News
KESSHA: Huenda shule za upili zikafungwa kufuatia ukosefu wa fedha

Katibu Mkuu wa Muungano wa walimu wakuu wa shule za upili nchini KESSHA Abdinoor Haji
ameonya kuhusu uwezekano wa shule kufungwa mapema iwapo pesa za kugharimia masomo hazitatolewa haraka.
Haji alisema ukosefu wa fedha hizo umeathiri shughuli mbalimbali shuleni kote nchini.
Haji alisema ucheleweshwaji wa kutolewa kwa fedha hizo umesababisha viwango vya elimu kudorora na ndio chanzo kikuu cha upatikanaji wa alama za E katika mitihani ya kitaifa ya KCSE kwa muda wa miaka mitatu iliyopita.
“Shule za kutwa ndizo ziliathiriwa zaidi kwa sababu zinategemea pakubwa fedha hizo za serikali. Ukosefu wa fedha hizo umedumaza uwezo wa kufanikisha upatikanaji wa elimu bora,” alisema Haji.
Aidha, alisema kutokana na ukosefu wa fedha, shule nyingi zimeshindwa kuwalipa wasambazaji bidhaa huku baadhi ya shule zikilazimika kuwaachisha kazi walimu walioajiriwa na bodi za usimamizi wa shule.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa KESSHA Willy Kuria alisema shule za upili zinaidai serikali kuu shillingi bilioni 17 za muhula wa kwanza na wa pili.
Kuria alisema ikiwa Wizara ya Elimu nchini itakosa kulipa malimbikizi hayo ya madeni, shule zitalazimika kufungwa mapema kwa sababu ya ukosefu wa pesa za kuwaweka wanafunzi shuleni.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Mboko: Serikali lazima ikomeshe mauaji dhidi ya Wanawake

Mbunge wa Likoni Mishi Mboko ameitaka serikali kuhakikisha inakomesha mauaji ya kiholela na unyanyasaji wa kingono dhidi ya Wanawake nchini.
Akizungumza na Wanahabari, Mishi alisema ni jambo la kusikitisha na kuhuzunisha kuona Wanawake wakiendelea kuuawa kila uchao na katika mazingira ya kutatanisha pasi na hatua zozote za kisheria kuchukuliwa dhidi ya wahusika.
Mbunge huyo aliitaka serikali kuongeza ufadhili kwa Muungano wa Wabunge Wanawake ili kuwawezesha kufanikisha kampeni ya kuhamasisha kwa umma dhidi ya ukatili wa kijinsia.
“Ni lazima visa kama hivi vikomeshwe, tumechoka na mauaji ya kila mara ya wanawake nchini na sisi pia tuko na haki ya kuishi na tunaiambia serikali kupitia bunge itenge pesa kupitia muungano wa wabunge wanawake ili kuelimisha jamii kuhusu kukomesha mauaji ya wanawake nchini”, alisema Mishi.

Mbunge wa Likoni na Wanawake wakipinga mauaji ya kiholela dhidi ya wanawake
Wakati huo huo aaliwataka maafisa wa usalama kushika doria kikamilifu hasa katika maeneo yanayokumbwa na visa vya ukatili dhidi ya wanawake huku akipendekeza mashirika yasiokuwa ya kiserikali kushirikiana na viongozi katika juhudi za kukomesha visa hivyo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Christine: Wahudumu wa afya 1,340 wapokea mafunzo Taita Taveta

Serikali ya kaunti ya Taita Taveta kupitia Wizara ya Afya inaendelea kutoa mafunzo kwa wahudumu wa afya wa nyanjani ili kuwawezesha kutekeleza majukumu yao bila vikwazo.
Naibu Gavana wa kaunti ya Taita Taveta Christine Kilalo alisema kuwa kati ya wahudumu hao 1,340 asilimia 75 tayari wanaendelea na mafunzo katika ngazi tofauti.
Kilalo aliahidi kushirikiana na wahudumu hao licha ya changamoto zinazowakabili nyanjani.
“Wamekubali wakafundiashwa ili waweze kutoa elimu ya afya na waweze kusaidia jamii kwa mambo ya usafi na pia kusaidia katika kuwasilisha ujumbe za kiafya na pia wakipata wagonjwa waweze kuwatuma mahali wanaweza wakapata huduma za matibabu’’, alisema Kilalo.
Wakati uohuo alidokeza kuwa serikali ya kaunti hiyo kwa ushirikiano na serikali kuu wameweka mikakati ya kuhakikisha wahudumu hao wanalipwa fedha ambazo zitawasaidia kujikimu kimaisha pamoja na familia zao.
“Tulikubaliana kama taifa asilimi 50 ambayo ni elfu mbili mia tano inalipwa na serikali kuu na asilimia 50 ambayo ni elfu mbili mia tano inalipwa na serikali ya kaunti na kama serikali tunaemda kukamilisha malipo’’, aliongeza Kilalo.
Taarifa ya Janet Mumbi