Business
Wahudumu wa Uchukuzi Kilifi Walia na Kupanda kwa Bei ya Mafuta

Siku moja baada ya mamlaka ya udhibiti wa kawi nchini, EPPRA kutangaza kupandishwa kwa bei ya mafuta, sekta ya uchukuzi katika kaunti ya Kilifi inaelezea hofu ya kuathirika kwa biashara zao.
Wahudumu wa tuktuk,teksi, bodaboda na magari ya usafiri wa umma hapa mjini Kilifi wanasema kupanda kwa bei ya petrol na diseli kutaathiri pakubwa sekta hiyo ya uchukuzi.
Sasa wanasema kuwa watalazimika kuongeza nauli kwa abiria kutokana na gharama ya mafuta.
Ni hali ambayo imeathiri wakaazi ambao wanatarajiwa kutumia vyombo hivyo vya usafiri wakisema kuwa watalazimika kutembea kwa mguu kwa safari fupi fupi katika utekelezaji wa shughuli zao za kawaida.
Hatahivyo wametoa wito kwa serikali kuhakikisha kuwa inaingilia kati ili kuona kwamba bei za mafuta zinadhibitiwa.
Haya yamejiri huku lita moja ya mafuta aina ya petrol kaunti ya KIlifi ikiuzwa kwa shilingi 183.88 huku diseli ikiuzwa kwa shilingi 169.16 kila lita.
Lita moja ya mafuta ya taa inauzwa kwa shilingi 153.29.
Business
Mradi wa kiuchumi wa Dongo Kundu wavutia wawekezaji zaidi

Wawekezaji wa ndani na nje ya nchi wanaendelea kuonyesha nia ya kuekeza katika mradi wa kiuchumi wa dongo kundu kaunti ya Mombasa.
Mradi huo unaotarajiwa kuongeza uzalishaji katika viwanda na thamani ya bidhaa ndani ya nchi na nje, unatarajiwa kukamilika hivi karibuni.
Kampuni ya nishati kutoka China, Ruike Energy Group Limited, ni mwekezaji wa hivi karibuni kuonyesha nia ya kupata nafasi ndani ya eneo hilo la kiuchumi la Dongo Kundu kwa ajili ya kuanzisha kiwanda cha kusafisha mafuta.
Kulingana na halmashauri ya bandari nchini KPA hatua hiyo italeta faida Zaidi ikiwemo kubuni nafasi za ajira, ikuaji wa uchumi, upatikanaji wa vifaa vya baharini, na urahisi wa kufikia masoko ya kanda na ya kimataifa.
Taarifa ya Pauline Mwango
Business
KETRACO kuimarisha usalama wa chakula nchini

Shirika la usambazaji umeme nchini, KETRACO, limethibitisha dhamira yake ya kuimarisha usalama wa chakula, ukuaji wa kijani, na ushirikiano wa kieneo kupitia uekezaji mkubwa katika miundombinu ya umeme.
Katika maonesho ya Kimataifa ya kilimo ASK yanayoendelea kaunti ya Mombasa, KETRACO imeonyesha jinsi miundombinu yake ya umeme inavyowezesha kilimo cha kisasa na uzalishaji wa viwandani.
Kwa mujibu wa kaimu mkurugenzi mkuu, mhandisi Kipkemoi Kibias, KETRACO imekamilisha miradi 43 ya njia za kusafirisha umeme, huku mingine 29 ikitarajiwa kukamilika ifikapo mwaka 2028.
Kibias, alisema shirika hilo tayari limejenga zaidi ya kilomita elfu sita za njia za umeme wa msongo mkubwa, likiwa pia na vituo 46 vya kusambaza umeme na upanuzi wa mitambo 33.
Katika eneo la Pwani, Kibias alisema upanuzi wa mpango wa Green Energy Backbone umewezesha usambazaji wa kawi safi kwa asilimia 93, jambo lililopunguza utegemezi wa mafuta na kuchochea maendeleo ya biashara za kilimo, utalii na uchumi wa baharini.
Kibias alisema KETRACO inaendelea kuwekeza katika teknolojia za kisasa na kuunganisha Kenya na nchi jirani kupitia njia za kimataifa kama zile za Ethiopia, Tanzania na Uganda hatua zitakazowezesha biashara ya umeme Afrika Mashariki.
Taarifa ya Mwanahabari wetu