News
Watu watatu wakamatwa katika Mahakama ya Milimani

Watu watatu wanaodaiwa kuwa wafanyakazi wa kaunti ya Trans Nzoia wamekamatwa na maafisa wa polisi waliokuwa wamevalia sare baada ya kusikiza kesi inayomkabili gavana wa kaunti hiyo George Natembeya katika Mahakama ya Milimani jijini Nairobi.
Watatu hao walikamtwa mda mfupi baada ya Jaji Zipporah Gichana, kuagiza upande wa mashtaka kuwasilisha ushahidi dhidi ya kesi ya ufisadi inayomkabili gavana huyo.
Agizo hilo lilifuata tamko la upande wa mashtaka kwamba ilifeli kufuta agizo la awali la Mahakama la kuwasilisha ushahidi.
“Nyaraka na taarifa hizo zilipaswa kuwa zimetolewa kufikia sasa, kwa hiyo ninaelekeza upande wa mashtaka kufuata maagizo ya awali”, aliagiza Jaji Gichana.
Upande wa mashtaka uliomba mda wa wiki mbili zaidi ili kutii maagizo ya awali ya kuwasilisha ushahidi wa nyaraka.
“Hati nyingi zinapatikana kutoka kaunti ya Trans Nzoia na tumeshindwa kuzipata, tunaomba wiki mbili za ziada ili kutii,” Wakili wa Serikali Victor Awiti aliwasilisha.
Hata hivyo, upande wa utetezi ulipinga ombi hilo, ukisema ni sawa na matumizi mabaya ya mchakato wa Mahakama.
Upande wa mashtaka uliamriwa kufichua nyenzo zote husika kabla ya Juni 16 kesi hiyo itakapotajwa.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Wahudumu wa afya Lamu watishia kuishtaki serikali ya kaunti hiyo

Wahudumu wa Afya kaunti ya Lamu wametishia kuelekea Mahakamani kuishtaki serikali ya kaunti hiyo kwa kukaidi kutekeleza matakwa yao.
Wahudumu hao waliishtumu serikali ya kaunti ya Lamu kwa kupuuza matakwa yao na badala yake kutumia vitisho ili kuwashurutisha kurejea kazini.
Kulingana na viongozi wa wahudumu hao, licha ya mgomo wao kuendelea kwa zaidi ya wiki mbili serikali ya kaunti hiyo imekataa kata kuandaa vikao vya kusuluhisha malalamishi yao.
Baadhi ya changamoto wanazolalamikia ni pamoja na kufanya kazi kwa zaidi ya miaka 10 bila ya kupandishwa vyeo, kupuuzwa kwa mkataba wa makubaliano ya nyongeza ya mishahara, kunyimwa kwa mishahara kwa baadhi ya wahudumu hao miongoni mwa matakwa mengine.
“Mkiendelea kutufinyilia itabidi tufuate njia ya sheria kwa sababu tunajua tunalilia haki yetu, haiwezekani serikali ya kaunti inashindwa kutupandisha vyeo ilhali tumefanya kazi kwa miaka 15 sasa, hatuwezi kuendelea kufanya kazi katika mazingira duni na pia mkataba wa makubaliano kuhusu nyongeza ya mishahara sharti itekelezwe” walisisitiza viongozi hao.
Wakati uo huo serikali ya kaunti ya Lamu imejibu malimishi yao kupitia barua na kutangaza kuwa mgomu huo ni kinyume cha seria na kuwataka wahudumu hao kurejea kazini mara moja.
Taarifa ya Elizabeth Mwende
News
Rais Ruto atuma KDF kusimamia ujenzi wa hospitali nchini

Rais William Ruto ametuma jeshi la KDF kusimamia ujenzi wa vituo vya afya zaidi ya 75 kote nchini katika juhudi za kuhakikisha ujenzi unakamilika kwa haraka.
Akizungumza katika kaunti ya Narok wakati wa uzinduzi wa hospitali ya Sogoo Level 4, waziri wa ulinzi Patrick Mariru alifichua kuwa ujenzi wa hospitali hiyo yenye mamlaka kamili itakamilika baada ya mda wa miezi 11.
Ujenzi wa hospitali ya Sogoo Level 4 ulivutia rais Ruto alipozuru eneo hilo mwezi mei mwaka 2025, jambo lililomfanya kuagiza KDF kuipandisha hadhi.
Mariru hata hivyo alishikilia kuwa wafanyikazi wote wasio na ujuzi watatolewa kutoka kwa jamii.
“Jeshi litamsimamia mkandarasi. Hilo liwe wazi, kazi yote itafanywa na vijana wa Sogoo. Tutaweka maafisa wawili na kila jioni watanipa ripoti ya maendeleo,” alisema Mariru.
“Tuna zaidi ya miradi 75 tunayosimamia na sio kwamba tunabadilisha wakala wa serikali tunataka tu kushirikiana na ofisi tofauti miongoni mwao wizara za afya na michezo.”
Taarifa ya Joseph Jira