News
IEBC kufafanua mda mwafaka wa kampeni za uchaguzi

Mwenyekiti wa Tume ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC Erastus Ethekon ametangaza mipango ya kushauriana na mwanasheria mkuu wa serikali ya Kenya ili kufafanua kipi kinajumuisha kampeni ya mapema kabla ya Uchaguzi mkuu wa 2027.
Akizungumza jijini Nairobi, Ethekon alisema Tume ya IEBC ina nia ya kufafanua mda wa kampeni na kuangazia masuala kuhusu utayarishaji wa uchaguzi kabla ya wakati.
“Nchini Kenya, kila siku, kila saa inafanana na msimu wa kampeni. Iwapo mtu atahudhuria hafla ya mazishi anazungumzia uchaguzi, hivyo inamaanisha ni kampeni? aliuliza Ethekon.
Mwenyekiti huyo mpya wa IEBC alisema ni vigumu kuangazia mda mwafaka wa kampeni ya uchaguzi unapofaa kuanza.
Kuhusu suala la uchaguzi ndogo nchini, Ethekon alihakikishia wakenya kwamba ratiba kamili itatolewa mara tu michakato ya ndani ya tume hiyo itakapokamilika.
“Kuhusu suala la muda wa uchaguzi mdogo, tutakuwa tukitangaza ratiba mara baada ya kamati ya uendeshaji kutoa taarifa zote kisha tutawasilisha maelezo. Kuweni na subira tutashughulikia ratiba,” alisema Mwenyekiti huyo.
Vile vile alikiri changamoto za kiutendaji zinazokabili tume hiyo japo akahakikishia wakenya kuwa hatua zinachukuliwa ili kuzitatua.
“Kulikuwa na baadhi ya mambo ambayo tuko nje ya udhibiti wetu, lakini tunafanya kazi usiku kucha kutekeleza shughuli hizi zote kama wale ambao wamepewa jukumu la kusimamia uchaguzi,” aliongeza Ethekon.
Hapo awali, Ethekon alisema uchaguzi mkuu wa 2027 utakuwa huru na wa haki, na kuondoa uwezekano wa wizi wa kura.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Mabadiliko ya tabianchi yatajwa kuchangia mapato duni ya samaki, Lamu

Wadau katika sekta ya mazingira kaunti ya Lamu wanasema mabadiliko ya hali ya anga yanayoshuhudiwa sawa na ujenzi wa bandari ya Lamu kumechangia mapato ya samaki kupungua katika bahari hindi.
Mahmoud Yusuf ambaye ni mwanazingira alisema zana za kizamani wanazotumia wavuvi kuvua samaki pia zinachangia mapato duni ya samaki.
Yusuf alisema tangu ujenzi huo wa bandari uanze, maji ya bahari chini yamekuwa na matope kutokana na kuchimbwa na kufukuliwa kwa bahari, hali iliyochangia samaki kutorokea bahari kuu.
Mwanamazingira huyo aliitaka serikali kuwapa wavuvi vifaa vya kisasa vya uvuvi sawa na meli za uvuvi zitakazowawezesha kufika maji makuu, baada ya bandari ya ndani kuharibika.
Taarifa ya Joseph Jira.
News
Gachagua atangaza azma ya kuwania urais 2027

Kinara wa chama cha DCP Rigathi Gachagua ametangaza nia ya kuwania wadhfa wa urais mwaka 2027 akilenga kumg’oa rais William Ruto mamlakani.
Gachagua amekuwa akifanya ziara katika eneo la mlima kenya pamoja na viongozi wa chama chake akitumia mikutano ya barabarani kutangaza azma yake ya kuwania urais.
Kulingana na Gachagua serikali ya sasa inatumia mikutano ya ikulu kuendeleza vitendo vya ufisadi, na ameahidi kuwa akichaguliwa atakomesha matumizi mabaya ya fedha za umma.
Katika ziara hiyo viongozi wa chama chake walieza kuwa Gachagua ndiye mgombea anayefaa kupeperusha bendera ya upinzani, wakidai eneo la mlima kenya limejiondoa katika uungwaji mkono wa serikali ya sasa.
Taarifa ya Joseph Jira.