News
Gachagua amtaka Rais Ruto kuangazia usalama wa Mandera

Kinara wa chama cha DCP Rigathi Gachagua amekosoa serikali kwa kusalia kimya kuhusiana na madai ya uwepo wa jeshi la Jubaland hapa nchini.
Naibu huyo wa rais wa zamani sasa anamtaka rais William Ruto kutoa amri ya kufurusha jeshi hilo kutoka eneo la Mandera na kurejesha hali ya usalama.
Akizungumza katika ibada ya jumapili katika kanisa la PCEA Ongata Rongai, Agosti 31, 2025, Gachagua alikashifu uvamizi huo akisema uwepo wa jeshi hilo utasambaratisha usalama mjini humo.
Vile vile alimlaumu rais Ruto akisema anachukua mda kukabiliana na ufisadi nchini suala ambalo linaendelea kurejesha nyuma maendeleo ya taifa.
“Nakusema wabunge wote kazi yao ni kuchukua hongo na hatakubali hiyo maneno, nikafurahi sana kama ameamua hivyo kwa sababu yeye mwenyewe ndiye mwenye kuhonga wabunge, nilifikiri hayo maneno ya hongo yamefika mwisho lakini sasa yameongezeka, pale ikulu ndio mahali kwa hongo na ufisadi”,alidai Gachagua
Wakati huo huo waziri wa usalama wa zamani Fred Matiang’i aliyeandamana na Gachagua aliomba wakenya kuwaunga mkono wanaoendeleza kamapeni za kumuondoa rais William Ruto mamlakani.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Mahakama ya Kilifi imetoa hukumu kwa wanaume 6 wanaokabiliwa na mashtaka ya unajisi

Mahakama ya Kilifi imetoa hukumu kwa wanaume 6 wanaokabiliwa na mashtaka ya unajisi.
Hakimu wa Mahakama hiyo Ivy Wasike alimhukumu Lucky Munga na Hassan Daniel kifungo cha miaka 30 gerezani baada ya Mahakama kubaini kwamba walihusika kwa kuwatendea unyama watoto wa umri wa miaka 13 na 15.
Safari Karisa Lewa alihukumiwa kifungo cha miaka 15 gerezani kwa kumnajisi mtoto wake mwenyewe wa umri wa miaka 14 huku Eric Ruwa na Lucky Katana Kenga wakihukumiwa kifungo cha miaka 6 gerezani kwa kosa sawa na hilo.
Hata hivyo Mahakama hiyo ilimhukumu kifungo cha miaka 3 Kithi Kombe kutokana na kesi hiyo kwa mtoto wa miaka 15, japo baadaye Mahakama ikabaini kwamba mshukiwa sio baba halali wa mtoto aliyezaliwa baada ya Kithi kumnajisi mtoto huyo.
Akizungumza wakati wa vikao vya Mahakama baada ya kutoa hukumu hizo, Hakimu Wasike alisema Mahakama umezingatia ushahidi uliyotolewa Mahakamani huku akiwarai wananchi kujitenga na visawishi vibaya ili kuepuka mkono wa sheria.
Hakimu Wasike alihoji kwamba washtakiwa wa haki ya kukata rufaa dhidi ya uamuzi wa Mahakama lakini kwa kuzingatia taratibu zote za Mahakama na sheria.
Taarifa ya Teclar Yeri
News
Thoya: Serikali kuu iongeze mgao wa fedha kwa sekta ya Afya

Naibu gavana wa kaunti ya Mombasa Francis Thoya ametoa changamoto kwa serikali kuu kuongeza mgao wa fedha ili kufanikisha utaoji wa huduma za afya.
Akizungumza katika kaunti hiyo, Thoya alisema kuwa huduma nyingi za afya katika kaunti hiyo ya Mombasa zinakabiliwa na changamoto ya raslimali ndogo hali ambayo inakwamisha juhudi za kuwahudumia wananchi ipasavyo.
Thoya pia alitaka serikali kuhakikisha inaharakisha kuajiri wahudumu zaidi wa afya ili wenyeji wa Mombasa waweze kupata huduma bora za matibabu bila changamoto zozote.
Aidha, Thoya alisema kwamba hali ya uhaba wa wahudumu wa afya ni changamoto kuu ambayo inazuia utoaji wa huduma bora za matibabu hali inayowafanya wale wachache waliopo kufanya kazi katika mazingira magumu.
Taarifa ya Janet Mumbi