Business
Wahudumu wa Uchukuzi Kilifi Walia na Kupanda kwa Bei ya Mafuta

Siku moja baada ya mamlaka ya udhibiti wa kawi nchini, EPPRA kutangaza kupandishwa kwa bei ya mafuta, sekta ya uchukuzi katika kaunti ya Kilifi inaelezea hofu ya kuathirika kwa biashara zao.
Wahudumu wa tuktuk,teksi, bodaboda na magari ya usafiri wa umma hapa mjini Kilifi wanasema kupanda kwa bei ya petrol na diseli kutaathiri pakubwa sekta hiyo ya uchukuzi.
Sasa wanasema kuwa watalazimika kuongeza nauli kwa abiria kutokana na gharama ya mafuta.
Ni hali ambayo imeathiri wakaazi ambao wanatarajiwa kutumia vyombo hivyo vya usafiri wakisema kuwa watalazimika kutembea kwa mguu kwa safari fupi fupi katika utekelezaji wa shughuli zao za kawaida.
Hatahivyo wametoa wito kwa serikali kuhakikisha kuwa inaingilia kati ili kuona kwamba bei za mafuta zinadhibitiwa.
Haya yamejiri huku lita moja ya mafuta aina ya petrol kaunti ya KIlifi ikiuzwa kwa shilingi 183.88 huku diseli ikiuzwa kwa shilingi 169.16 kila lita.
Lita moja ya mafuta ya taa inauzwa kwa shilingi 153.29.
Business
Muungano wa bodi za leseni za vileo wapinga sera ya NACADA

Muungano wa bodi za kudhibiti na kutoa leseni za vileo nchini umepinga vikali pendekezo la Sera ya Mwaka 2025 ya Mamlaka ya Kudhibiti Matumizi ya Pombe na Dawa za Kulevya (NACADA), wakidai kuwa linaenda kinyume na ugatuzi na kuondoa mamlaka ya kikatiba ya serikali za kaunti katika usimamizi wa biashara ya vileo.
Wakizungumza mjini Diani kaunti ya Kwale, wanachama wa Muungano huo wakiongozwa na Mwenyekiti wao, Julius Owino, walisisitiza kuwa serikali za kaunti ndizo zenye jukumu la kisheria na kikatiba la kutoa leseni, kusimamia, na kutekeleza sheria zinazohusu uuzaji wa pombe.
“Sera hii ya NACADA ni jaribio la kuingilia majukumu ya kaunti na itaathiri mapato ya serikali za kaunti, kaunti lazima zisalie na mamlaka kamili ya kusimamia biashara ya vileo kama ilivyowekwa katika Katiba,” alisema Owino.
Owino pia aliitaka NACADA kushirikiana na kaunti kwa njia ya mashauriano badala ya kujaribu kuchukua majukumu yao, akiongeza kuwa ushirikiano thabiti ndio utaleta mafanikio katika udhibiti wa pombe na dawa za kulevya.
Kauli yake iliungwa mkono na Richard Osongo, Mwenyekiti wa wamiliki wa baa katika kaunti ya Kwale, ambaye alitoa onyo kali dhidi ya kile alichokiita “unyanyasaji wa mamlaka za kaunti na NACADA.”
Muungano huo ulieleza kuwa utatoa mapendekezo rasmi kwa serikali ya kitaifa na kuhimiza mjadala wa wazi kabla ya utekelezaji wowote wa sera hiyo mpya.
Taarifa ya Elizabeth Mwende
Business
Wavuvi Kwale wadai kuhangaishwa na wavuvi wa Tanzania

Wavuvi kaunti ya Kwale walalamikia kukandamizwa na wavuvi kutoka taifa jirani la Tanzania kufuatia mizozo ya mipaka.
Kulingana nao wavuvi hao, wamekua wakinyanyaswa na hata kutozwa faini ya hadi shilingi milioni 4 wanapopatikana wakivua katika sehemu zinazodaiwa kuwa katika nchi ya Tanzania na maafisa hao.
Juma Rama Yusuf mwenyekiti wa wavuvi eneo la Jimbo na mwenzake wa Vanga Ngoto Mohamed walisema kuwa wavuvi wa Tanzania wamepewa uhuru wa kutekeleza shughuli za uvuvi humu nchini ili hali wenyeji wanahangaika.
Aidha waliitaka serikali ya Kenya na ile ya Tanzania kuja pamoja na kutatua swala la mipaka katika bahari hindi ili kukomesha mizozo ya mara kwa mara inaoshuhudiwa kati ya wavuvi wa Kenya na maafisa walinda bahari kutoka Tanzania.
Taarifa ya Pauline Mwango