News
IEBC yahakikishia wakenya usalama wa taarifa za usajali

Tume uchaguzi na mipaka nchini (IEBC) imerejesha tovuti yake ambayo wapigakura huthibitisha taarifa zao za usajili, baada ya kipindi cha ukarabati.
Hii ni kufuatia malalamishi ya umma kuhusu hitilafu isiyoeleweka ambayo ilisababisha mamilioni ya wakenya kushindwa kupata taarifa zao za usajili kama wapigakura.
Tume hiyo ilitangaza kwamba tovuti hiyo sasa imerejea mtandaoni, kufuatia kipindi cha ukarabati wa mfumo unaolenga kuhamisha miundombinu yake ili kuimarisha utendakazi na usalama.
Tangazo hilo lilifuatia siku za sintofahamu ambapo wakenya hawakuweza kuthibitisha maelezo yao ya usajili, iwe kupitia tovuti ya IEBC au kwa njia ya ujumbe mfupi.
Wapigakura walipata ugumu wa kutuma nambari ya kitambulisho au ya pasipoti pamoja na mwaka wao wa kuzaliwa, kulingana na mahitaji ya IEBC.
Njia zote mbili za uthibitishaji hazikuweza kufikiwa wakati wa ukarabati, na hivyo kusababisha wasiwasi kuongezeka, haswa wakati joto la kisiasa linapozidi kuongezeka kuelekea uchaguzi Mkuu wa mwaka 2027.
Katika taarifa iliyotolewa siku ya Jumapili 6, Julai 2025 bodi ya uchaguzi iliwahakikishia wapiga kura, ikisema, “Tungependa kuwahakikishia wakenya wote kwamba maelezo ya usajili wa wapigakura 22,120,458 waliojiandikisha, kama yalivyorekodiwa wakati wa uchaguzi mkuu wa 2022, yanasalia shwari na salama.
IEBC iliongeza kuwa uboreshaji wa mfumo ulikuwa muhimu ili kuimarisha utoaji wa huduma kupitia utendakazi bora wa mfumo na usalama wa data.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Mvuvi aliyezama baharini Watamu apatikana Tanariver

Mwili wa mvuvi Hudhefa Laly aliyepotea baharini huko Watamu eneo bunge la Kilifi Kaskazini Kaunti ya Kilifi akiwa na ndugu yake Athman Laly umepatikana eneo la Shakiko -Mathole, kaunti ya Tana River.
Ndugu hao wawili walitoweka habarini siku ya Alhamisi 24, Julai 2025 katika bahari hindi wakati wakiendelea na shughuli zao za uvuvi.
Vitengo mbali mbali vya uokozi vimekuwa vikiendesha zoezi la kutafuta miili ya wawili hao kwa ushirikiano na wavuvi eneo la Watamu.
Kufikia sasa mwili wa Athman Laly kakake Hudhefa ungali haujapatikana huku juhudi za kuutafuta zikiendelea.
Jamii ya wavuvi katika eneo la Watamu ikiongozwa na kiongozi wa vijana Bakari Shaban iliiomba serikali ya kaunti ya Kilifi na ile ya kitaifa kununua boti za uokozi ili kusaidia kuokoa maisha wakati kunapotokea dharura baharini.
“Tunaomba tupate boti za kuokoa maisha baharini, popote alipo waziri Ali Joho angalau tupate boti za uokozi kama mbili hapa Watamu ni kitovu cha utalii kunamahoteli mengi, watalii wote wanaokuja Watamu mpaka leo hakuna boti za uokozi”, alisema Shaban.
Awali wao wazazi wa wavuvi waliopotea baharini Lali Athman Lali na Dhurai Mohamed Ali waliiomba serikali kuweka juhudi zaidi za kuwasaidia kuwapata wanawao kwani ndio tegemeo kubwa kwa familia yao.
“Uko usaidizi unatumika, kuna vijana wanaojitolea kwa maboti wanaenda ile sehemu ambayo wavuvi wanavua, wanajaribu kuzunguka lakini toka siku hiyo hawajapata chochote: Katika Maisha yangu mimi nawategemea hawa watoto kunisomeshea hawa watoto wangu ambao ni wadogo zao mashule, kwa chakula kwa hivyo naomba serikali inisaidie kwa sababu ndio tegemeo langu hao watoto”.walisema wazazi.
Kisa hiki kilijiri miezi kadhaa baada ya mvuvi mmoja kutoka eneo la Mnarani mjini Kilifi kufariki baharini baada ya kugongwa kichwani kwa pondo na wavuvi wenzake kulipotokea mzozo kuhusu pato la samaki.
Kufikia sasa mwili wa mvuvi huyo haujapatikana.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Mombasa inaongoza kwa maambukizi ya MPOX nchini

Wizara ya afya nchini imesema kaunti ya Mombasa inaongoza kwa visa vya maambukizi ya ugonjwa wa Mpox.
Kwa mujibu wa mkurugenzi mkuu wa idara ya afya nchini Daktari Patrick Amoth, kaunti ya Mombasa imerekodi visa 139 kati ya visa 300 vilivyoripotiwa na wizara hiyo.
Amoth alidokeza kuwa serikali itatangaza siku maalum ya kutoa chanjo ya kudhibiti msambao wa ugonjwa huo wakishirikiana na shirika la afya ulimwenguni WHO.
Mkurugenzi huyo vile vile alimesema zoezi hilo litaambatana na hamasa kwa wananchi kuhusu namna ya kujikinga na maambukizi zaidi.
“Kwa wakati huu Mombasa ndio inaongoza kwa idadi ya visa 139 kwa hivyo tuchuke tahadhari kuhakikisha kwamba tunazuia maambukizi, na tunafanya mpango pamoja na shirika la afya duniani WHO, hapa tutakuja na mpango wa chanjo na ikifika huo wakati tunaomba watu wajitokeze wapate chanjo ili wapate kinga”,alisema Daktari Amoth.
Wakati huo huo Amoth aliokeza kuwa uchunguzi wa vifo vya watu wanne walioaga dunia wiki chache zilizopita huko Migadini, eneo bunge la Changamwe kaunti ya Mombasa umebaini walifariki kutokana na magonjwa mengine na wala sio maambukizi ya ugonjwa wa MPOX kama ilivyodhaniwa na wakaazi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu.