News
JSC, yashutumu mashambulizi dhidi ya Idara ya Mahakama

Tume ya huduma za Mahakama nchini JSC imeshtumu vikali tabia inayoendelea kusheheni nchini ya kuwashambulia hadharani majaji kuhusu uamuzi wanaoutoa wa dhamana kwa washukiwa wa kesi za maandamano.
Katika taarifa iliyotolewa na JSC kupitia Katibu wa Idara wa Tume hiyo Winfridah Mokaya, ilisema tume hiyo imeonyesha wasiwasi mkubwa kuhusu athari za maamuzi ya hivi majuzi yaliyotolewa na Mahakama ya Nanyuki.
Katika Mahakama hiyo zaidi ya watu 100 waliokamatwa kutokana na maandamano ya Julai 7 katika kaunti ya Laikipia waliachiliwa kwa dhamana ya shilingi elfu 50 pesa taslimu kila mmoja baada ya kushtakiwa kwa uharibifu wa mali.
“Tunashangazwa na tabia ya kuwashambulia majaji hadhara kuhusu uamuzi wanaotoa kuhusu washukiwa wa maandamano ya Juni 25 na Julai 7 wakati wa maandamano ya Sabasaba na Mahakama iko kisheria na inafuata sheria”, alisema Mokaya.
Winfridah ambaye pia ni Msajili mkuu wa Idara ya Mahakama nchini amesema wakosoaji akiwema Jaji mkuu wa zamani David Maraga ambao wanashinikiza kuondolewa kwa mashtaka ya ugaidi dhidi ya waandamanaji, akisema wanafaa kuheshimu mahakama.
Wakati huo huo ameonya kwamba mashambulizi dhidi ya idara ya Mahakama huenda yakasambaratisha shughuli za kupatikana haki kwa wananchi.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Kongamano la kukomesha visa vya dhuluma za kijinsia Taita Taveta

Idara ya usalama kaunti ya Taita taveta imeandaa kongamano maalum ili kujadili namna ya kukomesha visa vya dhuluma za kijinsia na kingono kaunti hiyo.
Kongamano hilo limefanyika katika eneo la Werugha, eneo bunge la Wundanyi kaunti ya Taita Taveta na limejumuisha maafisa wakuu wa serikali ya kaunti hiyo, viongozi wa kijamii pamoja na wananchi.
Kamishna wa kaunti ya Taita Taveta Josephine Onunga alibainisha kuwa kuna ongezeko la visa 186 ndani ya miaka miwili, eneo bunge la Taveta likirekodi visa 64 huku Wundanyi ikirekodi 38 hivyo kuwataka wakaazi kushirikiana na idara mbalimbali za usalama ili kukomesha visa hivyo.
“Tunapendekeza ushirikiano mkubwa zaidi na zaidi kuanzia mashinani kila boma tulindane, tujuliane hali, hakikisha unamlinda mwenzako”, alisema Onunga.
Kwa upande wao Wanaharakati wa kupambana na dhuluma za kijinsia wakiongozwa na Mary Mgola walieleza hofu yao kutokana na ongezeko la visa hivyo hasa maeneo ya mashinani.
Walisema ukosefu wa mashahidi wa kutosha wakati kesi hizo zinapowasilishwa Mahakamani, ikitajwa kama changamoto kuu wakati wa kusuluhisha kesi hizo.
Mgola aliitaka Mahakama kuhakikisha wanatoa ulinzi wa kutosha kwa mashahidi wa kesi za dhuluma za kijinsia na kingono.
Taarifa ya Elizabeth Mwende
News
Mboko: Serikali lazima ikomeshe mauaji dhidi ya Wanawake

Mbunge wa Likoni Mishi Mboko ameitaka serikali kuhakikisha inakomesha mauaji ya kiholela na unyanyasaji wa kingono dhidi ya Wanawake nchini.
Akizungumza na Wanahabari, Mishi alisema ni jambo la kusikitisha na kuhuzunisha kuona Wanawake wakiendelea kuuawa kila uchao na katika mazingira ya kutatanisha pasi na hatua zozote za kisheria kuchukuliwa dhidi ya wahusika.
Mbunge huyo aliitaka serikali kuongeza ufadhili kwa Muungano wa Wabunge Wanawake ili kuwawezesha kufanikisha kampeni ya kuhamasisha kwa umma dhidi ya ukatili wa kijinsia.
“Ni lazima visa kama hivi vikomeshwe, tumechoka na mauaji ya kila mara ya wanawake nchini na sisi pia tuko na haki ya kuishi na tunaiambia serikali kupitia bunge itenge pesa kupitia muungano wa wabunge wanawake ili kuelimisha jamii kuhusu kukomesha mauaji ya wanawake nchini”, alisema Mishi.

Mbunge wa Likoni na Wanawake wakipinga mauaji ya kiholela dhidi ya wanawake
Wakati huo huo aaliwataka maafisa wa usalama kushika doria kikamilifu hasa katika maeneo yanayokumbwa na visa vya ukatili dhidi ya wanawake huku akipendekeza mashirika yasiokuwa ya kiserikali kushirikiana na viongozi katika juhudi za kukomesha visa hivyo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu