilisha uamuzi wa bunge la Kilifi dhidi ya Spika Mwambire

Mahakama kuu ya Malindi imebatilisha uamuzi wa bunge la kaunti ya Kilifi wa kumtimua Mamlakani Spika wa bunge hilo Teddy Mwambire na kuagiza Spika Mwambire kurejea kazini.
Jaji Njagi aliagiza pia Spika Mwambire kurejea kazi licha ya bunge hilo kumtimua Mamlakani Juni 30 kutokana na madai ya kutokuwa na imani naye.
Jaji Njagi alilitaka bunge hilo kuzingatia kanuni na sheria na kumpa nafasi Spika Mwambire kutekeleza majukumu yake ya kikazi kwa mujibu wa sheria hadi kesi hiyo iliyowasilishwa na Mahakamani itakaposkizwa na kuamuliwa.
Jaji huyo hata hivyo aliwasilisha faili ya kesi hiyo kwa Jaji Mugure Thande ambapo kesi hiyo itaskizwa rasmi mnamo tarehe 14, Julai mwaka huu huku walalamishi wa kesi hiyo akiwemo Kassim Mwadena na Emmanuel Kazungu Chai wakidai kwamba bunge hilo lilikiuka sheria na haki za Spika Mwambire.
Itakumbukwa kwamba mnamo Juni 30 mwaka huu, bunge la kaunti ya Kilifi lilipiga kura 40 kati ya 50 na kuidhinishwa kutimuliwa Mamlakani kwa Spika Mwambire kwa misingi ya ukiukaji wa Katibu, utumizi mbaya wa ofisi ya umma, ukandamizaji wa miradi ya serikali ya kaunti ya Kilifi miongoni mwa shtuma zengine.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Anselim, ashutumu utovu wa usalama Taita Taveta

Kaimu Spika katika bunge la kaunti ya Taita Taveta Anselim Mwadime alieleza kusikitishwa na mauaji ya mhudumu mmoja wa bodaboda aliyeuliwa na kisha pikipiki yake kuchukuliwa katika eneo la chuo kikuu cha Taita Taveta.
Mwadime alisema kuna baadhi ya abiria ambao ni wahuni hubebwa na kisha kuwashambulia wahudumu wa pikipiki hadi kuwaua au hata kutoweka na pikipiki.
Aidha, Mwadime alisema kama viongozi wa kaunti ya Taita Taveta hawataruhusu visa hivyo kuendelezwa katika kaunti hiyo.
Vilevile, Mwadime aliishinikiza idara ya usalama kwenye kaunti ya Taita Taveta kuwajibika ipasavyo ili kudhibiti visa vya utovu wa usalama katika sekta ya bodaboda na wanaohusika wakabiliwe kisheria.
“Hili jambo linafaa kufuatiliwa kwa undani. Na tunalilaani vikali sisi kama viongozi wa Taita Taveta’’ alisema Mwadime.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Viongozi wahimizwa kushirikiana kubuni ajira kwa vijana

Mwakilishi wa wadi ya Sabaki eneo bunge la Magarini kaunti ya Kilifi Rose Baraka alitoa wito kwa viongozi wa kaunti ya Kilifi kushirikiana na mashirika ya kijamii pamoja na wawekezaji katika kaunti ya Kilifi ili kudhibiti changamoto za ukosefu wa ajira miongoni mwa vijana.
Rose alisema hatua hiyo itasaidia pakubwa kuwaepusha vijana kujiingiza kwenye utumizi wa mihadarati sawa na uhalifu.
Akizungumza wakati wa kikao kilichowaleta pamoja maafisa wa shirika la SHOFCO pamoja na wakaazi wa Sabaki, Rose aliahidi kushirikiana na mashirika mbalimbali ya kijamii katika juhudi za kuwasadia wananchi kujiendeleza kupitia mpango wa ajira.
“Vijana ni wengi, kazi ni kidogo. Sisi kama viongozi tunastahili kutia bidii kutafuta haya mashirika ili tuangalie vijana wetu wasaidika vipi’’ alisema Rose Baraka.
Kwa upande wake Afisa wa Shirika la SHOFCO eneo la Magarini Kelvin Mtawali Karisa aliupongeza ushirikiano wa mwakilishi wa wadi huyo na shirika hilo na kuwataka vijana kujiunga kwenye makundi mbalimbali ili waweze kupata mikopo ya kujiendeleza kimaisha.
Taarifa ya Janet Mumbi