News
Kampeni ya Chanjo kwa watoto yafanikiwa nchini

Wizara ya afya nchini imesema kufikia sasa watoto milioni 3.3 wamepokezwa chanjo ya surua kati ya watoto milioni 6.5 waliolengwa.
Ripoti ya wizara hiyo pia iliongeza kuwa watoto milioni 12.1 wamepokea chanjo ya homa ya matumbo kati ya waliolengwa milioni 19.2.
Vile vile ripoti hiyo ilisema kuwa zaidi ya watoto elfu nne ambao walikuwa hawajapokea chanjo yeyote awali sasa wamefanikiwa kuchanjwa.
Wizara hiyo iliongeza kuwa kampeni hiyo ya kitaifa ya chanjo iliyoanza tarehe 5 Julai, 2025, imepokelewa vyema na wazazi, viongozi wa dini, walezi, wahudumu wa afya na wakenya kwa jumla.
Wizara hiyo ilishauri wazazi na walezi kuhakikisha watoto wao wanapewa chanjo hiyo ikiwa zimesalia siku tatu pekee kabla kampeni kuu kukamilika.
Chanjo hizo zimeidhinishwa na shirikala afya dunia WHO na zimethibitshwa kuwa salama, bora na huokoa maisha.
Waziri wa afya Aden Duale alisema serikali imejitolea kuhakikisha hakuna mtoto atakayepoteza maisha kwa ugonjwa unaoweza kuzuilika kwa Chanjo.
Taarifa ya Joseph Jira
News
David Maraga amfokea mkurugenzi wa mashtaka ya umma

Jaji mkuu mstaafu David Maraga amefokea ofisi ya mkurugenzi wa mashtaka ya umma kwa kuwashtaki kwa makosa ya ugaidi vijana waliokamatwa wakati wa maandamano.
Maraga alisema hatua hiyo inawadhulumu vijana hao ambao wamesalia korokoroni wakisubiri kesi yao kuamuliwa.
Maraga pia aliaka kesi hizo zitupiliwe mbali akisema hazina msingi, akidai hatua hiyo ni utumizi mbaya wa sheria kwa madai ya kukabiliana na magaidi, ilihali walioshtakiwa walikuwa wakishinikiza uongozi bora nchini.
Maraga pamoja na wanaharakati wa kutetea haki za binadam walimtaka mkurugenzi wa mashtaka ya umma Renson Ingonga kuwajibika na kutupilia mbali kesi hizo na kuwaruhusu washukiwa kuendelea na maisha yao.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Ripoti ya upasuaji:Wakili Mathew Kyalo Mbobu alipigwa risasi mara nane

Ripoti ya upasuaji wa maiti kuhusu kifo cha wakili Mathew Kyalo Mbobu imebaini alipigwa risasi mara nane katika tukio la uvamizi ambalo lilisababisha kifo chake.
Kulingana na mpasuaji mkuu wa serikali Dkt. Johansen Oduor, risasi mbili zimepatikana zikiwa zingali mwilini, moja ikiwa imekwama kwenye uti wa mgongo.
Oduor alidokeza kuwa uvamizi huo ulitekelezwa kwa maksudi na kwa karibu zaidi ambapo risasi nyingi zilimpiga upande wake wa kulia.
Oduor vile vile alifichua kuwa majeraha kwenye sehemu ya shingo na uti wa mgongo yalisababisha uvujaji wa damu nyingi hali iliyochangia kifo.
Awali spika wa bunge la seneti Amason Kingi aligiza asasi za usalama kufanya uchunguzi wa haraka kufuatia kifo cha wakili Mbobu.
Kingi alimtaja mauaji ya wakili huyo kama yakinyama huku akimtaja wakili Mbobu kama mtu jasiri na aliyejitolea kuhudumia raia.
Wakili huyo alifariki baada ya kupigwa risasi jioni siku ya jumanne tarehe 9 Septemba 2025, akiwa katika gari lake kwenye barabara ya Lang’ata.
Taarifa za polisi zilisema mwathiriwa alipigwa risasi na watu waliokuwa kwenye pikipiki muda mfupi baada ya saa moja na nusu usiku.
Ilisemekana wakili huyo alikuwa akiendesha gari kuelekea nyumbani wakati mshambuliaji aliposimamisha pikipiki kando ya gari lake na kufyatua risasi kabla ya kuondoka kwa kasi.
Taarifa ya Joseph Jira