News
Bunge la kaunti ya Kilifi kujadili hatma ya Spika Mwambire

Mswada unaolenga kumuondoa Mamlakani Spika wa bunge la kaunti ya Kilifi Teddy Mwambire, uliwasilishwa kwa Karani wa bunge hilo Micheal Ngala.
Kulingana na utaratibu wa mabunge ya kaunti, Mswada uliowasilishwa na Mwakilishi wadi wa Tezo Thomas Chengo, utapelekwa kwa ofisi ya Spika ambaye kwa mujibu wa Sheria atauwasilisha kwa kamati ya shughuli za bunge hilo kabla ya kuwasilishwa bungeni ili kujadiliwa.
Hii itakuwa mara ya kwanza kwa bunge hilo kujadili hatma ya Spika Teddy Mwambire.
Miongoni mwa madai yaliyoibuliwa dhidi ya Spika Mwambire, ni pamoja na kuendelea kuhudumu katika wadhfa wake akiwa bado ni Mwenyekiti wa Chama cha ODM kaunti ya Kilifi, kuhujumu serikali ya Gavana Gideon Mungaro katika utekelezwaji wa miradi ya maendeleo miongoni mwa madai mwengine.
Kumekuwa na mpasuko mkubwa katika bunge la kaunti ya Kilifi baina ya Wawakilishi wadi wanaoegemea upande wa Gavana Mungaro na wale wanaokosoa serikali yake.

Picha kwa hisani: Bunge la kaunti ya Kilifi
Akizungumza na CocoFm, Spika Teddy Mwambire alithibitisha kuwasilishwa kwa mswada huu mbele ya Karani wa bunge hilo, japo mswada huo haujawasilishwa ofisini mwake huku akihoji kwamba shtuma hizo dhidi yake hazina msingi wowote.
Hata hivyo alisema atafuata sheria kuhakikisha kwamba mswada huo unazingatia vigezo vyote vya kisheria vya kuwasilisha mswada bungeni na kujadiliwa kikamilifu.
Itakumbukwa kwamba mwezi uliopita vurugu zilishuhudiwa wakati Wawakilishi wadi wakijadili bajeti ya kaunti hali iliyosababisha kushambuliwa kwa Mwakilishi wadi mteule Elina Mapenzi na wenzake wawili Ibrahim Matumbo (Watamu) na Twaher Abdulkarim (Sheila).
Vurugu hizo zilishuhudiwa wakati baadhi ya Wawakikishi wadi wanaoegemea mrengo wa Gavana Mungaro kususia vikao vya bunge vilivyotarajiwa kumhoji Waziri wa Afya kaunti ya Kilifi Peter Mworogo na Katibu wake David Mulewa kwa madai ya usimamizi mbaya wa Wizara ya Afya kaunti ya Kilifi.
Taarifa ya Eric Ponda
News
Nassir: Kaunti ya Mombasa wametenga milioni 80 za Afya

Gavana wa kaunti ya Mombasa, Abdulswamad Shariff Nassir amesema serikali ya kaunti ya Mombasa wametenga shilingi milioni 80 kugharamia sehemu ya matibabu ya wakaazi ambao hutibiwa katika hospitali za Level 4 na Level 5.
Akizungumza katika kaunti ya Mombasa, Nassir alisema fedha hizo zitagharamia bima ya afya ya SHA ya wenyeji wa kaunti hiyo kwa muda wa mwaka mmoja.
Gavana Nassir pia alisema fedha hizo zitagharamia madeni ya ziada ya matibabu kwa watoto wa chini ya umri wa miaka 5 ambao wanatibiwa kupitia bima hiyo ya SHA.
“Tumeweka dawati maalum na fedha kuweza kuwalipia ile amana ambayo ilikuwa inalipiwa SHA. Na itakuwa sio ya Public health pekee lakini kando na Public health mnakuwa mumelipiwa kwa mwaka mzima’’, alisema gavana Nassir
Wakati huo huo Gavana Nassir alieleza matumaini kwamba mpango huo utasaidia kwa asilimia kubwa kuimarisha huduma za matibabu kwa wenyeji wa kaunti hiyo.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Chibule, apendekeza adhabu kali kwa wanaoendeleza dhulma za kijinsia

Naibu gavana kaunti ya Kilifi Flora Mbetsa Chibule, amependekeza adhabu kali kwa watu wanaotekeleza visa vya dhulma za kijinsia katika jamii.
Chibule alisema visa vya dhulma za kijinsi dhidi ya watoto vimekithiri katika jamii hasa kaunti ya Kilifi, akiahidi ushirikiano wa hali ya juu na wadau mbalimbali ili kukomesha visa hivyo.
Akizungumza wakati wa maadhimisho ya hamasa kuhusu dhulma za kijinsia katika uwanja wa Bofa Youth mjini Kilifi, Chibule alisema ili kufanikisha ndoto ya mtoto wa kike ni lazima haki zao za kimsingi zilindwe.
“Kwa ambao wanadhulumu mtoto wa kike na kiume, kwa wale ambao wanaingia misuli kwa misuli wanafaa kuwekwa gerezani kabisa”, alisema Chibule.

Wanaharakati wa kijamii wapinga unyanyasaji wa kijinsi, Kilifi
Kwa upande wake Mwakilishi wa kike kaunti ya Kilifi Getrude Mbeyu aliyeandaa hafla hiyo kupitia hazina ya kitaifa ya NGAAF na kutoa hundi ya kima cha shilingi milioni 1.6 kwa makundi 14, alisisitiza hamasa zaidi kwa jamii kuhusu jinsi ya kukomesha visa hivyo.
“Ni jukumu letu la kuwaeleza hawa watu watambua jinsi ya kuripoti hizi kesi, yani kwa mfano umedhulumiwa ni wapi pa kuanzia na hatua hii itakomesha hizi visa”, alisema Mbeyu.
Naye Mzee wa mataa wa Kiwandani mjini Kilifi Elina Nyevu alisema visa vya dhulma za kimapenzi vimekithiri mno katika mtaa huo, akipendekeza hamasa zaidi kwa jamii.
“Hapa kwetu Kiwandani visa vya dhulma za kijinsia ni vingi sana, kuna ulevi na ukosefu wa ajira ambao umechangia utumiaji wa Mihadarati na unyanyasaji wa watoto wadogo kimapenzi, alisema Elina.
Hata hivyo katika halfa hiyo baadhi ya watoto waliopitia madhila hayo hasa ubakaji wameelezea masaibu waliopitia japo haki yao kupitia idara ya usalama walikosa kufaulu.
Taarifa ya Lolani Kalu.