News
Karua na Mutunga, waishtaki Tanzania

Aliyekuwa Jaji mkuu nchini Willy Mutunga pamoja na Kinara wa chama cha People’s Liberation Party Martha Karua wameishtaki serikali ya Tanzania katika Mahakama ya Haki ya Afrika Mashariki (EACJ).
Mutunga na Karua pamoja na Wanaharakati wengine wanane wa haki za binadamu akiwemo Hussein Khalid, Gloria Kimani, Lyn Nguji, Hanifa Adan, Boniface Mwangi na Agatha Atuhaire walishtumu serikali hiyo kwa kuwazuia kuingia nchini humo.
Wanane hao walidai kwamba haki zao zilikiukwa kwa kuondolewa kwa nguvu nchini humo huku wakidai kwamba serikali ya Tanzania ilikiuka mikataba ya Kikanda.

Jumba la Jumuiya ya Afrika Mashariki iliyo na Mahakama ya EACJ
Wanane hao sasa wanaitaka Mahakama hiyo kuishurutisha serikali ya Tanzania kuondoa alama zozote hasi za uhamiaji kwenye Pasipoti zao za usafiri na kuwalipa fidia maalum kwa gharama walizopata wakitafuta ushauri wa kisaikolojia kutokana na msongo wa mawazo na kihisia.
Haya yanajiri wiki chache baada ya Willy Mutunga, Martha karua na Wanaharakati wanane wa kutetea haki za kibinadamu kutoka nchini Kenya na Uganda kutimuliwa nchini humo baada ya kuzuiliwa.
Wakenya hao walikuwa wamezuru nchini kusikiliza na kumuakilisha Kiongozi wa chama cha upinzani nchini humo Tundu Lissu katika kesi ya uhaini inayomkabili.
Lissu ambaye anakabilia na kesi ya uhaini pamoja na tuhuma za kuchapisha taarifa za uongo yupo rumande akisubiri kesi yake kutajwa tena tarehe 16 mwezi Juni 2025.
Taarifa ya Elizabeth Mwende
News
Nassir: Kaunti ya Mombasa wametenga milioni 80 za Afya

Gavana wa kaunti ya Mombasa, Abdulswamad Shariff Nassir amesema serikali ya kaunti ya Mombasa wametenga shilingi milioni 80 kugharamia sehemu ya matibabu ya wakaazi ambao hutibiwa katika hospitali za Level 4 na Level 5.
Akizungumza katika kaunti ya Mombasa, Nassir alisema fedha hizo zitagharamia bima ya afya ya SHA ya wenyeji wa kaunti hiyo kwa muda wa mwaka mmoja.
Gavana Nassir pia alisema fedha hizo zitagharamia madeni ya ziada ya matibabu kwa watoto wa chini ya umri wa miaka 5 ambao wanatibiwa kupitia bima hiyo ya SHA.
“Tumeweka dawati maalum na fedha kuweza kuwalipia ile amana ambayo ilikuwa inalipiwa SHA. Na itakuwa sio ya Public health pekee lakini kando na Public health mnakuwa mumelipiwa kwa mwaka mzima’’, alisema gavana Nassir
Wakati huo huo Gavana Nassir alieleza matumaini kwamba mpango huo utasaidia kwa asilimia kubwa kuimarisha huduma za matibabu kwa wenyeji wa kaunti hiyo.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Chibule, apendekeza adhabu kali kwa wanaoendeleza dhulma za kijinsia

Naibu gavana kaunti ya Kilifi Flora Mbetsa Chibule, amependekeza adhabu kali kwa watu wanaotekeleza visa vya dhulma za kijinsia katika jamii.
Chibule alisema visa vya dhulma za kijinsi dhidi ya watoto vimekithiri katika jamii hasa kaunti ya Kilifi, akiahidi ushirikiano wa hali ya juu na wadau mbalimbali ili kukomesha visa hivyo.
Akizungumza wakati wa maadhimisho ya hamasa kuhusu dhulma za kijinsia katika uwanja wa Bofa Youth mjini Kilifi, Chibule alisema ili kufanikisha ndoto ya mtoto wa kike ni lazima haki zao za kimsingi zilindwe.
“Kwa ambao wanadhulumu mtoto wa kike na kiume, kwa wale ambao wanaingia misuli kwa misuli wanafaa kuwekwa gerezani kabisa”, alisema Chibule.

Wanaharakati wa kijamii wapinga unyanyasaji wa kijinsi, Kilifi
Kwa upande wake Mwakilishi wa kike kaunti ya Kilifi Getrude Mbeyu aliyeandaa hafla hiyo kupitia hazina ya kitaifa ya NGAAF na kutoa hundi ya kima cha shilingi milioni 1.6 kwa makundi 14, alisisitiza hamasa zaidi kwa jamii kuhusu jinsi ya kukomesha visa hivyo.
“Ni jukumu letu la kuwaeleza hawa watu watambua jinsi ya kuripoti hizi kesi, yani kwa mfano umedhulumiwa ni wapi pa kuanzia na hatua hii itakomesha hizi visa”, alisema Mbeyu.
Naye Mzee wa mataa wa Kiwandani mjini Kilifi Elina Nyevu alisema visa vya dhulma za kimapenzi vimekithiri mno katika mtaa huo, akipendekeza hamasa zaidi kwa jamii.
“Hapa kwetu Kiwandani visa vya dhulma za kijinsia ni vingi sana, kuna ulevi na ukosefu wa ajira ambao umechangia utumiaji wa Mihadarati na unyanyasaji wa watoto wadogo kimapenzi, alisema Elina.
Hata hivyo katika halfa hiyo baadhi ya watoto waliopitia madhila hayo hasa ubakaji wameelezea masaibu waliopitia japo haki yao kupitia idara ya usalama walikosa kufaulu.
Taarifa ya Lolani Kalu.