News
Kampuni ya Simba Cement yafungwa, Kaloleni

Serikali ya kaunti ya Kilifi kwa ushirikiano na Wizara ya Madini imesitisha rasmi shughuli zote za uchimbaji madini zinazotekelezwa na kampuni ya Simba Cement eneo la Kaloleni kaunti ya Kilifi.
Agizo hilo limetolewa na Gavana wa kaunti ya Kilifi Gideon Mung’aro pamoja na Waziri wa madini na raslimali za uchumi wa bahari nchini Ali Hassan Joho, wakisema kampuni hiyo imeshindwa kufuata sheria za mazingira na haiwafaidi wakaazi wa eneo hilo.
Viongozi hao walisema shughuli za uchimbaji wa kampuni hiyo zimekuwa zikiathiri mazingira na wakazi wa maeneo ya karibu, huku wakiahidi kwamba serikali haitavumilia ukosefu wa uwajibikaji unaotishia afya na maisha ya wananchi.
Walisisitiza kwamba kampuni hiyo haitaruhusiwa kuendelea na shughuli zake hadi pale itakapokidhi masharti yote ya kisheria na kuthibitisha kwamba haileti madhara kwa binadamu wala mazingira.
“Hii kampuni wacha nikuambie waziri haisadii wananchi wa Kilifi kwa chochote waziri, na leo hii watu wa kambe ribe mnisikize na mnisikize kwa makini, vile nilifanya Jaribuni ndivyo nitakavyofanya leo, kuanzia kesho asubuhi na nitawafuata na barua kesho mwelezeni mwajiri wenu kwamba hii kampuni tumeifunga na nitawafuata na barua”, alisema Gavana Mung’aro.
Hatua hii iliungwa mkono na baadhi ya viongozi wa jamii na wanaharakati wa mazingira, wakisema kuwa ni wakati wa kuwajibisha wawekezaji wanaokiuka haki za wananchi kwa msingi ya maendeleo.
Simba Cement, ambayo imekuwa ikihusishwa na miradi mikubwa ya ujenzi, sasa inalazimika kukabiliwa na masharti mapya kabla ya kurejelea shughuli zake za kawaida.
Taarifa ya Elizabeth Mwende
News
Mahakama kuu yatupilia mbali ombi la Gachagua

Mahakama kuu imetupilia mbali ombi la pili la aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua la kutaka jopo la majaji watatu wanaosikiliza kesi ya kupinga kubanduliwa wake mamlakani kuzuiliwa kuskiza kesi hiyo.
Gachagua alisema kwamba majaji hao watatu akiwemo Jaji Eric Ogola, Anthony Mrima na Fridah Mugambi wanafaa kuondolewa kwenye kesi hiyo kwa misingi kwamba uteuzi wao haujazingatia sheria.
Mahakama hiyo ilitupilia mbali ombi hilo, na kusema kwamba jopo hilo la majaji watatu liliteuliwa na Jaji mkuu Martha Koome kwa kuambatana na sheria na kanuni za idara ya Mahakama.
Mahakama imeshikilia kwamba jopo hilo la majaji wa Mahakama kuu litaendelea kusikiliza kesi hiyo hadi wakati wa kutoa uamuzi kwa kuzingatia sheria, na kanuni za idara ya Mahakama pamoja na Katiba ya Kenya.
Mahakama hiyo pia ilitupilia mbali ombi la Mwanaharakati Fredrick Mula ambaye alitaka kubadilishwa kuwa mlalamishi katika kesi nne za kuondolewa mashtaka dhidi ya aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua ambazo alikuwa amewasilisha awali na kisha kutaka kujiondoa.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Wazee wa Kaya wanataka bunge kupitisha sheria kudhibiti mauaji ya wazee

Muungano wa Wazee wa Kaya kaunti ya Kilifi umeitaka serikali kuu kupitia bunge la kitaifa kubadilisha sheria ya mwaka wa 1926 kuhusu uchawi ili kuwezesha utamaduni kudhibiti mauaji ya wazee yanayoendelea kushuhudiwa kaunti ya Kilifi.
Wakiongozwa na Stanley Kahindi Kiraga wamesema kuwa sheria hiyo imechangia pakubwa mauaji ya wakongwe Kilifi kutokana na swala kuwa haitambui uwepo wa uchawi na jinsi ya kuudhibiti.
Kiraga sasa anasema ni sharti sheria hiyo iondolewe au ifanyiwe ukarabati bungeni hali itayopelekea uchawi kudhibitiwa kupitia mila na utamaduni.
“Vijana wanaowaua wazee wakiwasingizia kuwa wachawi wanazidi kuongezeka na kwa sababu hakuna sheria ya moja kwa moja ya kuwashtaki na kuwafunga” amesema Kiraga akieleza kusikitishwa kwake na ongezeko la magenge ya vijana wanaolipwa kutekelezwa mauaji ya wazee kwa shutuma za uchawi.
Taarifa ya Hamis Kombe