Entertainment
Wakili George Kithi na Mbosso Khan Waanzisha Ushirikiano wa Kimkakati kuinua Muziki wa Africa Mashariki

Wakili na mwanasiasa maarufu kutoka Kilifi, George Kithi, ameweka wazi azma yake ya kuendelea kukuza sekta ya muziki na ubunifu katika ukanda wa Pwani ya Kenya kwa njia za kimkakati na kimataifa.
Wakili Kithi aliyasema haya Jijini Dar es salaam Tanzania alipokutana na kufanya mazungumzo na Mwanamuziki nyota wa Bongo flavor, Mbosso Khan, katika mazungumzo yaliyolenga kuleta mageuzi ya kweli katika Sekta ya muziki wa Pwani na Kenya kwa ujumla.
“Nilifanya kikao chenye mafanikio na msanii maarufu kutoka Tanzania, Mbosso Khan, jijini Dar es Salaam, ambapo tulijadili mbinu za kimkakati katika kuboresha muziki na kukuza wasanii hususan kutoka Kaunti ya Kilifi na eneo zima la Pwani.,” Kithi alisema.
Mkutano huu ni hatua Moja wapo ya kuendeleza uhusiano kati ya Kiongozi huyo na Mwanamuziki Mbosso baada ya ziara ya Mwanamuziki huyo Mjini Kilifi mnamo Desemba 31, 2023, ilitia fora na kuweka Msingi mahusiano bora.
Ziara ya Mbosso mjini Kilifi ilizua gumzo Kwa jinsi ilivyoshabikiwa kufuatia show yake ya kukata na shoka katika eneo la Old Fery Kilifi, na kuwavutia maelfu ya mashabiki.
Tukio hilo liliangazia kiwango cha hamasa na kiu ya burudani ambayo Pwani inayo na huenda ndicho Kithi anataka kuendeleza kwa vitendo.
Miongoni mwa mambo wanayolengwa katika usjirikiano huu pia ni kuleta mshikamano na ushirikiano wa karibu baina ya wasanii wa Africa Mashariki Kwa lengo ya kukuza sekta na muziki Kwa kutumia teknolojia ya kisasa, vifaa bora, na ubadilishanaji wa maarifa kutoka pande zote mbili za mipaka.
Zaidi ya hayo, walitathmini njia za kuwasaidia wasanii kibiashara kwa kuwapatia mafunzo kuhusu jinsi ya kutumia teknolojia kupata mapato kupitia majukwaa mbali mbali ya kidijitali mfano mapato ya muziki kupitia mtandaoni (streaming royalties), uuzaji wa maudhui (content monetization), ushirikiano na chapa mbalimbali (brand partnerships), pamoja na mbinu za kujenga hadhira kupitia mitandao ya kijamii. Lengo kuu likiwa ni kuhakikisha kuwa kipaji kinaweza kubadilishwa kuwa taaluma, na muziki kuwa chanzo halisi cha mapato.
Kwa mujibu wa Kithi, mafunzo haya yatasaidia sana kubadilisha fikra za muziki kuwa kipaji tu, hadi kuwa chanzo cha mapato na ajirankwa vijana wa Pwani.
Huenda hii ikawa hatua kubwa kuelekea kuinua uchumi wa kijamii kupitia sekta ya ubunifu.
“Maarifa katika eneo hili yanaweza kubadilisha ari kuwa taaluma na kipaji kuwa chanzo cha mapato,” alisema Kithi.
“Tumejikita katika kukuza vipaji, kujenga ushirikiano, na kuunda fursa zitakazoinua vijana wetu na kuiweka kanda yetu kwenye ramani ya dunia” aliongezea.
George Kithi ametangaza kuwa kuna mengine mengi yanakuja, ikiwa ni pamoja na miradi mipya ya ushirikiano, mafunzo ya ubunifu, na kuibua vipaji vijijini.
Entertainment
Chris Brown Akanusha Shtaka la Kumshambulia Producer kwa Chupa

