News
IEBC yahakikishia wakenya usalama wa taarifa za usajali

Tume uchaguzi na mipaka nchini (IEBC) imerejesha tovuti yake ambayo wapigakura huthibitisha taarifa zao za usajili, baada ya kipindi cha ukarabati.
Hii ni kufuatia malalamishi ya umma kuhusu hitilafu isiyoeleweka ambayo ilisababisha mamilioni ya wakenya kushindwa kupata taarifa zao za usajili kama wapigakura.
Tume hiyo ilitangaza kwamba tovuti hiyo sasa imerejea mtandaoni, kufuatia kipindi cha ukarabati wa mfumo unaolenga kuhamisha miundombinu yake ili kuimarisha utendakazi na usalama.
Tangazo hilo lilifuatia siku za sintofahamu ambapo wakenya hawakuweza kuthibitisha maelezo yao ya usajili, iwe kupitia tovuti ya IEBC au kwa njia ya ujumbe mfupi.
Wapigakura walipata ugumu wa kutuma nambari ya kitambulisho au ya pasipoti pamoja na mwaka wao wa kuzaliwa, kulingana na mahitaji ya IEBC.
Njia zote mbili za uthibitishaji hazikuweza kufikiwa wakati wa ukarabati, na hivyo kusababisha wasiwasi kuongezeka, haswa wakati joto la kisiasa linapozidi kuongezeka kuelekea uchaguzi Mkuu wa mwaka 2027.
Katika taarifa iliyotolewa siku ya Jumapili 6, Julai 2025 bodi ya uchaguzi iliwahakikishia wapiga kura, ikisema, “Tungependa kuwahakikishia wakenya wote kwamba maelezo ya usajili wa wapigakura 22,120,458 waliojiandikisha, kama yalivyorekodiwa wakati wa uchaguzi mkuu wa 2022, yanasalia shwari na salama.
IEBC iliongeza kuwa uboreshaji wa mfumo ulikuwa muhimu ili kuimarisha utoaji wa huduma kupitia utendakazi bora wa mfumo na usalama wa data.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Anselim, ashutumu utovu wa usalama Taita Taveta

Kaimu Spika katika bunge la kaunti ya Taita Taveta Anselim Mwadime alieleza kusikitishwa na mauaji ya mhudumu mmoja wa bodaboda aliyeuliwa na kisha pikipiki yake kuchukuliwa katika eneo la chuo kikuu cha Taita Taveta.
Mwadime alisema kuna baadhi ya abiria ambao ni wahuni hubebwa na kisha kuwashambulia wahudumu wa pikipiki hadi kuwaua au hata kutoweka na pikipiki.
Aidha, Mwadime alisema kama viongozi wa kaunti ya Taita Taveta hawataruhusu visa hivyo kuendelezwa katika kaunti hiyo.
Vilevile, Mwadime aliishinikiza idara ya usalama kwenye kaunti ya Taita Taveta kuwajibika ipasavyo ili kudhibiti visa vya utovu wa usalama katika sekta ya bodaboda na wanaohusika wakabiliwe kisheria.
“Hili jambo linafaa kufuatiliwa kwa undani. Na tunalilaani vikali sisi kama viongozi wa Taita Taveta’’ alisema Mwadime.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Viongozi wahimizwa kushirikiana kubuni ajira kwa vijana

Mwakilishi wa wadi ya Sabaki eneo bunge la Magarini kaunti ya Kilifi Rose Baraka alitoa wito kwa viongozi wa kaunti ya Kilifi kushirikiana na mashirika ya kijamii pamoja na wawekezaji katika kaunti ya Kilifi ili kudhibiti changamoto za ukosefu wa ajira miongoni mwa vijana.
Rose alisema hatua hiyo itasaidia pakubwa kuwaepusha vijana kujiingiza kwenye utumizi wa mihadarati sawa na uhalifu.
Akizungumza wakati wa kikao kilichowaleta pamoja maafisa wa shirika la SHOFCO pamoja na wakaazi wa Sabaki, Rose aliahidi kushirikiana na mashirika mbalimbali ya kijamii katika juhudi za kuwasadia wananchi kujiendeleza kupitia mpango wa ajira.
“Vijana ni wengi, kazi ni kidogo. Sisi kama viongozi tunastahili kutia bidii kutafuta haya mashirika ili tuangalie vijana wetu wasaidika vipi’’ alisema Rose Baraka.
Kwa upande wake Afisa wa Shirika la SHOFCO eneo la Magarini Kelvin Mtawali Karisa aliupongeza ushirikiano wa mwakilishi wa wadi huyo na shirika hilo na kuwataka vijana kujiunga kwenye makundi mbalimbali ili waweze kupata mikopo ya kujiendeleza kimaisha.
Taarifa ya Janet Mumbi