News
Hatma ya Gavana Mutai kuwekwa wazi na bunge la Seneti

Kesi inayosubiriwa kwa hamu ya kumuondoa madarakani Gavana wa Kericho Erick Mutai, imeanza rasmi katika bunge la Seneti.
Kulingana na ratiba rasmi iliyotolewa na Karani wa bunge la Seneti, kikao kilitarajiwa kuanza saa tatu asubuhi kwa mkutano wa faraghani wa maandalizi ya maseneta.
Kikao hiki cha ndani kililenga kuwapa wanachama nafasi ya kupitia kanuni za mashauri na mwelekeo wa kesi kabla ya ufunguzi rasmi.
Kikao cha hadhara kilitarajiwa kuanza saa nne asubuhi kwa taratibu za awali, ikiwemo kusomwa kwa wajibu wa Seneti na utambulisho wa pande zote mbili.
Wajumbe wa Bunge la kaunti ya Kericho waliowasilisha mashtaka hayo walitambulishwa rasmi pamoja na mawakili wao.
Gavana Mutai na timu yake ya utetezi pia walitarajiwa kuwasilishwa mbele ya Baraza.
Saa tano asubuhi, mashtaka dhidi ya gavana yalisomwa, yakitoa mwelekeo wa mijadala ya siku.
Baada ya hapo kulifanyika kikao cha dakika 90 cha kushughulikia maswali na hoja za awali kabla ya kuanza kwa usikilizaji wa ushahidi.
Baada ya mapumziko ya chakula cha mchana kuanzia saa saba mchana hadi saa nane na nusu alasiri, pande zote zilipewa muda wa kutoa kauli za ufunguzi.
Bunge la kaunti, kupitia wawakilishi wake lilipewa dakika 30 kueleza hoja zake kisha timu ya utetezi ya Gavana Mutai pia iliwekewa muda wa dakika 30 kujibu.
Sehemu kubwa ya kikao cha alasiri, kuanzia saa tisa na nusu hadi saa kumi na mbili na nusu jioni, ililenga uwasilishaji wa ushahidi.
Bunge la kaunti lilitengewa muda wa saa tatu kuwasilisha mashahidi wake na kufanya upekuzi wa mahojiano.
Upande wa gavana ulipewa muda wa saa mbili kuuliza maswali ya majibu kwa mashahidi hao.
Kesi ya Gavana Mutai imevutia hisia kote nchini, si Kericho pekee, kwani itajaribu nguvu za kisiasa kati ya mabunge ya kaunti na magavana, huku ikisisitiza jukumu la kikatiba la Seneti kama msuluhishi wa migogoro ya kuondoa viongozi madarakani.
Bunge la kaunti ya Kericho limewakilishwa na mawakili 12 wakiongozwa na Elisha Ongoya. Wanaosaidia ni Kimutai Bosek, Sharon Mibey, Elias Mutuma, Hillary Kiplangat, Brian Langat, Geoffrey Langat na Victor Kibet.
Wengine ni Evans Kiplangat, Elvis Kipkorir, Joel Wakhungu na Vincent Kipronoh.
Orodha iliyowasilishwa Seneti inajumuisha maafisa wanne wa kisheria, akiwemo Brian Maingi, Ian Kiplangat, Mitchel Mutuma na Japhet Koech.
Mutai, kwa upande wake, anawakilishwa na mawakili sita wakiongozwa na Katwa Kigen, Peter Wanyama, Rose Thiong’o, Doris Ng’eno, Joash Mitei na Evanson Kirui.
Wakati wa kutoa hotuba ya utangulizi, Wakili mkuu wa Bunge la kaunti, Elisha Ongoya, aliomba kuruhusiwa kuwasilisha ushahidi mpya, jambo lililopingwa vikali na timu ya utetezi ya Mutai.
“Mheshimiwa Spika, tunapinga vikali jaribio la kuwasilisha ushahidi mpya kwa wakati huu kwa sababu hatutakuwa na nafasi ya kuupitia na kujibu kwa kuzingatia kuwa leo tumepangiwa usikilizaji wa kesi,” alisema Kigen.
Nyaraka hizo zilijumuisha vocha za malipo za idara ya kilimo, ardhi na mipango ya miji ambazo hazikuwa zimewasilishwa awali.
Pia zilikuwa na taarifa za mashahidi, barua za uhamisho wa wafanyakazi, taarifa za M-Pesa, ripoti ya kamati ya ADHOC ya kazi mtaani, rekodi za malipo na barua za kufutwa kazi miongoni mwa nyingine.
Hata hivyo, katika uamuzi wake Spika Amason Kingi aliruhusu nyaraka hizo kuwasilishwa.
“Niliposikia maelezo ya wakili wa bunge la kaunti, alibainisha kwamba nyaraka hizo ziliachwa kwa bahati mbaya wakati wa kuandaa, hazileti ushahidi mpya… kwa hivyo, kwa mujibu wa kanuni ya 30 ya taratibu za kesi, nitaruhusu nyaraka hizo kuwasilishwa,” alisema Kingi.
Taarifa ya Elizabeth Mwende
News
Mahakama ya Malindi yawaachilia washukiwa 3 wa kesi ya Kwa Binzaro

