International News
Chanjo dhidi ya kisonono kutolewa karibuni

Chanjo za maradhi ya kisonono zitapatikana kwa wingi kuanzia Agosti 11, 2025 katika kliniki za afya Uingereza, katika jitihada za kukabiliana na viwango vya kuvunja rekodi vya maambukizi.
Awamu ya kwanza ya chanjo hizo itatolewa kwa wale walio katika hatari zaidi – wengi wao wakiwa wapenzi wa jinsia moja na wanaume wa jinsia mbili ambao wana historia ya wapenzi wengi wa ngono au magonjwa ya zinaa.
Huduma ya kitaifa ya afya Uingereza (NHS) ilisema hatua ya kusambaza chanzo hizo ni ya kwanza duniani, na inatabiriwa kuwa inaweza kuzuia visa vingi kama 100,000, na kunauwezekano wa NHS kuokoa karibu pauni milioni 8 katika muongo ujao.
Terrence Higgins Trust, ambao walifanya kampeni ya chanjo hiyo kuanzishwa nchini Uingereza, waliambia shirika la habari la BBC kuwa ni “ushindi mkubwa” kwa afya ya kijamii.
Kisonono ni maambukizi ya bakteria ambayo hupitishwa kupitia ngono isiyo salama.
Dalili zinaweza kujumuisha maumivu, kutokwa kwa maji yasiyo ya kawaida, kuvimba kwa sehemu za siri na utasa, lakini katika hali zingine kunaweza kuwa hakuna dalili kabisa.
NHS inasema inaweza kuepukwa kwa matumizi sahihi ya mipira ya kinga na kwa kukubali chanjo kama itatolewa.
Taarifa ya Joseph Jira
International News
Mgombea wa urais wa ACT wazalendo Luhaga Mpina, arejeshwa debeni

Mahakama kuu nchini Tanzania imemrejesha kwenye debe mgombea urais wa chama cha upinzani ACT wazalendo, Luhaga Mpina na kupindua maamuzi yaliyotolewa na tume ya uchaguzi nchini humo INEC.
Hii inamaana tume ya INEC ni lazima imjumuishe Mpina katika orodha ya majina ya watakaopigiwa kura, hatua itakayosababisha upinzani kwenye uchaguzi huo mkuu.
Hatua hii sasa inampa Mpina fursa ya kuanzisha kampeni za kutaka kumbandua mamlakani rais Samia Suluhu Hassan katika uchaguzi mkuu utakaofanyika Octoba 29 mwaka 2025.
Kampeni za uchaguzi tayari zinaendelea nchini humo.
INEC ilimzuia mpina kugombe wadhifa wa urais mwezi Agosti 26, 2025 ikidai chama cha ACT Wazalendo kilikiuka taratibu za chama kwa kumsimamisha Mpina kuwania wadhifa huo.
Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan akiwa katika kampeni za uchaguzi mkuu.
Katika uamuzi uliotolewa Alhamisi mwezi Septemba 11, 2025, jopo la majaji watatu mjini Dodoma liliagiza INEC kumuidhinisha Mpina kama mgombea wa urais.
Anatarajiwa kujumuika na wagombea wengine 16 kutoka vyama vidogo vya kisiasa katika mapambano hayo ya kuwania urais, ambao wote wanania ya kung’atua rais wa sasa Samia Suluhu Hassan mamlakani.
Chama cha Chadema kilizuiwa kugombea katika uchaguzi huo baada ya kiongozi wake Tundu Lissu kufunguliwa mashtaka ya uhaini.
Kiongozi wa upinzani wa Chadema Tundu Lissu akiwa mahakamani.
Rais Samia Suluhu Hassan alichukua hatamu za uongozi kama rais baada ya kifo cha John Pombe Magufuli mwaka 2021.
Taarifa ya Joseph Jira.
International News
Ghasia zatanda nchini Nepal licha ya marufuku ya kutotoka nje.

Marufuku ya kutotoka nje inaendelea kukiukwa nchini Nepal ambako ghasia za uharibifu wa mali na umwagikaji wa damu zinaendelea.
Serikali ya Waziri mkuu KP Sharma Oli, ilipinduliwa ndani ya masaa 48 baada ya kuzuka kwa maandamano hayo, ambapo waandamanaji waliokuwa na ghadhabu walivamia na kuteketeza makaazi ya Waziri mkuu Oli, pamoja na bunge la nchi hiyo.
Licha ya jeshi la nchi hiyo kutanganza hali ya tahadhari na marufuku ya kutotoka nje, Waandamanaji hao waliendelea kukiuka marufuku hiyo na kumiminika katika barabara za mji mkuu wa Kathmandu, huku wakiwashambulia maafisa wa usalama, lakini pia kulenga makaazi ya maafisa wakuu wa serikali, wakiwemo Wabunge na mawaziri huku wakiteketeza majumba na magari yao.
Kulingana na taarifa za maafisa wa usalama nchini humo, waandamanaji hao pia walivamia magereza na kuwaachilia huru jumla ya wafungwa elfu 13 katika kipindi cha wiki nzima ya maandamano.
Chanzo cha maandamano hayo yaliyoanzishwa na kizazi cha sasa cha Gen Z mapema wiki hii ni kukithiri kwa ufisadi serikalini mbali na sera duni zinazolenga kukandamiza vijana katika matumizi ya mitandao ya jamii.
Taarifa ya Eric Ponda