Msanii nyota wa Marekani, Chris Brown, amekana mashtaka mawili mahakamani yanayohusiana na madai ya shambulio kwa kutumia chupa katika kilabu cha usiku jijini London miaka miwili iliyopita.
Nyota huyo mwenye umri wa miaka 36 anatuhumiwa kumsababishia mtayarishaji wa muziki majeraha ya mwili katika tukio ambalo waendesha mashtaka wamelieleza kuwa “halikuwa na uchochezi wowote”.
Pia anakabiliwa na shtaka la kumiliki silaha hatari — ambayo ni chupa ya kileo.
Mashtaka haya mawili yaliongezwa mwezi uliopita kwenye shtaka la awali, kubwa zaidi, la kujaribu kumsababishia mtu majeraha mabaya ya mwili (GBH), ambalo tayari Bwana Brown alilishatupilia mbali kwa kujitetea kuwa si kweli.
Chris Brown anatarajiwa kufikishwa mahakamani kwa kesi hiyo mwezi Oktoba mwaka 2026.
Waendesha mashtaka wamesema kuwa mhanga wa tukio hilo, Abraham Diaw, alikuwa amesimama kwenye baa ya kilabu cha usiku kilichopo eneo la Soho mnamo tarehe 19 Februari 2023, wakati Chris Brown alimpiga kwa chupa mara kadhaa.
Mwimbaji huyo alikamatwa mwezi Mei katika hoteli ya nyota tano iliyopo Salford, Greater Manchester, baada ya kurejea Uingereza kwa ajili ya maandalizi ya ziara yake ya muziki barani Ulaya.
Alizuiliwa korokoroni kwa takriban wiki moja kabla ya kuachiliwa kwa dhamana baada ya kukubali kulipa ada ya dhamana ya pauni milioni tano (£5m) kwa mahakama.
Ada ya dhamana ni kiasi cha fedha kinachowekwa kama dhamana ya kifedha kuhakikisha mtuhumiwa atarudi mahakamani kwa kesi yake. Brown anaweza kupoteza fedha hizo endapo atakiuka masharti ya dhamana, ambayo yaliendelezwa katika kikao cha mahakama siku ya Ijumaa.
Kwa mujibu wa masharti hayo, Chris Brown anatakiwa kuishi katika anwani iliyopo Uingereza akisubiri kesi hiyo, na aliamriwa kukabidhi pasipoti yake kwa polisi.
Hata hivyo, ameruhusiwa kuendelea na ratiba ya ziara yake ya kimataifa ya Breezy Bowl XX kwa masharti kwamba atakabidhi pasipoti kila anapomaliza safari, na kuirudishiwa anapohitaji kusafiri kwa ajili ya maonesho.
Katika wiki za hivi karibuni, Brown amekuwa akitumbuiza kwenye viwanja na kumbi mbalimbali za burudani kote Uingereza na Ulaya, na kumaliza burudani mjini Paris mwishoni mwa wiki iliyopita. Sehemu ya ziara hiyo inayofanyika Marekani Kaskazini inatarajiwa kuanza baadaye mwezi huu na kufikia tamati tarehe 18 Oktoba.
Kikao kingine cha mahakama kimepangwa kufanyika tarehe 24 Oktoba.
Chris Brown ni miongoni mwa wanamuziki wakubwa zaidi wa R&B nchini Marekani, akiwa mshindi wa tuzo mbili za Grammy na nyimbo 19 zilizofika katika nafasi 10 za juu kwenye chati za Uingereza, zikiwemo Turn Up The Music, Freaky Friday, With You na Don’t Wake Me Up.
Mshitakiwa mwenza, Omololu Akinlolu, raia wa Marekani mwenye umri wa miaka 39 anayefahamika kisanii kama HoodyBaby, naye pia alikana shtaka la kumsababishia mtu majeraha ya mwili. Awali, alikana pia shtaka la kujaribu kusababisha majeraha mabaya ya mwili.
Chanzo: BBC
Entertainment
Justin Bierber Arejea na Album Mpya ‘SWAGG’

Msanii nyota wa muziki wa kimataifa, Justin Bieber, hatimaye ameachia rasmi albamu yake mpya na ya saba kwa jina “Swag”, ikiwa ni albamu yake ya kwanza tangu mwaka 2021 alipotoa Justice. Albamu hii imetoka leo na tayari imeanza kutikisa majukwaa mbalimbali ya muziki duniani.
Swag imejumuisha mastaa kadhaa akiwemo Gunna, Sexyy Red, Cash Cobain, pamoja na wasanii wengine wa kizazi kipya.
Albamu hiyo ina jumla ya nyimbo 20 na tayari baadhi ya vibao kama “Go Baby”, “Soulful” na Butterflies “zimeanza kupokelewa vizuri kwenye mitandao ya Spotify, Apple Music na YouTube.
Hii ni mara ya kwanza kwa Bieber kuachia albamu tangu alipopata matatizo ya kiafya mwaka 2022 yaliyosababisha asitishe ziara yake ya kimataifa ya Justice World Tour ambayo ilikuwa iendelee hadi mwaka 2023.
Ziara hiyo ilisitishwa mnamo Septemba 2022 baada ya Bieber kupatwa na maradhi ya Ramsay Hunt Syndrome, ugonjwa uliomsababishia kupooza upande mmoja wa uso.
Kwa kipindi cha miaka minne bila kazi mpya, mashabiki wa Justin Bieber duniani wamekuwa wakimsubiria kwa hamu ujio wa kazi mpya kutoka kwake. Kupitia Swag, msanii huyo ameonyesha kurejea kwa nguvu na ubunifu wa hali ya juu, huku akiwa katika hali nzuri kiafya na kisaikolojia.
Taarifa na Francos Mzungu