Mahakama Kuu ya Malindi imewaachilia washukiwa watatu wanaohusishwa na kesi ya mauaji ya halaki ya watu katika kijiji cha Kwa Binzaro eneo bunge la Magarini kaunti ya Kilifi.
Hakimu wa Mahakama hiyo Joy Wesonga aliagiza kuachiliwa huru kwa Safari Kenga Nzai, Gona Charo Kalama na Kahindi Kazungu Garama wote wakiwa wakaazi wa kijiji hicho cha Kwa Binzaro.
Watatu hao walikuwa wamekamatwa baada ya kudaiwa kuuza shamba la ekari tano kwa mshukuwa mkuu wa mauaji ya watu katika kijiji cha Kwa Binzaro Sherleen Temba Anido.
Hakimu Wesonga aliwaagiza washukiwa hao kuhakikisha wanasalimisha nakala za vitambulisha vyao vya kitaifa kwa idara husika, kuripoti kwa Naibu Chifu wa eneo hilo mara mbili kwa wiki pamoja na kujisalimisha kwa maafisa wa upelelezi wa kesi hiyo mara moja kila baada ya wiki mbili.

Miili iliyofukuliwa katika kijiji cha Kwa Binzaro
Wakati huo huo upande wa mashtaka ukiongozwa na Naibu mkurugenzi wa mashtaka ya umma Jamie Yamina, uliomba kuwasilisha watu wengine wanne Mahakamani ikiwemo Jairus Otieno na mkewe Lilian Akinyi, Kahonzi Katana Karisa na Loise Zawadi waliojionda kama washukiwa na kugeuka kuwa mashahidi wa serikali.
Upande wa mashtaka pia uliaka kupewa siku 60 zaidi kuendelea kuzuiliwa kwa washukiwa wakuu Sherleen Temba Anido, James Kahindi Kazungu, Thomas Mukunwe na Kahidi Kazungu Garama katika kituo cha polisi cha Ngerenya, Kilifi, Watamu na Kijipwa ili kukamilisha uchunguzi wao kwani wanne hao wanakabiliwa na mashtaka ya itikadi kali, ugaidi, kujihusisha na uhalifu na kupanga mauaji.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Chrispus aomba msahama bunge la kaunti ya Taita Taveta

Mwakilishi wadi ya Bomani mjini Taveta kaunti ya Taita Taveta Chrispus Tondoo ameliomba bunge la kaunti hiyo msamaha kutokana na matamshi aliyoyatoa hapo awali akikashifu bunge hilo kwa madai ya kushamiri kwa visa vya ufisadi na utepetevu.
Tondoo akiomba msamaha katika bunge hilo alisema alitambua athari zilizosababishwa na matamshi hayo kwa wenyeji wa kaunti hiyo na bunge hilo, hali ambayo imemfanya kuchukua hatua hiyo ya kuomba msamaha.
Aidha Tondoo aliahidi kuliheshimu bunge hilo kwa mujibu wa kanuni na Sheria za bunge la kaunti ya Taita Taveta.
‘’Naomba msamaha kutokana na matamshi ambayo niliyatoa tarehe 2 na tarehe 3 mwezi wa Juni mwaka huu wa 2025 kwani hayakuwa yenye heshima kwa wenyeji wa Taita Taveta na bunge la kaunti’’, alisema Tondoo.
Tondoo alikuwa Mwakikishi wa wadi wa pili kuomba msamaha baada ya Mwakilishi wa wadi ya Kaloleni mjini Voi Ahmed Azari kuchukua hatua hiyo mwezi mmoja uliyopita.
Haya yalijiri baada ya kaimu spika wa bunge hilo Anselim Mwadime kuapa kuwachulia hatua za kisheria wanachama wanne wa bunge hilo, wawili wakiwa ni Tondoo na Azari ambayo tayari wameomba msamaha huku wawili wakiwa wamesalia bila kuomba msamaha.
Taarifa ya Janet Mumbi
-
Entertainment10 hours ago
Mbilia Bel Anusurika Kwenye Ajali ya Barabarani – Kinshasa
-
Entertainment22 hours ago
#COCODRIVE: Crack Sound Siyo Mashine, Ni Vichwa – J Crack Asema Baada ya Kuibiwa Vyombo Studioni Kwake
-
International News19 hours ago
Mgombea wa urais wa ACT wazalendo Luhaga Mpina, arejeshwa debeni